WANAJUMUIYA YA MBARANG’ANDU WAIOMBA TAKUKURU KUCHUNGUZA MAPATO NA MATUMIZI YAKE


Salum Hamduni ateuliwa kuwa mkurugenzi mkuu wa TAKUKURU


NA STEPHANO MANGO, NAMTUMBO

WANANCHI ambao wanaizunguka jumuiya ya uhifadhi ya Mbarang’andu iliyopo wilayani Namtumbio mkoani Ruvuma wameiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) kuchunguza mapato na matumizi ya jumuiya hiyo kwa kipindi cha miaka mitano ili kuwepo na uwazi katika uendeshaji wa Jumuiya hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa uchaguzi wa wajumbe wapya wa jumuiya hiyo kutoka katika vijiji ambavyo vinaunda Jumuiya hiyo vya Mchomolo, Kitanda, Likuyuseka Maganga, Kilmasela, Nambecha, Songambele na Mtelemwahi, walisema wanashangaa kuitishwa kwa uchaguzi bila wale ambao wanamaliza muda wao kusoma taarifa ya utendaji kazi wa miaka mitano iliyopita.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Kitanda, Abdul Andunje alisema kuwa Jumuiya hiyo ni taasisi hivyo ina mali na madeni ambayo wamekuwa wakidaiwa na taasisi mbalimbali hivyo ni vyema taarifa ya mapato na matumizi ya jumuiya hiyo ikatolewa kwa uwazi ili unapofanyika uchaguzi mpya ikaeleweka utendaji kazi wa wajumbe ambao wanamaliza muda wao.

Andunje alisema kuwa ni kitu cha ajabu kuitisha uchaguzi bila kuelewa kwa kina kilichofanyika katika miaka mitano iliyopita ili kujua mali zilizopo na kinachodaiwa na sababu zake za kuwepo kwa hali hiyo.

Alisema kuwa kuruhusu uchaguzi bila kujua utendaji kazi wa wajumbe waliopita katika miaka mitano ni kuruhusu mianya ya ubadhirifu na wizi katika jumuiya hiyo ambayo imekuwa kivutio kikubwa cha watalii kutoka nchi za Ulaya na Marekani ambao wanatembelea jumuiya hiyo na kufanya shughuli za uwindaji.

Naye Erasto Gama kutoka katika kijiji cha Songambele alisema kuwa zipo shughuli za utalii na uwindaji ambao unafanyika katika Jumuiya hiyo ambazo zinaiingizia Serikali mapato na tozo mbalimbali hivyo ni muhimu uwazi ukawepo na wananchi kujua ukweli huo kwa sababu ni mali yao.

Gama alisema kuwa wajumbe ambao wanamaliza muda wao yapo ambayo wameyafanya katika utendaji kazi wao wa kipindi cha miaka mitano ambayo yanatakiwa yasemwe ili kuwapa fursa wananchi kujua kilichofanyika kwenye Jumuiya yao kitendo cha kuitisha uchaguzi bila kutolewa taarifa kinazua taharuki kwa sababu nyuma yake kuna vitu vinafichwa.

Alipotafutwa Afisa Ardhi  na Maliasili wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Saimon Sambalu ili aweze kuelezea kwa kina kinachodaiwa na wanajumuiya hakuweza kupatikana kwa madai kuwa alikuwa vijijini kikazi.

Hata hivyo kwa upande wake Afrikanus Challe ambaye ni Afisa Maliasili na Utalii wa Mkoa wa Ruvuma alisema kuwa kabla ya baraza la Jumuiya kuvunjwa kunatakiwa kuitishwe mkutano maalum ambao ajenda yake kubwa itakuwa kupeana taarifa za utendaji kazi na kuvunjwa kwa baraza.

Challe alisema kuwa kwa sasa taarifa ambayo anayo ni mchakato wa uchaguzi katika vijiji ambavyo vinaunda Baraza la Jumuiya hiyo, sasa kama kuna dosari zozote katika uundwaji wake ni lazima zifanyiwe kazi kwa uwazi na ukweli ili kuondoa makando kando hayo na kwamba analifuatilia jambo hilo na kuahidi kulitolea ufafanuzi .

 

 

No comments