SERIKALI KUPUNGUZA TOZO ZA LESENI MITANDAONI

 Tehama Shipping - Home | Facebook

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa, amesema Serikali inakwenda kuondoa asilimia hamsini ya ada za tozo mbalimbali za leseni kwenye marekebisho ya Kanuni za maudhui ya mtandaoni na maudhui ya utangazaji katika redio na televisheni yaliyofanywa hivi karibuni ili kuzalisha ajira na vipato.

Bashungwa alisema hayo jana Septemba 1, 2021 Dodoma katika kikao cha kupokea taarifa ya maboresho ya Rasimu ya Marekebisho ya Kanuni za Maudhui Mtandaoni za mwaka 2020 na Kanuni za Maudhui ya Utangazaji katika Redio na Televisheni za mwaka 2018 yaliyotolewa na wadau mbalimbali hivi karibuni.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Pauline Gekul na Mkurugenzi wa Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa.

“Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imeamua kwa dhati kufanya marekebisho ya kanuni hizi kwa kuwashirikisha wadau wake ambapo sasa katika kipindi kifupi kijacho tutashuhudia maboresho yanaleta matumaini na mapinduzi makubwa kwenye sekta na wadau wategemee ongezeko la ajira na kuboreka kwa vipato vyao kwa kiwango kikubwa,” alisema Bashungwa.

Bashungwa alisema ada kwa Leseni za ‘simulcasting’ imeondolewa kabisa ambapo ameeleza kwamba hatua hiyo imefikiwa baada ya kuzingatia maoni ya wadau ya kuiomba Serikali tahfifu ya ada husika ili waweze kumudu kulipa bila faini au kulimbikiza madeni ambapo amesema watoa huduma wanatazamiwa kuongezeka kutokana na viwango vya ada kuwa rafiki.

No comments