ASKARI MAGEREZA AWASIMAMIA MFUNGWA, MSHTAKIWA WAKITETA CHOONI MAHAKAMANI

KATIKA hali isiyo ya kawaida, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi
Wilaya ya Bababati Mkoani Manyara, mfungwa anayetumikia kifungo cha miaka 30 alionekana
akifanya kikao cha siri pembeni ya choo cha mahakama hiyo na mfanyabiashara Salehe
Alamri ambaye ni mshtakiwa wa kesi ya kumiliki silaha kinyume cha sheria huku
wakilindwa na askari Magereza ambaye hakufahamika jina lake.
Katika tukio hilo watu hao walionekana wakiteta kwa takribani
dakika 20 huku askari magereza akiwasimamia jambo ambalo liliubua maswali mengi
mahakamani hapo na kisha baadae mfungwa huyo alipelekwa katika mahabusu iliyopo
mahakamani hapo kabla ya kurejeshwa magereza.
Kesi ya kumiliki silaha kinyume na
sheria inayomkabili mfanyabiashara, Salehe Salim Alamri na wenzake imeahirishwa
jana katika mahakama ya hakimu mkazi wilayani Babati mkoani Manyara .
Kesi hiyo nambari 11 ya mwaka 2020 imeahirishwa jana na Hakimu
wa mahakama hiyo, Kimario hadi September 28 mwaka huu baada ya upande wa
jamhuri kueleza kwamba upelelezi bado haujakamilika.
Katika kesi hiyo Mfanyabiashara huyo anadaiwa mnamo Julai 26
mwaka 2019 akiwa katika eneo la Makame Kijenge jijini Arusha alikutwa akimiliki
silaha aina ya Riffle CAR 22 No. 00104516 kinyume na sheria.
Pia mfanyabiashara huyo siku hiyo hiyo alikutwa na silaha
nyingine aina ya Shotgun yenye nambari 00104513 mali ya HSK Safaris Ltd
aliyokuwa akiimiliki bila leseni wala kibali cha umiliki kutoka mamlaka husika.
Mbali na mfanyabiashara huyo mtuhumiwa mwingine, Gerald Joseh
Ole Kashiro anashtakiwa kwa kosa la kushindwa kutunza silaha sehemu salama
kinyume na sheria nambari 59(1)(a) na sheria nambari 61 ya sera ya udhibiti wa
silaha nambari 2 ya mwaka 2015.
Katika shitaka hilo Ole Kashiro anadaiwa mnamo Febuari 20
mwaka 2020 akiwa katika pori ya hifadhi ya akiba ya Simanjiro ndani ya wilaya
ya Simanjiro mkoani Manyara alishindwa kuhifadhi sehemu salama silaha aina ya
Rifle 300mm No.A757677 na nyingine aina ya Shotogun 12bore No.T.0611018 na
kishindwa kuzihifadhi sehemu salama hali iliyopelekea kuangukia mikononi mwa
mtu asiyekuwa na uhalali kisheria.
Itakumbukwa ya kwamba mbali na mashtaka anayokabiliwa Ole
Kashiro lakini pia anatumikia kifungo cha miaka 30 katika gereza la mkoa
Manyara kwa kosa la kukutwa na nyara za serikali katika kesi ya uhujumu uchumi
nambari 21 ya mwaka 2019 hukumu iliyosomwa na hakimu Jumaa Mwambago.

Post a Comment