ZIARA YA SASHA KENYA YAIBUA MJADALA



RAIS SAMIA SULUHU HASSAN APANGUA BARAZA LA MAWAZIRI - MICHUZI BLOG



 ZIARA ya siku mbili ya Rais Samia Suluhu Hassan 'SASHA' nchini Kenya, imeibua mjadala mkubwa nchini, kufuatia makubaliano yaliyofikiwa kati yake na mwenyeji wake, Uhuru Kenyatta wa kuondoa vikwazo vya kibiashara baina ya nchi hizi jirani.

Katika ziara hiyo, wawili hao walitia saini makubaliano ya ujenzi wa bomba la gesi kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa, mradi ambao endapo utafanikiwa, utaisaidia zaidi Kenya inayohitaji nishati kwa ajili ya matumizi ya viwanda vyake.

Pia, viongozi hao walikubaliana kuondoa vikwazo kwa wafanyabiashara wa nchi hizo mbili, ambapo kwa kuanzia, Rais Uhuru alitaka wafanyabiashara wa Tanzania kuwekeza bila kuhitaji kwanza vibali vya kufanya kazi (working permit).

Pia, mgogoro kuhusiana na mahindi ya Tanzania ambayo yalikuwa yamezuiwa mpakani, yametakiwa yawe yameruhusiwa kuingia Kenya ndani ya wiki mbili kuanzia juzi.

Kwa nyakati tofauti, watanzania wamekuwa na mjadala mkubwa katika mitandao ya kijamii juu ya makubaliano hayo, wengi wakionekana kuridhishwa nayo, huku wachache wakijiuliza kama itimisho la ziara hiyo lina tija kwa taifa.

Wanaounga mkono makubaliano hayo, walisema Tanzania itafaidika kwa kupata uwekezaji zaidi kutoka Kenya, hivyo kusaidia katika kukabiliana na tatizo la ajira, aidha pia kupata fursa ya kujifunza na kunufaika na uzoefu wa Kenya katika biashara ya bidhaa za viwandani.

Eneo jingine ambalo Tanzania itanufaika nalo ni soko la uhakika kwa bidhaa za kilimo, kama vile nafaka, matunda na maua.

Wale wanaotilia shaka ushirikiano huo mpya, wanadai kwa kuipelekea Kenya gesi, itamaanisha kuua viwanda vyetu, kwani majirani hao wenye uzoefu katika viwanda, watatengeneza bidhaa zao kwa gharama ndogo na hivyo kuvishusha bei hapa nchini, kitu ambacho kitapelekea kukosa soko kwa bidhaa zetu.

No comments