MTOTO WA SUNDAY MANARA ANAUMIZWA NA NINI?

VIJANA wa kizazi
cha Bongo Fleva leo hii ukiwaambia kuwa kuna walemavu wawili waliwahi kuwa
mastaa wa huu muziki huko nyuma watakataa katakata, lakini sisi ambao
tuliushuhudia ukihama kutoka hatua moja kwenda nyingine, tunawajua Mabaga
Fresh!
Sawa na mashabiki
wa soka wa enzi hizi ambao wanadhani Haji Manara ni maarufu kuliko alivyokuwa
baba yake, Sunday Manara 'Computer'.
Sisi wa enzi hizo
tunapendelea zaidi kumuita Mtoto wa Sunday Manara, hasa anapofanya jambo zuri
au baya, kwa sababu enzi tukiimba jina la baba yake, yeye alikuwa sawa tu na
watoto wengine tusiowajua majina wa gwiji huyo wa soka ambaye alipewa jina la
utani la kifaa ambacho ni Watanzania wachache mno walikuwa wakikifahamu miaka
hiyo!
Haji Manara si mtu
wa kwanza kutoka Simba kwenda Yanga katika ngazi ya uongozi. Alianza Super
Coach, Syllersaid Mziray, miaka ile ya mwanzoni mwa tisini akafuata Senzo
Masingisa miaka miwili iliyopita, kama kumbukumbu zangu zipo sawa!
Kama kuna siku
Mziray (Mwenyezi Mungu mpatie mapumziko ya amani) aliwahi kuisema Klabu ya
Simba kwa waliyomtenda, basi nadhani itakuwa ni ile siku anatoa sababu za
kujiunga na Yanga.
Vivyo hivyo, tangu
ajiondoe Simba, aliyekuwa CEO wao, Senzo amekuwa, mara nyingi, akikwepa
kuizungumzia Simba kwa mabaya.
Lakini hali ni
tofauti sana kwa huyu mtoto wa Sunday Manara. Tatizo liko wapi? Niliwahi kusema
hapo kabla kuwa Haji hakupenda kuondolewa katika ile nafasi yake ya ubosi wa kitengo
cha habari na siku zote alilalamikia njama zilizokuwa zikifanywa ile aondolewe.
Kwangu, kuna tatizo
lingine ninaliona kwa Haji. Licha ya kuchukizwa na kitendo cha kuondolewa,
lakini pia alihisi, yeye ni maarufu kuliko Klabu ya Simba, kiasi aliamini kuwa
akiondoka, mambo yatavurugika Msimbazi.
Aliamini ataondoka
na wafuasi na kusababisha 'rabsha' kutoka kwa mashabiki. Utulivu uliopo Simba
katika ishu yake unamtesa. Ndiyo maana, badala ya kuifanya vyema kazi yake ya
Uhamasishaji Yanga, kila mara anaizungumzia Simba.
Sasa amefikia hatua
ya kusema ataipeleka Simba Mahakamani kudai fidia kwa kufanyishwa kazi bila
mkataba. Of coz hiyo ni haki yake ya msingi, lakini ilikuwa ni lazima aseme
hadharani?
Kwanza kwa kusema
alifanyishwa kazi miaka sita bila mkataba, anajaribu kutuaminisha kuwa ni jinsi
gani yeye alikuwa radhi kuifanya kazi ile bure, ili mradi tu yupo Simba. Alijua
hatari ya kudai mkataba na yeye hakuwa tayari kukabili matokeo yake!
Kwa sisi tunaovijua
kidogo klabu hizi mbili za Kariakoo, ni heri uwe mbeba jezi wa Simba na Yanga
utapata maslahi makubwa kuliko kuwa Meneja wa timu yoyote ya Ligi Kuu, labda
ukiondoa Azam.
Haji alipenda
kuwepo na malumbano katika media baina yake na viongozi wa Simba. Lakini
pengine kwa kufahamu udhaifu wake, wameamua kukaa kimya bila kujibu
anachokisema, kitu ambacho kinamuumiza zaidi. Anatamani siku moja kiongozi
amjibu, lakini kitendo cha kumkalia kimya ni kama kumdharau.
Ushauri wangu kwa
Haji, angeachana na Simba, ni kubwa sana kwake. Kama ana madai, aende huko
mahakamani kimyakimya, lakini kwa yeye kujaribu kujipima ubavu na klabu hii,
anajidanganya.
Hakuna, narudia
tena, hakuna mtu binafsi aliyejaribu kuweka msuli wake kwa klabu hizi mbili
akafanikiwa. Mzee Hamis Kilomoni anaweza kuwa shahidi kwa Simba au ndugu yangu
Magoma kule Yanga.
Patrick Rweyimamu
aliyewahi kuondolewa umeneja Simba alikuwa na madai pia na klabu hiyo, lakini
uliwahi kumsikia akizunguka katika vituo vya redio akiiponda?
Antonio Nugaz
aliyeondolewa Yanga, unadhani amekifurahia kitendo hicho cha kuwekwa pembeni pale
Jangwani? Mbona humsikii kwenye mitandao akilalamika. Au unafikiri hajui kuwa
kuna watu flani ndiyo walisimamia ishu ya yeye kutoswa?

Post a Comment