Wanafunzi Saba wahofiwa kupoteza Maisha baada ya School Bus kuanguka kwenye korongo (Sinoni, Arusha)

 

Wanafunzi Saba wanahofiwa kupoteza maisha baada ya gari la Shule ya Msingi Ghati Memorial kuanguka kwenye korongo linalopitisha maji Mitaa ya Dampo, Sinoni.

Inadaiwa chanzo ni dereva kushindwa kulidhibiti gari alipofika eneo la tukio kutokana na mvua kubwa iliyonyesha kuanzia usiku hadi alfajiri ya leo Aprili 12, 2024.

Taarifa kutoka eneo la tukio imedaiwa Wanafunzi saba hawajulikani walipo, Watatu wameokolewa na mwili mmoja umepatikana, Dereva wa gari naye ameokolewa na yupo chini ya ulinzi.

JamiiForums ilipomtafuta Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, SACP Justine Masejo amesema “Nipo kwenye msafara, ila hizo taarifa nimezipata, kikosi cha Uokozi nipo eneo la tukio na Wanafunzi saba hawajulikani walipo wengine wameokolewa, taarifa kamili tutaitoa baadaye.”


WANANCHI WASHIRIKI KUTAFUTA WATOTO WALIOKUWA KWENYE ‘SCHOOL BUS’
Diwani wa Kata ya Sinoni, Michael Kivuyo amesema Wananchi wakishirikiana na Kikosi cha Uokozi wanashiriki zoezi la kutafuta Wanafunzi Saba ambao hawajulikani walipo baada ya Gari la Shule walilopanda kuanguka kwenye korongo, Asubuhi ya leo Aprili 12, 2024.

Amesema “Waliokuwa kwenye gari ni Wanafunzi 11, Dereva na Matroni. Wanafunzi Watatu, Dereva na Matroni wameokolewa, mwili mmoja umepatikana, Wananchi wameingia mtoni, wengine wamepewa usafiri kufuata uelekeo wa mto ili kuwatafuta ambao hawajapatikana.”

Aidha, inadaiwa Dereva wa ‘School Bus’ alipofika eneo la tukio alionywa na Bodaboda kutopita wakimsisitiza kuwa kasi ya maji ni kubwa, akalazimisha kupita akiwaambia alipita hapo awali, baada ya ajali na dereva kuokolewa, Bodaboda hao wakaanza kumshambulia kwa kumpiga, akaokolewa na Wasamalia wema.


No comments