CHAMURIHO AWATAKA WAHANDISI VIJANA KUJENGEWA UWEZO
WAZIRI wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi, Dkt.
Leonard Chamuriho, amezitaka Taasisi zote zinazohusika na kazi za kihandisi nchini
kuweka kipengele cha kuwajengea uwezo wahandisi vijana katika mikataba yote ya ujenzi
itakayoingiwa na Serikali kuanzia sasa.
Akifungua mkutano wa 18 wa Bodi ya Usajili wa Wahandisi
(ERB), jijini Dodoma, Waziri Chamuriho amesema sera na muelekeo wa Serikali kwa
sasa ni kuhakikisha wahandisi hususani vijana kuwa na uwezo wa kutosha kusimamia miradi ya ujenzi
inayoendelea nchini na inayotarajiwa kuanza hivi karibuni.
“Hakikisheni miradi mikubwa kama ya SGR, Bwawa la
Umeme la Julius Nyerere, miradi ya maji, bomba la mafuta, madaraja makubwa,
ujenzi wa meli na barabara unahusisha moja kwa moja wahandisi vijana”, amesema
Waziri Chamuriho.
Amebainisha kuwa Serikali imejipanga kuongeza ushiriki
wa sekta binafsi katika miradi yake ya maendeleo hivyo ni wajibu wa sekta binafsi
na serikali kushirikiana kuwawezesha wahandisi kupata uzoefu utakaowasaidia kufanyakazi
ndani na nje ya nchi.
Aidha, Waziri Chamuriho, amewashukuru Benki ya Dunia
na Serikali ya Norway kwa kufadhili programu mbalimbali za kuwajengea uwezo wahandisi
hususani wanawake na kutoa wito kwa taasisi nyingine kuiga mfano huo.
Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
(Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Malongo, ameitaka ERB kufanya tathimini ya maazimio
yaliyofikiwa mwaka jana kuona kama yametekelezwa na hivyo kujipima katika yale matarajio
yaliyofikiwa.
Amezungumzia umuhimu wa kufuatilia wahandisi wahitimu wanaofanya vizuri katika masomo yao ili kuona kama wanafanya vizuri katika utendaji wa kazi zao kama ambavyo maadili ya taaluma yao yanavyowataka.
Wahandisi 632 wakila kiapo cha utii katika maadhimisho
ya 18 ya Siku ya Wahandisi, jijini Dodoma.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya ERB, Prof.
Ninatubu Lema, zaidi ya wahandisi 32,145 wamesajiliwa na bodi hiyo tangu kuanzishwa
kwake.
Akiwakaribisha wahandisi, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,
Anthony Mtaka, amewataka wahandisi kuwekeza katika mkoa huo ili kuufanya mji mkuu
wa nchi kuwa katika viwango bora vya miundombinu.
Zaidi ya wahandisi 600 wamekula kiapo cha utii leo katika
kikao hicho na kukabidhiwa leseni tayari kwa kuanza kazi za kihandisi.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Post a Comment