ASILIMIA 45 YA WATANZANIA WANATIBIWA KWA MITI SHAMBA

 Department of Development Studies - Prof. Kabote

 

KAIMU Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), upande wa Taaluma, Profesa Samwel Kabote amesema asilimia 45 ya watanzania wanatibiwa kwa tiba asili na tiba mbadala.


Alitoa kauli hiyo wakati akifunga maadhimisho na maonesho ya wiki ya tiba asili ya Mwafrika Kanda ya Mashariki yaliyofanyika kwenye viwanja vya Soko Kuu la Chifu Kingalu Manispaa ya Morogoro yaliyowakutanisha wadau wote kwenye mnyororo wa thamani ya mimea dawa kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania.

"Takwimu zinaonyesha kuwa tiba asili inachangia kwa kiasi cha asilimia 45 katika kutoa huduma za afya kwa Watanzania na asilimia 55 ndiyo madawa mengine ya madukani, kwa hiyo asilimia hizo sio ndogo kama ambavyo watu wengi wanadhani maana naamini wengi zaidi wanaikimbilia tiba asili katika kutatua changamoto zao mbalimbali za kiafya na hivyo kupata afya ya kuwawezesha kufanya kazi za kiuchumi," alisistiza Profesa Kabote.

Aidha amewataka waganga wa tiba asili na mbadala kuendelea na juhudi za kuboresha dawa hizo kwa kushirikiana na watafiti wa SUA na Chuo cha Afya Muhimbili na taasisi zingine za kupima ubora na usajili ili zizidi kuaminika na jamii nzima bila kujali elimu ya mtu, kipato wala rangi yake na hivyo kuongeza soko na huduma zaidi kwa jamii na kujiongezea kipato.

Profesa Kabote ametoa wito kwa waganga wa tiba asili kushirikiana na watafiti kote nchini katika kubaini miti dawa ambayo wanaona ina faida kubwa katika tiba ili ifanyiwe utafiti zaidi na kuongeza thamani ya mimea hiyo ili kupta dawa za kitanzania nzuri na zenye ubora wa hali ya juu kwa matumizi ya hapa nchini na nje ya nchi.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufunga maadhimisho hayo Mkurugenzi wa Shahada za Juu Utafiti, Ushauri na Uhawilishaji wa Teknolojia Profesa Hesron Karimuribo alisema Wizara ya Afya inatambua mchango mkubwa wa SUA katika jitihada za kusaidia tiba asili nchini na ndio maana wakapewa nafasi ya kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo kwa kanda ya mashariki.

"Kama mkurugenzi mwenye dhamana ya utafiti SUA tumekuwa tukihakikisha tunafanya tafiti mbalimbali kupitia wataalamu na watafiti wa chuo chetu katika sekta ya tiba asili kwa kushirikiana na wadau hawa ili kuboresha na kuongeza thamani dawa zao na namna wanavyotoa huduma lakini pia kuhamasisha upandaji wa mimea dawa ili isiweze kutoweka kwa kuwa inatumiwa sana na kuvunwa kwa wingi," alisema.

Ameongeza kuwa SUA imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kufanya tafiti za kupata dawa za kukabiliana na ugonjwa wa UVIKO -19 ambapo umepata dawa mbalimbali ikiwemo dawa maarufu ya SYNADOL ambayo inatumiwa na watanzania wengi kwa sasa ndani nan je ya Mkoa wa Morogoro kutokana na ufanisi wake katika kusaidia wagonjwa hao.

Akieleza ushirikiano wa SUA na wadau wa tiba asili Mtafiti Mkuu wa Mradi wa GRILL Dkt. Faith Mabiki alisema kuwa uanzishwaji wa jukwaa la ubunifu la wadau wa bidhaa za tiba asili nchini GRILL ni moja kati ya mikakati mikubwa iliyozaa mafanikio makubwa katika kuwakutanisha wadau wote kwenye mnyororo wa thamani lakini pia kuwapa sauti ya pamoja na kubadilishana mawazo na uzoefu nchini.

"Sisi kama watafiti wa SUA ambao tumekuwa tukifanya kazi karibu sana na wadau hawa wa tiba asili, tunajivunia mabadiliko makubwa tunayoyaona sasa tunapofika kwa kila mganga wa tiba asili kwa kuona namna wanavyofungasha bidhaa zao na kutengenza dawa katika ubora wa hali ya juu tofauti na zamani ambapo walikuwa wakiwapatia wateja au wagonjwa wao magome ya miti, majani na kuweka kwenye mifuko isiyofaa kuweka dawa," alisema Dkt. Mabiki.

Kwa upande wake Mratibu wa tiba asili na tiba mbadala mkoa wa Morogoro Dkt. Wille –Anne Ngalula alisema kuwa jukwaa la ubunifu la tiba asili Tanzania lililoanzishwa na SUA linaendeleza malengo na jitihada za Serikali katika suala zima la utoaji wa dawa na kuboresha afya nchini kupitia tiba asili.

’’Kwa sasa Mkoa wa Morogoro una waganga wa tiba asili waliosajiliwa na Baraza la Tiba Asili Tanzania wamefikia 1872 na tayari maduka 71 ya tiba asili yamesajili katika mkoa wa Morogoro, hii inaonyesha mwamko mkubwa uliopo kwa wganga hawa katika kufuata sheria na kanuni za serikali katika utoaji wao wa huduma lakini pia muitikio wa wananchi katika kutafuta huduma zao ndio maana wanaongezeka siku hadi siku na hii inatokana na kazi kubwa iliyofanywa na SUA pamoja na timu yetu ya mkoa," alieleza Dkt. Ngalula.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyamna vya Waganga wa Tiba Asili Tanzania Mkoa wa Morogoro (SHIVYATIATA) Ramadhani Sanze ameishukuru SUA kwa kuendelea kuwa mlezi wa waganga wa tiba asili nchini na kwa jitihada wanazozifanya katika kuboresha utoaji wao wa huduma kwa wagonjwa kwani imeongeza thamani ya dawa zao lakini pia kuwajengea kuaminika na kujiamini katika utoaji wa huduma na hivyo kuwaongezea elimu na kipato.

Maadhimisho ya tiba ya wiki ya tiba asili ya Mwafrika Kanda ya Mashariki yamefanyika kwa kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo kutoa huduma za ugani kwa waganga wa tiba asili kwenye maeneo yao ya kutolea huduma, kongamano la kisayansi la tiba asili kwa njia ya mtandao pamoja na maonesho makubwa ya kanda ya mashariki yaliyokutanisha waganga wa tiba asili na wadau wengine kwenye mnyororo wa thamani wa tiba asili kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania.


No comments