WANANCHI NAMTUMBO WATAKA TAARIFA YA MAPATO NA MATUMIZI


FULL AUDIO: Ofisi ya Kijiji Yapigwa Kufuli.....Wananchi wacharuka | EDDY  BLOG | Edwinmoshi Official Blog

NA STEPHANO MANGO, NAMTUMBO

BAADHI ya wananchi katika Kijiji cha Mchomoro kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo Mkoani Ruvuma wamemtaka Mwenyekiti wa Kijiji hicho ,Mtendaji wa kijiji na Mhasibu wa kijiji hicho kuitisha mkutano wa hadhara na kuwasomea mapato na matumizi ili kuwepo na uwazi wa fedha za wananchi

Wakizungumza na timu ya waandishi wa habari waliotembelea kijiji hicho jana walisema kuwa ni haki yao kupata taarifa ya maendeleo ya kijiji ikiwa ni pamoja na taarifa za mapato na matumizi ya fedha ambazo zinatokana na michango yao na fedha kutoka Halmashauri.

Mmoja wa wanakijiji hicho, Faraji Said alisema kuwa toka viongozi hao wa kijiji wachaguliwe mwaka 2019 wameshindwa kufanya mkutano wa hadhara na kuwasomea mapato na matumizi kwa sababu ambazo wanazijua wenyewe hali ambayo inaleta mashaka katika matumizi ya fedha za wananchi.

Said alisema kuwa ipo mikutano ya dharura na mikutano ya kuidhinishiwa matumizi ya fedha ambayo imekuwa ikiitishwa kwa lengo lake binafsi mwenyekiti na wenzake na kulazimisha ajenda kuwa moja bila kupata ufafanuzi hali ambayo imekuwa ikizorotesha maendeleo ya kijiji.

“Akiitisha mkutano basi ujue kuwa anataka kuomba fedha za kuendeshea ofisi au anataka kupata baraka za kuwafukuza wafugaji jamii ya wasukuma ambao hawajampa fedha ambazo alikuwa anazitaka kutoka kwa wasukuma hao ambao wamekuwa wakilisha mifugo yao katika maeneo ya kijiji”alisema Said.

Alisema kuwa jamii ya wanamchomoro wanahitaji kupata haki zao lakini wamekuwa wakikwamishwa na uongozi mbovu wa kijiji hicho ambao umekuwa ukijali zaidi maslahi yao badala ya maslahi mapana ya wananchi.

Naye Adam Chake alisema katika kijiji hicho walifanikiwa kujenga boma la Zahanati mwaka 2019 ambapo Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Chiristine Mdeme alipotembelea ujenzi huo aliahidi Kutoa milioni moja, na hayati Rais Dk John Magufuli aliahidi Kutoa milioni 100/= pia jumuiya ya hifadhi ya Mbarang’andu nao waliahidi Kutoa milioni 8.947/= lakini mpaka sasa hatujapata taarifa kuhusu ujio wa fedha hizo au matumizi yake.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji hicho Said Mohamed Mkalela alisema kuwa madai hayo siyo ya ukweli na kwamba amepanga kufanya mkutano wa robo mwaka hivi karibuni ili kuweza kutolea ufafanuzi.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Namtumbo Evance Nachimbiya alisema kuwa katika vikao vyake na viongozi wa vijiji na watendaji wa Halmashauri hiyo alielekeza kutatua kero za wananchi kwa wakati na Kutoa taarifa za utendaji kazi kwa wananchi ili wananchi waweze kufahamu serikali yao inachofanya.

Nachimbiya alisema kuwa kuwasomea mapato na matumizi wananchi ni haki yao na sio jambo la msaada kwa sababu hizo ni fedha zao kwani kutokufanya hivyo ni kwenda kinyume na kanuni na sheria na hatua zinachukuliwa ili kubaini ukweli wa madai ya wananchi kabla ya sheria kuchukua mkondo wake.

 



No comments