VIONGOZI NAMTUMBO WANASUBIRI MABANGO YA RAIS SAMIA SULUHU HASSAN?


President Samia disappointed with kind of debate in Parliament - The Citizen

NA STEPHANO MANGO, SONGEA

WANANCHI kote nchini bado wana kumbukumbu na hotuba za Rais Samia Suluu Hassan, alizotoa katika matukio mbalimbali ambapo ameonyesha mwelekeo wa serikali yake kwa kutoa maelekezo yenye nia ya kutibu majeraha na kugusa maeneo yaliyo kuwa yakilalamikiwa na kukwamisha kasi ya maendeleo.

Akihutubia baada ya kuwaapisha Mawaziri, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu, alisisitiza ufanyaji  kazi wenye kuondoa kero kwa wananchi na uletaji tija kwa taifa na kuepusha mabango kutoka kwa wananchi.

Rais aliwaonya watendaji wa chini akisema kuwa viongozi  wakikutana na mabango ya malalamiko katika ziara zao basi atawaondoa  Mkurungenzi wa Halmashairi husika pamoja na Mkuu wa wilaya hiyo.

Alisema imekuwa ni kawaida viongozi wakifanya ziara mkoani na wilayani wanapokewa na mabango ya wananchi wakilalamikia kero mbalimbali na masuala yanayolalamikiwa sio ya kitaifa.

“Naomba tunapokuja huko, Mimi, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu, tukikuta bango basi ziwe ni issues (masuala) ya kitaifa lakini si mambo  ya kushughulikiwa kule chini.

"Nataka  niseme bango moja aidha Mkurugenzi au Mkuu wa wilaya amekwenda, na hii haina maana mkazuie watu kuandika kero zao, naomba kero za wananchi zikashughulikiwe. Tumekuja tumekuta bango moja, Mkuu wa wilaya na Mkurungenzi umekwenda.

"Ninaomba mkafanye kazi na kuwatumikia watanzania bila ubaguzi kama mlivyoapa hapa, mkawe msaada na si bugudha au adha kwa watanzania, mkawe neema na sio kero na nuksi kwa watanzania, mkasimamie haki na sio udhalimu na dhulima na unyanyasaji kwa watanzania," alisema Rais Samia.

Pamoja na onyo hilo, bado kuna viongozi, pengine kwa kufanya kazi kwa mazoea au makusudi,  wanapuuzia kutatua kero za wananchi jambo ambalo  linaweza kusababisha uwepo wa mabango wakati wa ziara ya viongozi wakuu wa nchi.

Hivi karibuni imeripotiwa habari za kuwepo kwa mgogoro wa ardhi kati ya mkuu wa wilaya mstaafu wa Namtumbo, Luckness Amlima na wananchi katika kitongoji cha Nyerere katika kijiji cha Mchomoro.

Wananchi kutoka koo 16 wa kijiji hicho kilichopo katika Kijiji cha Mchomoro kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo Mkoani Ruvuma, walimuomba aliyekuwa Mkuu wa Mkoa  wa Ruvuma, Christine Mdeme kuingilia kati utatuzi wa mgogoro wa ardhi yao zaidi ya heka 700 kati yao Luckness Amlima ili waweze kuendelea na shughuli zao za kimaendeleo.

Wananchi hao wanalalamika kuwa wakiwa na familia 68 wamekuwa hawasikilizwi na viongozi wao, wakihisi wanamlinda kiongozi mwenzao, kwani kwa zaidi ya miaka minne sasa wamekuwa wakipuuzia mgogoro huo kwa sababu zao binafsi hali ambayo inaashiria kuwa ni kumpendelea mkuu huyo wa wilaya mstaafu.

Rashid Malamaye anayesimama kwa niaba ya koo hizo, anasema mkuu huyo wa wilaya amevamia katika maeneo yao ya asili ambayo wao walikuwa wanayatumia kwa shughuli za kilimo na ufugaji kwa miaka mingi. 

Anasema katika mashamba hayo kulikuwa na nyumba za nyasi, mazao ya muda mrefu aina ya minazi, machungwa, migomba na mihogo yamechomwa moto na kufyekwa, huku pia walinzi wakiwa wamewekwa kulinda maeneo yao kuwazuia wasiingie.

Taarifa zinasema kiongozi huyo wa zamani aliomba na kupewa kiasi cha heka 40, lakini kwa mshangao wa wananchi, amedhulumu ekari 700, tena bila vikao vya vijiji kama sheria inavyosema.

Wananchi wanasikitishwa na jambo hili kwani viongozi wa kijiji badala ya kulinda raia na mali zao wao wamekuwa chanzo cha kutengeneza migogoro kinyume na kiapo chao cha uadilifu ambacho waliapa.

Alifafanua kuwa hali iliyopo kwa sasa sio nzuri kwani wenye mashamba wakienda kufanya shughuli zao wanakamatwa na kufunguliwa kesi mbalimbali katika kituo cha polisi Wilaya ya Namtumbo hali ambayo inazidisha uhasama kati ya wananchi na mkuu huyo.

Mwenyekiti wa kijiji hicho Said Mohamed Mkalela anakiri kuwepo kwa mgogoro huo na kusema kuwa hatua zinaendelea kuchukuliwa ingawa wananchi hao wamekuwa wakikosa imani nao kutokana na kuchelewa kumalizika kwa mgogoro huo.

Mkalela alisema kuwa wao waliingia madarakani mwaka 2019 lakini nyaraka zinaonyesha mwekezaji huyo alipata eneo la heka 40 kihalali toka mwaka 2016 katika maeneo ya Namambigi na sio Mihane, lakini hatua za kutatua mgogoro huo zinaendelea ingawa wananchi wanateseka.

Cha kushangaza, mtuhumiwa anakataa kuwepo kwa mgogoro huo, akidai waulizwa viongozi wa vijiji.

Katibu Tawala wa Wilaya, Aden Nchimbi anakiri kuusikia mgogoro huo na kuagiza wahusika kwa kushirikiana na afisa ardhi wa Halmashauri kukutana na kuumaliza ili kuwaondolea kero wananchi.

Jambo lililo wazi hapa ni kuwa viongozi wa vijiji hawawezi kuutatua mgogoro huo kwa vile wana masilahi kwenye suala hilo.

Taarifa zilipofika hapo zinaonyesha kuwa mkuu huyo aliomba mashamba  heka 50 na kupewa heka 40 kisheria kwenye mashamba ya Namambigi lakini katika mazingira ya kutatanisha hivi sasa ana miliki heka zaidi ya 600 na kusababisha uvamizi wa mashamba ya wananchi.

Uvamizi huo umepelekea kufika mpaka kwenye mashamba ya wanakijiji katika eneo la Mihane ambapo mazao yao aina ya michungwa, minazi, na migomba ilifyekwa huku wananchi wakikamatwa na kubambikwa kesi na mkuu huyo wa wilaya mstaafu.

Viongozi wa kijiji ambao wana jukumu la kulinda raia na mali zao hawajachukua hatua stahiki za kukomesha mgogoro huu kwani wanaonyesha kumbeba kiongozi huyo wa zamani.

Kwa namna mazingira ya suala hili yalivyo, wanakijiji wakiwa wametoa taarifa za mgogoro huo kwa viongozi wao wa CCM, Mkurugenzi wa Halmashauri, na Mkuu wa Wilaya, ni wazi kuwa hitimisho la suala hilo ni mabango kwenye ujio wa viongozi wa kitaifa kwani muunganiko wa viongozi wa ngazi zote wakikandamiza, ni vigumu haki kutendeka.

 

No comments