KUNA MENGI YA KUJIFUNZA KWA MO

 

NIMEKUWAkaribu na soka letu kwa muda mrefu sasa, nikiwa naucheza katika ngazi za shule za msingi na sekondari na hatua kubwa kabisa kuifikia ni ile ya Ligi Daraja la Tatu, ngazi ya Mkoa enzi zile.

Bingwa wa Mkoa miaka ile halikuwa jambo dogo, kwani baada ya ubingwa huo, ilifuata ngazi ya Kanda, ambako mabingwa wa mikoa na washindi wao wa pili walicheza na washindi wa hapo, walipanda daraja la Pili Taifa, hatua moja kabla ya kufika Ligi Daraja la Kwanza, ambalo ndilo lilikuwa hatua ya juu kabisa.

Lakini hata baada ya kuachana na soka la uwan jani, nimehudumu kwa miaka mingi pia nikiwa kama mwandishi wa habari za michezo na burudani, kitu kilichonipa fursa ya kufahamu mambo mengi yanayohusu soka, hasa viongozi na vyama vyake, kuanzia mikoani hadi Karume pale.

Kwa klabu zetu kubwa za Simba na Yanga, ambazo ndiyo mfano wa mpira wetu, zingeweza kuwa na maendeleo makubwa sana kama tungepata aina ya viongozi wenye ndoto za mbali, kwa sababu tayari zina mtaji mkubwa wa mashabiki, lakini hali imekuwa tofauti kwa vile siku zote zimekutana na viongozi wanaopenda kukamua maziwa pasipo kuhakiki malisho bora.

Kama klabu hizi mbili ziliweza kujenga majengo yao katika miaka ya sabini na baadaye Yanga kuwa na Uwanja wao, vipi leo hii, mashabiki wao wakiwa wameongezeka pengine mara tatu ya hapo awali, wanashindwa kuwa na viwanja vyao vyenye hadhi?

Tatizo kubwa lililo nyuma ya pazia kwa aina ya viongozi wanaopatikana katika miaka ya hivi karibuni ni kutokuwa na jicho la kutazama maendeleo, badala yake wanaangalia katika kujinufaisha wao binafsi. Ukitaka kuamini haya, tazama jinsi vita kubwa inayopiganwa wakati wa uchaguzi.

Watu wanatumbukiza fedha kuhonga wanachama, wanatumia hila, kampeni chafu na hata kuibuliana kashfa, ili mradi tu waweze kupata nafasi za uongozi. Unatoa hadi mamilioni ya shilingi ili ushinde uongozi, utarudishaje pesa zako? Ni kama wale wanasiasa wanaolia machozi ya Mamba kwenye kampeni, wakionyesha hisia za kuguswa na matatizo ya wananchi, kumbe ni wanafiki wanaowaza posho, mishahara mikubwa na hadhi ya kibunge mjengoni.

Klabu hizi ndizo timu pekee zinazoweza kushawishi wanachama kuzichangia pasipo hata kutumia nguvu. Leo hii, klabu hizi zinaweza kusafiri kwa msaada kwenda katika kituo chochote cha mechi zake za Ligi Kuu na huko zikapata hoteli yenye hadhi kwa mkopo, wachezaji wakala watakacho na bado wakasafiri kurejea Dar es Salaam kwa wakati.

Na wanaweza kufanya hivyo msimu mzima. Wanachojali sana mashabiki ni matokeo mazuri uwanjani. Kama timu zina mitaji hii, ni vipi viongozi wanashindwa kutengeneza mfumo wa klabu kuweza kujiendesha kwa faida?

Lakini hata hivyo, kushindwa kubuni njia mbadala za kuiendesha klabu yenye mtaji mkubwa wa mashabiki kwa maendeleo linaweza kuwa tatizo moja, lakini weledi wa uongozi, ndilo tatizo kubwa zaidi linalozikumba klabu hizi mbili pendwa hapa nchini.

Mtu akishakuwa kiongozi, Mwenyekiti kwa mfano, anataka yeye ndiye awe kocha wa timu, mtunza hazina wa klabu, yaani kifupi ni kuwa viongozi wengi wa klabu hizi, hawajui utendaji kazi wa kitaaluma.

Wakati fulani nikiwa mwandishi wa michezo, nilisafiri kuelekea Morogoro kwenye moja kati ya mechi za klabu hizi. Nikiwa njiani, majira ya saa nne asubuhi, simu yangu ilipokea ujumbe kutoka kwa mmoja wa viongozi wa timu hiyo kunitaarifu juu ya mapendekezo yake ya kikosi kwa kocha wa timu.

"Tumemwambia kocha atupangie wachezaji hawa na hawa ndiyo wakae benchi," ilisema sehemu ya ujumbe huo na kuorodhesha wachezaji hao.

Ni jambo la ajabu sana, vipi kiongozi atoe mapendekezo ya wachezaji wa kucheza mechi badala ya kazi hiyo kufanywa na mwalimu? Na hata kocha, hawezi kupanga wachezaji wa kucheza mechi pasipo kupata ripoti ya daktari wa timu juu ya fitness ya wachezaji!

Tatizo hili ndilo hasa linalofanya klabu hizi zinashindwa kusogea. Lakini ujio wa Mo kwa namna ya Uwekezaji, ni funzo kubwa ambalo linaweza kuwa ni mwarobaini wa kuusaidia mpira wetu, achana na klabu hizo mbili pekee.

Mo ameibadilisha Simba ndani na nje ya Uwanja na kuifanya kuwa timu ya kisasa kwa kila namna. Katika benchi la ufundi, licha ya kocha na msaidizi wake, lakini yupo mwalimu wa viungo, daktari wa timu, mchambuzi wa mechi ambao kila mmoja anafanya kazi kwa mujibu wa alichokisomea kwenye eneo husika.

Ni ngumu kufikiria, kama leo hii Mangungu ana ujasiri wa kupenyeza kikaratasi kwa kocha Didier Gomes akitaka 'mchezaji' wake apangwe.

Mo amefanya hivyo pia hadi kwenye bodi. Anajua yeye si fundi sana wa kujua vipaji na biashara ya wachezaji. Amewaweka watu wa namna hiyo ili wamsaidie. Hao ni kama akina Magori, Hans Poppe, Kassim Dewji, Mulamu na wenzao, ambao ili kubalance mambo, wamewekwa chini ya mwanamama Barbara Gonzalez.

Viongozi wanafanya majukumu yao ili benchi la ufundi na lenyewe lifanye majukumu yake. Matokeo yake ni kama unavyoona, wachezaji wanajituma, makocha wanajituma na kikosi chote kina furaha.

Lakini angalia upande wa pili, kwa Wananchi. Kuna mtu anaitwa Injinia. Yeye ndiye anasajili wachezaji, yeye ndiye anajadiliana na kocha. Mbaya zaidi, yeye ndiye mwakilishi wa mdhamini ndani ya klabu.

Ingawa kimuundo unaona kama Yanga nayo ina benchi la ufundi linalohitajika kwa timu ya kisasa, lakini siyo vibaya kuhisi, kwa namna  timu inavyoendeshwa, kwamba huenda Injinia huwa anapenyeza 'mawazo' yake juu ya nani aanze kucheza na nani asicheze kwenye mechi husika.

Kama matajiri wa nchi yetu wataamua kuwekeza kwenye mpira wa miguu, kisha wakaajiri watu wenye taaluma kwenye maeneo husika, ni wazi kuwa tunaweza kuwa na timu zinazotisha kama Simba hata zaidi ya nne au tano kwa wakati mmoja.

Fikiria kama Azam itakuwa namna hiyo, Yanga, uwekezaji wa maana pia ukafanywa Kagera na Mtibwa, vipi tukose timu zinazoweza kupambana kwenye anga la kimataifa kama ilivyo sasa kwa Afrika Kusini ambayo inaingiza timu mbili hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika?

Watu wenye hela wapo, pengine TFF iunde timu ya wataalamu wa kwenda kutoa ushawishi kwa matajiri ili waone namna gani wanaweza kupata faida kwa kuwekeza kwenye soka.

Hawa wataalamu wawatembelee na kuzungumza na watu kama akina Rostam Aziz ili airejeshe timu ya nyumbani kwao kule Mirambo, Bin Slum wa Coastal Union, Asas afanye hivyo kwa Lipuli na wengine na wengineo.

No comments