USIJIDANGANYE, HAKUNA ANAYEKUZUNGUMZIA VIZURI

 First Consider In-person Focus Group Discussions | Research Design Review

KUNA dhambi moja kubwa sana ya asili ambayo sisi ngozi nyeusi tunayo, ubinafsi. Hii ni dhambi kubwa ambayo imezalisha dhambi zingine nyingi ndogo ndogo, lakini ambazo zina madhara makubwa katika maisha yetu ya kila siku.

Ubinafsi ninaousema hapa hata wewe unayesoma makala haya unao. Ule wa kutamani vitu vyote vizuri vinakuwa upande wako, yaani uwe na nyumba nzuri, gari zuri, mume handsome, mke beautiful, mchumba mzuri, mshahara mnono, biashara kubwa, yaani kama hivyo!

Sina uhakika, na nasema tena sina uhakika, kama kuna mtu angependa kumuomba Mwenyezi Mungu mambo hayo mazuri yamkute jirani yake. Kama yupo, mtu huyo, hapa duniani, naamini njia ya peponi kwake ni nyeupe kabisa.

Siyo vibaya kuwa na mawazo ya kutaka kupata kila kitu kizuri, kinachotufanya sisi tuonekane wa ajabu ni kwamba wakati tunajiombea mazuri, tunawaombea wenzetu mabaya!

Yaani wakati wewe unajiombea gari kali la kisasa na la gharama la kutembelea, mimi huniombei nipate japo baiskeli. Ungependa nitembee kwa miguu ili siku moja unipe lifti nione jinsi gari lako lilivyo bomba.

Ndiyo maana katika hali halisi, huwa tunazungumza maneno mengi sana juu ya watu waliofanikiwa. Mwizi yule, mchawi yule, jambazi, anajiuza huyo, anauza unga na vitu vingine vya namna hiyo.

Yaani huwa tupo tu na negativity kwa wenzetu. Siyo kwamba hatuamini katika watu kufanikiwa, la hasha. Watu tunawaona wanavyopambana na baadhi yao kushinda vita. Sisi tu tunaongozwa na ile dhambi, yaani mafanikio ya mtu tunapenda kuyatia doa, ili mradi tu isiwe kirahisi namna hiyo.

Ubinafsi huu tulio nao, umetufanya hata tusiwape thamani watu wema ambao Mwenyezi Mungu amewajaalia uwezo wa kutoa. Mtu akiwa na tabia ya kuwapa watu wanaohitaji kwa urahisi, tunakimbilia kumpaka matope "   Masharti ya mganga hayo"

Maana ni lazima pia tukubali kuwa pamoja na dhambi hii ya ubinafsi, kuna baadhi yetu wamejaaliwa karama ya kupata na kutoa. Yaani mtu anafanya vizuri kwenye kazi zake na wakati huo huo, ni mwepesi kuguswa na shida za wengine. Anapojitokeza mtu wa namna hii, na hasa akiwa ni mfanyabiashara, tutasema anafanya hivyo kwa sababu mganga wake kampa hayo masharti!

Dhambi hii ya ubinafsi imetufanya tuwe watu wa kusengenyana, wanafiki na tuliojaa hadaa nyingi. Unaweza kuwa na majadiliano na wenzako, tuseme muwe zaidi ya watatu. My friend, yaani ukitoka tu, huku nyuma badala wajadili yale uliyoyatoa, wanakujadili wewe!

Wakati pekee ambao angalau unajifariji kuwa watu hawakusemi vibaya, ni pale tu unapokuwa nao, yaani ukiachana nao wewe unageuka kuwa ajenda.

Ndiyo maana nikasema, usije ukajidanganya mwenyewe kwa kudhani kuwa kwa sababu una mashoga zako, rafiki zako, au ndugu zako basi wewe upo salama. Hata kama unawasaidia, kuna nyakati wanakusimanga na kukuombea mabaya.

Just imagine mtu anakutatulia shida zako, anakupa connections, anakupa michongo na vitu kama hivyo, lakini akiondoka, unaanza kuzungumza kuhusu udhaifu wake.

Kuna wale wa kula vyombo. Unaweza kuwaita rafiki zako kwa ajili ya kupiga nao stori mbili tatu huku mkipiga moja baridi moja moto. Watakuja na mtakaa pamoja mnabadilishana mawazo. Ukiondoka kwenda chooni, wanabadilisha mazungumzo: "Sijui kazifuma wapi mbwa huyu, leo mbona tutakoma!"

Usione wanakupamba ukawaona ndiyo marafiki, wanakumaliza sana usipokuwa nao. Wengine wanakupamba kwa sababu wameuona udhaifu wako upo hapo. Si unajua kuna wenzetu wengine wana kilema cha kupenda kusifiwa? Sasa wakigundua una kipaji hicho na bahati nzuri ukawa na mafanikio kimaisha, usijisahau.

"Ukitaka hela yake yule bwege wee mpambe tu, hata milioni anakupa."

Ninachojaribu kusema hapa ni kwamba, jitahidi kwa kadiri unavyoweza, kuishi maisha yako. Usije ukajikondesha bure kwa kujiona huna kitu. Kitu kikubwa sana ambacho Mungu amekujaalia ni afya, hivyo vingine vinapatikana ukiweka bidii.

Au usijione una kasoro hii na kwamba watu wanakuzungumzia sana. Puuza hayo mawazo. Uwe na kasoro, usiwe na kasoro, watu hawataacha kukusema.

Hebu fikiria, pamoja na upendo wote ambao Yesu anasemwa alikuwa nao, lakini bado watu walimtia ubaya, wakamuadhibu kikatili na kumuua. Sasa wewe ni nani hata uachwe?

Pambana na maisha yako, kila mtu kimpango wake!

 

 

 

No comments