DAKTARI MIREMBE ATAKA WAJAWAZITO KUACHA MITUNGI



 MKURUGENZI Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Magonjwa ya Akili Mirembe Dkt. Paul Lawale amewaasa akina Mama kuacha matumizi ya vilevi wanapokuwa wajawazito ili kuwanusuru watoto walio tumboni kuzaliwa wakiwa na matatizo ya afya ya akili.


Dkt. Lawale amesema hayo Jijini Dodoma wakati akisoma tamko la siku ya maadhimisho ya afya ya akili duniani yanayoadhimishwa Oktoba 10 kila mwaka kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima.

Amesema mama mjamzito anapokunywa pombe anamuweka hatarini mtoto atakayezaliwa kwani inaweza kumsababishia athari katika ukuaji wa ubongo kwa mtoto aliye tumboni na hivyo kumsababishia tatizo la afya ya akili pindi atakapozaliwa.

“Tunapoangalia ongezeko la watu wenye matatizo ya afya ya akili, lazima tuangalie tangu mtoto anapokuwa tumboni, wapo akina mama wengi wanatumia vilevi wanapokuwa wajawazito hii ina athari kwa mtoto aliye tumboni, " alisema Dkt. Lawale.

Ameongeza kuwa Mama mjamzito anapotumia vilevi inasababisha ukuaji wa ubongo wa Mtoto kuathirika na kusababisha Mtoto kuzaliwa na matatizo ya afya ya akili na kuendelea kuongeza idadi ya wagonjwa wenye matatizo ya afya ya akili nchini. 

 

 

No comments