WAKALA UNUNUZI WA MAHINDI RUVUMA WADAIWA KUWATENGA WAKULIMA, WANUNUA MAZAO YA WAKUBWA
NA STEPHANO MANGO, SONGEA
WAKULIMA wa zao la mahindi Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma
wameilalamikia Serikali kupitia wakala wa hifadhi ya Taifa (NFRA) Kanda ya
Songea kwa kushindwa kununua mahindi yao badala yake wananunua mahindi ya
wafanyabiashara wakubwa na viongozi wa kada mbalimbali nyakati za usiku.
Wakizungumza mbele ya waandishi wa habari jana nje ya eneo la
NFRA Kanda ya Songea kwa nyakati tofauti mjini hapa, wakulima hao ambao
wameomba majina yao yahifadhiwe walisema kuwa mahindi yao hayanunuliwi kwa
kigezo kuwa ni machafu na hayana ubora wakati jambo hilo sio la ukweli.
Walisema kuwa nyakati za usiku kumekuwa na magari ambayo
yanaingia moja kwa moja ndani na kwenda kupimwa kwa lengo la kuuzwa
mahindi bila kuzingatia utaratibu wa kufuata foleni kama
ulivyopangwa hali ambayo imekuwa ikiwashangaza na kuhoji kuwa mahindi
hayo ni ya watu gani na yanatoka wapi.
Walisema kuwa awali waliambiwa kuwa watanunua mahindi
toka kwa wakulima gunia 80, baadae wakasema watanunua gunia 50 kwa kila mkulima
lakini leo wanasema kuwa watanunua mahindi gunia 10 kwa kila mkulima, kitu
kinachowashangaza kwani wako kwenye foleni kwa muda wa wiki mbili na kila mmoja
akiwa na magunia zaidi ya mia moja.
“Tunashindwa kuelewa hatima yenu ni ipi katika ununuzi wa
mahindi yetu, kila kukicha tunaandikisha majina ya wakulima 20 lakini katika
kwenda kupima wakulima 7 tu kati ya 20 ndio wanafanikiwa kupimiwa mahindi yao
na 13 waliobaki mahindi yao yanatolewa nje kwa madai kuwa ni machafu, huku
tukiwa tunadaiwa fedha za usafiri wa mahindi kutoka vijijini kuyaleta hapa,"
alisema mmoja wa wakulima hao.
Walimeiomba Serikali kuona umuhimu wa kuangalia kwa upana wake
suala la ununuzi wa zao hilo kutoka kwa wakulima kwa sababu ndio zao pekee kwao
na wakati wa msimu ujao wa kilimo unakaribia.
Kwa upande wake Meneja wa NFRA Kanda ya Kusini Mohamed Nondo
alisema kuwa fedha wanazopokea toka Serikalini ni ndogo, hivyo kadri
wanavyopokea ndivyo wanavyonunua, na kwamba kwa sasa wanatarajia kununua tani
4000.
Nondo alisema kuwa madai mengine yanayotolewa na wakulima hao
hayana ukweli wowote na kama kuna mkulima ana ushahidi wa jambo hilo basi
aupeleke kwenye vyombo vinavohusika ili hatua ziweze kuchukuliwa.

Post a Comment