Jihadhari, Kukopa au kukopesha ni hatari!
PENGINE kichwa cha habari cha makala hii,
kinaweza kukupa maswali mengi, lakini huo ndiyo ukweli katika dunia ya sasa.
Wakati fulani nikifanya kazi katika taasisi moja binafsi, tulikuwa katika
mkutano wa kawaida kati yetu waajiriwa na mwajiri, kijana mwenzetu wa
Kitanzania ambaye alibarikiwa.
Alikuwa na kawaida ya kututia moyo, kwamba
tukitaka kufanikiwa katika maisha, lazima tufanye kazi kwa bidii, lakini
tukilenga kujiajiri. Hatuwezi kutajirikia katika kazi yake, kitu ambacho
tulimshangaa sana kwani si waajiri wengi huwafumbua macho watu waliowaajiri.
Katika mazungumzo hayo hata hivyo, alitueleza
kuwa na katika kuutafuta utajiri, kamwe hatuwezi kuupata bila kupata mikopo.
Iwe kutoka kwa watu binafsi au taasisi, kwa sababu katika kukua kibiashara,
kunahitaji uwekezaji mkubwa.
Yes, watu wanakopa iwe katika taasisi kubwa za
kimataifa, za kitaifa na hata taasisi ndogo ndogo zilizosajiliwa na watu
binafsi, kila mmoja akiwa na vigezo vyake kulingana na eneo na kiwango cha
hela. Watu binafsi, ambao mara nyingi huwa na masharti nafuu kuliko taasisi,
wana riba kubwa.
Wanakuwa na riba kubwa kwa sababu ya risk kubwa
waliyonayo katika kurejesha fedha zao kwa sababu kwanza wanafanya kinyume cha
sheria, ni rahisi kurukwa. Maana hata kama mnaweza kuandikishana, lakini
aliyekopesha atakapokwenda mahakamani, atashindwa kwa sababu sheria haimpi
mamlaka ya kukopesha.
Hii inafanya mikataba ya kukopeshana inayoingiwa
baina ya watu binafsi, mara nyingi inakuwa ni ya ujanja ujanja, ambayo inambana
mkopaji kiasi kwamba ni bora alipe anachodaiwa kuliko kupelekana mahakamani.
Lakini kwa nini ninasema kukopa ni hatari na ni
kifo? Hii inatokana na matukio ambayo nimeanza kusimuliwa kwa miaka mingi na
ambayo baadhi ya simulizi hizo ninawajua wahusika. Na si tu kukopa, bali ni
hatari kwako pia hata kukopesha.
Wakati flani enzi za kusoma shule za msingi,
niliishi Singida. Kwa udogo wa mji ule, ilikuwa ni rahisi kuwafahamu
wafanyabiashara, wahindi, waarabu na hata wazawa. Sasa baada ya miaka mingi ya
kuhama kutoka kule na kujichanganya kwenye maeneo mengine, siku moja nikakutana
na rafiki yangu wa enzi hizo.
Stori nyingi za Singida, mara unamkumbuka yule,
huyu na flani? Katika kukumbushana, tukafika kwa mfanyabiashara mmoja ambaye
alikuwa na tabia ya kutoa pipi kwa watoto, kila tukienda kununua chochote
dukani kwake miaka hiyo, akasababisha watoto kuwa wengi dukani kwake. Jamaa
akasema ‘walimuua bwana..’!
Ilikuaje? Jamaa alikua na kawaida ya kuwakopesha
wafanyabiashara wadogo bidhaa kwa mali kauli, wao wanaenda kuuza minadani
halafu mwisho wa wiki wanamlipa, wanachukua mzigo mpya. Sasa inadaiwa kuna
jamaa walichukua mzigo mkubwa, kulipa wakaona tabu. Kwa hiyo ili kurahisisha,
wakapanga njama, usiku wakamvamia na kumuua!
Kesi hizi ziko nyingi kutokana na simulizi.
Lakini si kuua tu, wengine wanakopesha lakini hawana wema na wewe. Kuna watu
wanakukopesha kwa mfano, unaweka dhamana labda kibanda chako (nyumba). Muda wa
kulipa ukifika, mkopeshaji hapatikani kwa simu wala kazini au nyumbani kwake.
Halafu baada ya wiki mbili au mwezi mbele, anaibuka na kudai hataki hela, ila
kwa kuwa umekiuka mkataba, anataka nyumba.
Mtavutana lakini kwa kuwa hawa watu wana
mitandao, wanashinda kesi na kujikuta umeuza nyumba yako yenye thamani ya
milioni 50 kwa milioni tano tu labda. Na wengine, ingawa hili ni la kiimani
zaidi, wanadai unakopeshwa, halafu muda wa kulipa ukikaribia, unarogwa, ama
unasahau kulipa, au unapata upungufu wa afya ya akili!
Sasa hiyo ni kukopa. Hali iko hivyo pia kwa
kukopesha. Unampa mtu, ambaye mara nyingi ni yule unayemuamini, kiasi kikubwa
cha fedha ukiamini atarejesha, lakini bahati mbaya, ama mambo yanakwenda kombo
au kwa sababu tu ya tamaa, anaona bora akuue ili awe huru!
Nimeandika hivi kwa sababu kuna habari imetokea
siku mbili hizi zilizopita kule Afrika Kusini imeniuma sana. Kuna Mtanzania
mmoja alikuwa na makazi yake nchini Msumbiji, akifanya shughuli zake. Wanasema
ni mwenyeji wa Kinondoni Dar es Salaam.
Sasa kwa namna wanavyosema, alikuwa amemkopesha
Mtanzania mwenzake mmoja ambaye yeye alikuwa anaishi Johannesburg, Afrika
Kusini. Katika kudaiana, yule mdaiwa, akamwambia mdeni wake aende Sauzi, ili
akampatie chake.
Kufika kule akawasiliana na mkewe aliyemuacha
Msumbiji kuwa amefika salama, lakini baada ya hapo hakupatikana tena hadi siku
tatu baadaye mwili wake ulipopatikana katika moja ya hospitali jijini humo,
akiwa amepigwa risasi na watu wasiojulikana.
Ni ngumu kusema aliyemkopesha ndiye aliyemuua
kwa sababu hakuna uthibitisho, lakini ni rahisi kupata dhambi ya kuunganisha
doti na kuweze kumhisi.
Katika maisha haya ni vigumu kuishi bila mikopo,
lakini ni kitu cha msingi sana kuwa makini na kiasi cha mikopo tunayokopa au
kukopeshwa, maana wakati mwingine badala ya kutusaidia ili kupunguza ukali wa
maisha, inatufanya kuwa ndicho chanzo cha kupoteza kabisa maisha.
Kama ni lazima, ni vyema kukopa kiwango kidogo
cha fedha ambacho kwanza hautashindwa kukilipa hata kama ni kidogo kidogo,
lakini pia hata mkopeshaji wako hawezi kutetereka kwa wewe kushindwa kulipa
deni. Ingawa hata hivyo, kiwango kidogo cha deni unalodaiwa haiwezi kuwa sababu
tosha ya kutopata madhara kwa kushindwa kulipa.
Ushahidi wa matukio ya watu kupigana visu na
mapanga, hasa jijini Dar es Salaam kwa sababu ya kudaiana shilingi mia moja au
mia mbili unathibitisha hili. Kitu cha msingi kabisa katika kukabiliana na
madeni unayodaiwa, ni kuwa na lugha ya kunyenyekea kwa mdeni wako. Haipendezi,
unadaiwa halafu unatoa lugha inayompa hasira mdeni wako kama vile..”nini bwana
weee, hela yenyewe shin’ ngapi unanisumbua?”
Hizi ni lugha ya kupandishana presha. Yaani uje
kwangu mikono nyuma uombe nikukopeshe elfu kumi, halafu kesho nikufuate unilipe
unipe majibu kama haya, yanaleta hasira. Kwa hiyo lugha, hasa ya staha ni
silaha ya kwanza kuitumia kwa mtu anayekudai. Unyenyekevu katika kulizungumzia
deni lako linamfanya hata anayekudai aamini unachomwambia, hata kama yeye
atapanda juu kwa hasira.
Kwa wale tulio na baraka za kuweza kuwakopesha
wengine, siyo kila mkopaji ni mwema kwako, hata kama ni rafiki yako kipenzi,
ndugu au jamaa unayemuamini. Imethibitika mara nyingi kwamba fedha ni shetani
asiye na wema, kwani hata baadhi ya watoto hupanga njama za kuwaua wazazi wao
ili warithi mali mapema!
Kopesha kwa kiasi, dai kwa staha. Kitu salama
kabisa, ni kuepuka kukopesha. Kama umebarikiwa kuwa na ziada, ni bora kutoa
misaada kuliko kukopesha kibinafsi. Vinginevyo, sajili taasisi, kwani deni la
taasisi halifi.
Vivyo hivyo, ni bora kukopa kwenye taasisi
zilizosajiliwa kuliko kwenda kwa mtu binafsi. Watu wa benki hawawezi kupanga
njama za kukudhuru kwa sababu fedha ile haina mwenyewe, sana sana watakupeleka
mahakamani ambako utashinikizwa kulipa kwa mujibu wa sheria.

Post a Comment