HOMA YA MARBURG TANZANIA: WHO KUTUMA TIMU YA DHARURA YA WATAALAMU KAGERA

Shirika la Afya Duniani (WHO) linatuma timu ya dharura mkoani Kagera nchini Tanzania kufanya uchunguzi zaidi wa magonjwa ya mlipuko kufuatia mlipuko wa ugonjwa wa Virusi vya Marburg (MVD) wa kwanza kabisa nchini humo.

Dkt. Matshidiso Moeti, Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika alisema juhudi za mamlaka za afya za Tanzania kubaini chanzo cha ugonjwa huo ni kielelezo tosha cha dhamira ya dhati ya kukabiliana na mlipuko huo.

"Tunafanya kazi na serikali kuongeza kasi ya hatua za kudhibiti na kukomesha kuenea kwa virusi na kumaliza milipuko haraka iwezekanavyo," alisema katika taarifa iliyotolewa Machi 21, 2023.

Timu ya dharura ya wataalamu wa WHO itaangazia kutafuta visa katika jamii na vituo vya afya vya mkoa huo ili kubaini muingiliano zaidi na kutoa huduma zinazofaa.

Wizara ya Afya nchini Tanzania ilithibitisha kutokea kwa mlipuko wa ugonjwa huo katika Wilaya ya Kanda ya Ziwa ya Bukoba Jumanne tarehe 21 Machi 2023, takribani siku 4 baada ya taarifa za "ugonjwa usiojulikana" kusambaa na kuua watu watano akiwemo mhudumu wa afya.

Watu hao kabla ya kufariki walipatwa na dalili za homa, kutapika, kutokwa na damu kutoka sehemu mbalimbali za mwili na figo kushindwa kufanya kazi. Serikali inasema kwa sasa inafuatilia watu 160 ambao wanaweza kuwa walichangamana na watu walioambukizwa.

 


 

No comments