ASANTE LENGAI OLE SABAYA

LENGAI Ole Sabaya,
aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, amehukumiwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha
kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyang'anyi wa kutumia silaha. Pamoja
naye, wapo wengine wawili.
Katika hali ya
kawaida ya kibinadamu, hili la kufungwa siyo jambo ambalo ungependa mwenzako
limtokee, hasa kwa uwingi wa miaka aliyohukumiwa, ingawa pia haipendezi mtu
anapovunja sheria ambayo kimsingi alipaswa kuisimamia.
Sitapenda kuingia
kwa undani juu ya kile alichokifanya, kwa sababu tayari mahakama imejiridhisha,
pasipo shaka kuwa alifanya jinai. Hata hivyo, anayo haki ya kukata rufani na
nani anajua, anaweza kushinda na kurejea uraiani.
Lakini vyovyote
itakavyokuwa, Sabaya ametupatia somo moja kubwa sana ambalo wala hauna haja ya
kuwa na Shahada ya Uzamivu ili kulielewa vyema. Linaeleweka kirahisi kabisa,
ili mradi tu, ukubali kwamba ni somo.
Katika umri wake wa
miaka 34, dogo alifikia levo za juu kabisa kiasi kwamba alikuwa mmoja kati ya
'Untouchables' wachache tuliobarikiwa kuwa nao hapa nchini.
Akiwa DC tu, (yes,
Mkuu wa Wilaya ni mtu mdogo tu kimuundo serikalini, licha ya ukweli kuwa ni
mwakilishi wa Rais katika eneo lake. Juu yake kuna watu wengi kabla hajamfikia
aliyemteua), Sabaya alikuwa na nguvu za ajabu!
Kama uliifuatilia
vizuri kesi yake, kuna mambo alikuwa anafanya kwa sababu tu alikuwa shahiba wa
Rais. Binafsi, niliwahi kumsikia akihojiwa siku chache kabla hajakamatwa,
akijisifu kuwa alikuwa na uwezo wa kumpigia Rais Magufuli simu hata saa nane za
usiku.
Can You Imagine!
Kwa namna nilivyokuwa nikimfuatilia marehemu Magufuli, ninaamini kabisa wapo
mawaziri ambao hawakuthubutu kumpigia mida hiyo.
Achana na
alichokuwa akiongea naye, nazungumzia tu hiyo fursa! Katika kipindi kile, wenye
fursa hizo walikuwa wachache na bahati nzuri, wengi wao wanafahamika.
Sabaya alijisahau,
akaamini mambo yatakuwa vile milele, hakuweza hata kujikumbusha kuwa baadhi ya
matendo yake yalikuwa ni jinai na wanasheria wanasema jinai haifi!
Kwa nini ninasema
Asante Sabaya? Ninasema hivi kwa sababu watu wa aina yake wapo wengi, siyo tu
wale walioko serikalini, lakini hata kwenye taasisi za umma na binafsi.
Vyeo hivi ni kama
makoti ya kuazima, muda wowote mwenye lake atakuja kulichukua, tena bila
kulazimika kukutaarifu ili angalau ulifue.
Wapo watu wenye
hizo nafasi za kufanya maamuzi au kutoa maelekezo, wanasahau kwamba ipo siku
watakuja wengine kukaa hapo walipo.
Wamejaa dharau,
viburi na jeuri ya madaraka. Wanajiona wao kama watu spesheli hivi, kwamba
hakuna zaidi yao. Wapo baadhi yao, wanaogopwa na kunyenyekewa kuliko hata
waliowateua kukamata nafasi hizo.
Yes, ukiwa na
nafasi, hasa ya uongozi, lazima uwe imara, usiyeyumba na mwenye uthubutu, ili
mradi tu, shughuli tarajiwa ziende kama inavyotakiwa.
Lakini, tujifunze
kuwa na kiasi. Siyo kila jambo linahitaji nguvu kulifanya liende, au dharau kwa
unaowaongoza, kejeli na majigambo. Maisha huwa ni magumu sana cheo hicho
kikiondoka.
Wapo baadhi yetu
wanatumia nafasi walizokabidhiwa kuwaumiza wenzao, kwa sababu tu ya ama tamaa,
wivu, ushamba au hata kujionesha kuwa wao ndiyo wao.
Ukiwa muungwana kwa
unaowaongoza, uongozi wako utapata baraka za Mungu, naye atakubariki udumu hapo
ulipo, lakini ukienda kinyume anguko lako litapikiwa pilau mlango wa pili.
Kama mtu ambaye
aliweza kuingia popote katika mikoa ya Arusha na Kilimanjaro na kufanya lolote
alilotaka hivi sasa ni mfungwa, wewe ni nani usiwaze kuwa kesho yaweza kuwa
zamu yako.
Kuna baadhi ya
watendaji katika nyadhifa zao serikalini, wanajiona miungu watu, kisa tu kule
juu kuna mtu wa kumlinda. Wapo wengine ni mabosi huku kwenye sekta binafsi,
wanawaumiza wenzao kwa sababu tu ni maswahiba wa wenye mali.
Cheo, hata kiwe
kikubwa vipi, kina mwisho na ukikitumia kwa ubaya, kitakulipa ubaya pia!

Post a Comment