Serikali yadhamiria kuimarisha Uwanja wa Ndege Julius Nyerere

 

Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imekusudia kuuimarisha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa  Julius Nyerere (JNIA) uliopo mkoani Dar es Salaam, ili uwe kitovu cha usafiri wa anga kwenye Ukanda wa Afrika Mashariki.

Amesema ili kufanikisha jambo hilo Serikali imepanga  kuufanyia ukarabati uwanja namba mbili (terminal 2) uliopo JNIA. 

Akizungumza mkoani Dar es Salaam wakati wa  mapokezi ya ndege mpya aina ya Boeing B 737-9 Max iliyowasili nchini ikitokea  Seattle, Marekani,  Majaliwa amesema uwanja wa ndege  namba mbili wa JNIA utakapokamilika utakuwa mahususi kwa  ndege zinazofanya safari zake ndani ya  Tanzania.

Amesema uwanja huo namba mbili utasaidia kuongeza miruko ya ndege na safari  hasa za kwenda katika masoko mbalimbali.

Waziri Mkuu  ameziagiza taasisi zote zinazotoa huduma katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere kuboresha huduma zao li kuvutia wateja na kuufanya uwanja huo kutoa huduma bora katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.

No comments