MZEE PAUL KIMITI AUNGA MKONO MASHAMBA MAKUBWA YA SAMIA

Mwenyekiti wa Taasisi ya Kumbukizi ya Mwalimu Nyerere, amesifu mpango wa Serikali wa kuanzisha mashamba makubwa maarufu kama Buld Better Tomorrow.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, mzee Kimiti alisema mpango kama huo uliwahi kubuniwa na aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Sokoine na Mwalimu Nyerere walianzisha mfuko kuanzia mwaka 1983 hadi 1988, ingawa wazo hilo halikufikiwa kwa vile alifariki mapema.

Mzee Kimiti aliwataka vijana kuwa wawajibikaji katika kila sekta lakini pia kujenga utamaduni wa kupenda kilimo.

Alisema katika mpango huo, Sokoine alijitolea kutoa nusu ya mshahara wake ili kuwezesha jambo hilo, kwani kwa mazoea, watu wanaolima hapa nchini ni wazee badala ya vijana ambao ndiyo wenye nguvu.

Jana, Rais Samia Suluhu Hassan alizindua mpango kamambe wa mashamba makubwa huko Chinangali Dodoma, ambako vijana wapatao 800 watapewa mafunzo kwa miezi minne kabla ya kukabidhiwa mashamba hayo ili walime.

Aidha, sambamba na uzinduzi huo, pia Rais Samia alikabidhi magari na mitambo kwa Tume Maalum itakayosimamia mashamba hayo na kumtaka Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe kuhakikisha fedha zinazotolewa kwenye mpango huo hazitumiwi kwa matumizi mengine.

Mzee Kimiti licha ya kuwahi kuwa Waziri na Mkuu wa Mikoa kadhaa wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere pia alikuwa ni mtaalam wa kilimo aliyesomea nchi mbalimbali duniani.

 


 

No comments