WASANII WAIJIA JUU BASATA

 MwanaFA - YouTube

SIKU chache baada ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), kutoa mwongozo kwa wasanii wa muziki wa kizazi kipya kupeleka kazi zao ili kuhakikiwa kabla ya kuziruhusu kupigwa redioni na katika televisheni, wasanii wameibuka na kuipinga kila kona.

Lengo la Basata katika mwongozo huo, ni kile ilichosema kulinda maadili ya maudhui na hata uonekanaji kwenye video.

Wasanii hao wamesema jambo hilo ni la kizamani na linalolenga kurudisha nyuma sanaa hiyo ambayo sasa imekua kubwa na yenye kutoa ajira za kutosha kwa maelfu ya vijana nchini.

Waliopinga waziwazi ni pamoja na mkongwe wa Bongo Fleva, Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA ambaye pia ni Mbunge wa Muheza kupitia CCM.

Mwana FA ameitaka Basata kufikiria upya kuhusu jambo hilo, kwani linaenda kuiumiza sanaa. Nyota mwingine wa muziki huo wa kizazi kipya, Ney wa Mitego, ambaye amekwenda mbali zaidi na kudai anafanya mchakato wa kujitoa katika Baraza hilo ili awe huru wa kuweza kufanya muziki na kusambaza mwenyewe mitaani.

Z Anto pia ni miongoni mwa wasanii wanaolalamikia hatua hiyo ya Basata, akidai kitendo hicho kinakwenda kuua mitaji ya wasanii, kwani kazi hizo zinakwenda kuhakikiwa ikiwa tayari wameshgrekodi au kutengeneza video.

 

No comments