UKARIBU NA CHOKI ULIVYONIPONZA TWANGA PEPETA

NI wakati ule
African Stars ipo katika ubora wake, ile Twanga Pepeta yenyewe ikiwa na nyota
wake kibao, ikiwa imesheheni kila idara.
Ile Twanga ambayo
kila mpenzi wa burudani ya muziki aliipenda na kuufanya uwanja wao wa nyumbani
pale Mango Garden Kinondoni uwe haukauki nyomi ya watu kila Jumamosi. Jumapili
watu pia walijaa sana viwanja vya Leaders Club nyakati za mchana na usiku
ulimalizika kwa mashabiki wa Temeke na viunga vya jirani kujivinjari pale TCC
Chang'ombe.
Twanga pepeta
iliyokuwa ina -shine mbele ya bendi zingine kali kama FM Academia ya Nyoshi el
Saadat, TOT ya Ramadhan Masanja 'Banzastone', Mchinga Sound ya Adolph Mbinga na
Roggart Hegga, Akudo Impact ukiachilia mbali Msondo na Sikinde.
Asha Baraka 'Iron
Lady' aliifanya bendi yake kuwa bora ambayo iligeuka na kuwa ndoto ya kila
mwanamuziki kuitamani. Kumbuka ile safu kali ya uimbaji chini ya Ally Choki,
Jessica Charles, Salehe Kupaza, Luiza Nyoni (Mbutu) na Hamis Amigolas.
Kulikuwa na mpiga
ngoma anaitwa MCD na mpiga gitaa Abuu Semhando. Kama kuna eneo ambalo bendi ile
ililipatia, basi ni katika ile unenguaji. Acha kabisa, kulikuwa na Aisha
Madinda na Lilian Internet, walikuwa mastaa wakubwa sana enzi hizo.
Nilikuwa mwandishi
wa habari za michezo na burudani wakati huo. Nilifahamiana na wanamuziki wengi
na baadhi yao kujenga ukaribu hata katika maisha nje ya muziki. Miongoni mwa
watu nilioelewana nao sana alikuwa ni Ally Choki mwenye majina mengi ya utani
kama Mzee wa Farasi, Mzee wa Kijiko, Mwarabu wa Kibaha, Kamarade na kadhalika.
Kuna nyakati ambazo
Choki ndiye alikuwa ni nyota mkubwa kabisa katika kundi hilo, licha ya
wanamuziki wote wa bendi hiyo kuwa mastaa. Wanamuziki wote wangepanda jukwaani
lakini Choki alikuwa wa mwisho na ndiye ambaye angetunzwa sana na mashabiki
kuliko wenzake.
Kutokana na ukaribu
huo, nami nikawa naandika mara kwa mara habari zake na za bendi yake, ingawa
pia niliandika na za wanamuziki na bendi zingine. Kama ambavyo ilitokea katika
kumbi zote, niliingia bure kwa sababu ya kazi yangu. Maana licha ya kuburudika,
lakini pia ningetoka na habari ya kuweza kuandika kesho yake.
Ikatokea siku moja,
Ally Choki alijiondoa Twanga na kuanzisha bendi yake, Extra Bongo 'Next Level'
ambayo alisaidiwa uendeshaji na mtu mmoja anaitwa Fikiri Madinda. Japo ilikuwa
ni bendi changa, lakini jina la Choki liliibeba.
Ikatokea kupata
umaarufu mkubwa ghafla na hivyo kuonekana kama mshindani wa African Stars. Baada ya Choki kuondoka
African Stars, nikaanza kuona dalili za 'kufungiwa vioo' na Asha Baraka ambaye
kabla ya hapo, tulikuwa tukielewana sana.
Ingawa nilijua
ananinunia kwa sababu ya Choki kuhama, lakini sikuona mimi nahusika vipi na
kuhama huko, lakini nikaamua na mimi kukausha, lakini maisha yanaendelea.
Sikuacha kuandika
habari za Twanga wala wanamuziki wake, lakini pia niliandika kwa kasi ileile
zile zilizoihusu Extra Bongo na wanamuziki wake.
Siku moja katika
miaka ile ya katikati ya 2000, kama ilivyo desturi, Jumamosi usiku yapata kama saa
nne hivi, nilienda Mango Garden. Kwa kuwa walinzi wengi wa pale walikuwa wananifahamu,
waliniruhusu kuingia.
Lakini ndani,
nikazuiwa. Aliyenizuia kuingia alikuwa ni kaka yangu, mzee Abuu Semhando.
Akanishika kifuani kisha kwa upole kabisa akaniambia.
"Sikiliza
ndugu yangu, Mkurugenzi ameagiza ukija tusikuruhusu kuingia, mimi sijui nini
kimetokea, ila naomba unielewe."
Mkurugenzi
aliyekuwa anasemwa ni Asha Baraka ambaye nilimuona akiwa amesimama pembeni
akitutazama. Kwa namna uhusiano wetu ulivyokuwa unadorora, sikushangaa.
Lakini nikataka kuwa
mbishi, nikamwambia Abuu. "Kwa hiyo kaka unanizuia mimi kufanya kazi
yangu? Au unafikiri nimekuja kustarehe hapa?"
Akanijibu anatambua
kama niko kazini, lakini yeye amepewa maagizo na hawezi kuyakiuka.
Sikulazimisha, nikamwelewa nikatoka nje.
Sikwenda tena
katika bendi hiyo hadi Ally Choki aliporejea katika bendi hiyo baada ya kundi
lake kusambaratika. Wakati akijiandaa kurejea, nilimwambia sitakwenda kule kwa
sababu bosi wake hanitaki.
Akaniambia yeye
akiwepo nitaingia. Siku mbili kabla hajatangazwa kurudi Twanga, nilikuwa naye
Mango Garden tunakula. Mara akatokea Da Asha (waandishi wengi humwita hivyo),
akatufuata tulipokuwa. Akanisalimia 'hujambo wewe, za siku? Naona uko na rafiki
yako.'
Maisha yakaendelea

Post a Comment