DKT. SENGATI AAHIDI KUPAMBANA NA CHANGAMOTO YA UMASIKINI SHINYANGA


DC SENGATI KUTUMIA MIFEREJI MINGINE KUTATUA KERO, WAPINGA MAENDELEO  KUSHUGHULIKIWA - YouTube

Na Anthony Ishengoma- Shinyanga.

MKUU wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati amesema mkoa huo una utajiri wa rasilimali lakini hali ya maisha ya wananchi wake haiendani na hali halisi, akiitaja kuwa ndiyo changamoto kubwa.

Dkt. Sengati amesema hayo leo wakati wa kumkaribisha Katibu Tawala Mpya wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Batlida Buriani ambaye kwa mara ya kwanza amefika katika ofisi yake mpya tayari kwa makabidhiano na kuendelea majukumu yake mapya.

Dkt. Sengati aliongeza kuwa Shinyanga kuna umasikini ambao umejificha katika utajiri mkubwa lakini hususani kwa wakazi wa pembezoni akiahidi kuifanyia kazi changamoto hiyo ili wakazi wake waweze kuinua hali yao itakayoendana na rasirimali zilizopo.

‘’Unakuta mtu ana ng'ombe zaidi ya elfu moja lakini mtu huyo anaishi katika mazingira yaliyo duni sana au haoni faida ya kupeleka mtoto katika elimu ya juu hii changamoto ambayo lazima tuifanyie kazi,” alisisitiza bosi huyo wa mkoa.

Naye Katibu Tawala Dkt. Batlida Buriani amesema kuwa lazima kuwe na ubunifu katika kutafuta vyanzo vipya vya mapato na kuzitaka Halmashauri za Mkoa wa Shinyanga kukusanya mapato bila ya kuleta kero kwa wananchi.

Aidha Dkt. Buriani amesema pia ipo haja ya kuingalia upya mianya yote ambayo imekuwa ikichangia upoteaji wa mapato kwa lengo la kuinua na kukuza uchumi wa mkoa wa Shinyanga.

Pamoja na mambo mengine Dkt. Buriani amesema ataliangazia pia suala la maendeleo na ustawi wa jamii kwa kuhakikisha ipo miradi ambayo inaweze kuingiza kipato kwa wazee na wanawake ili nao waweze kuchangia katika kujiletea maendeleo lakini pia kuchangia katika maendeleo ya Taifa.

‘’Najua Shinyanga kuna wazee wengi sana na hali zao sio nzuri na katika jambo ambalo ninataka tufanikiwe ni kuhakikisha wanashiriki katika miradi ambayo itawanufaisha najua kuwa Shinyanga kuna mifugo mingi hivyo tunaweza tukatumia fursa ya mifugo iliyopo kuzalisha siagi kwa wingi sana," alisema.

Naye aliyekuwa Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Bw. Albert Msovera alisema bado kuna changamoto ya watumishi lakini zipo juhudi ambazo zimekuwa zikiendelea kuhakikisha changamoto hiyo inatatuliwa na hivyo kumtaka mrithi wake kuangalia namna bora ya kuendelea kulifanyia kazi jambo hilo ili kukabiliana na upungufu wa rasilimali watu.

 

No comments