USHIRIKINA WATAJWA KARIAKOO DERBY
BAADA ya tambo
nyingi za kila namna kutoka kwa wababe wa soka la Tanzania, Yanga na Simba
zinazotoka eneo moja la Kariakoo, jijini Dar es Salaam, hatimaye, kwa jinsi
isivyotarajiwa, halikupigwa pale Uwanja wa Benjamin Mkapa, kama ilivyopangwa
Mei 8, 2021.
Awali, mchezo huo
ilikuwa upigwe saa 11 jioni. Mashabiki kutoka kila pembe ya nchi na jirani
walijitokeza uwanjani kuanzia majira ya asubuhi hadi mchana wa saa nane,
liliposikika tangazo, sambamba na kwenye page za klabu zote mbili kuwa mchezo
huo umesogezwa mbele hadi saa moja usiku.
Klabu zote mbili
zilithibitisha kupata taarifa hizo za kusogezwa mbele kwa muda. Katika taarifa
rasmi ya Shirikisho la soka Tanzania TFF, zilisema suala hilo limetokana na wao
kupokea maelekezo kutoka Wizara ya Habari, Michezo, Utamaduni na Sanaa.
Yes, kikanuni, TFF
ipo chini ya Wizara hii. Wakati Simba ilikubaliana na jambo hilo la kusogezwa
mbele kwa muda, wapinzani wao, walikataa. Yanga walisema watapeleka timu yao
uwanjani kwa saa za awali, kwani taarifa ya kusogezwa kwa muda, lilifanyika nje
ya matakwa ya kanuni.
Kwamba, ili mechi
iweze kusogezwa mbele ya muda wa awali, taarifa inapaswa kutolewa kwa klabu
husika, angalau si chini ya saa 24 kabla ya muda wa awali. Kwa kanuni hii,
Yanga walikuwa sahihi.
Kwa kuzingatia
hilo, Yanga iliwasili uwanjani kwa muda wa awali na baada ya kufanya taratibu
zote ingawa hakukuwa na mwamuzi, ilipotimia saa 11.30, baada ya kusubiri kwa
dakika 15 ili wapinzani wao watokee, wakaondoka kabisa uwanjani kurejea kambini
kwao.
Simba waliwasili
uwanjani kwa muda wa mabadiliko, lakini wakiwa uwanjani wakipasha, walisikia
tangazo lililosema kuwa mchezo huo umeahirishwa hadi itakapotangazwa tena. Kama
ilivyokuwa kwa Yanga, Simba nao wakapanda gari lao na kurejea kambini kwao.
KIMBEMBE KINAANZIA HAPO.....NANI ANAHUSIKA?
TFF kupitia kwa
Rais wake, Wallace Karia, anadai wao walipokea maagizo kutoka wizarani kuwa
mchezo huo usogezwe mbele kwa vile isingewezekana kuwa na matukio mawili ya
kitaifa kwa wakati mmoja.
Ikumbukwe kuwa
wakati mchezo huo ukienda kuanza saa 11 jioni, siku hiyohiyo Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, alikuwa mgeni rasmi katika shughuli ya uzinduzi wa kitabu
cha Rais wa Awamu ya Pili, Mzee Ali Hassan Mwinyi, shughuli ambayo pia
ilihudhuriwa na Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete.
Hata hivyo, TFF
ilisema Bodi ya Ligi, ambayo ndiyo msimamizi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, ndiyo
itatoa taarifa rasmi.
Baadaye, Kiongozi
wa Shughuli za Serikali Bungeni, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, aliitaka wizara
na taasisi zinazohusika na sakata hilo, kutoa ufafanuzi wa haraka, ikiwa ni
pamoja na namna gani walionunua tiketi watakavyorudishiwa fedha zao.
Kufuatia kauli hiyo
ya Waziri Mkuu, Bodi ya Ligi imetoa taarifa ambayo hata hivyo, haina tofauti za
mwanzo ambazo zimekuwa zikitolewa, huku ikishindwa kutaja ni nani hasa na
sababu zipi, zilizosababisha fedheha hiyo kwa familia ya soka nchini.
Wakati sakata hilo
likiwa bado limewachanganya mashabiki wa soka nchini, ambao wanasubiri kujua
mtu hasa aliyetoa amri ya kusogezwa kwa mchezo huo na sababu zake, maneno
yamekuwa mengi baina ya watani hao wa jadi.
Shabiki mmoja
kutoka Bagamoyo, ambaye hakutaka jina lake kutajwa, lakini akisisitiza yeye ni
mtu wa ndani wa mojawapo ya klabu hizo anaibuka na simulizi hii...
"Unasikia
bwana, jamaa zetu walikuwa wanajua kabisa kuwa game hii inaenda kula kwao, kwa
hiyo walijaribu kila mbinu, lakini kila wakirudi mezani, ubao ulikuwa unasomeka
kwa wao kupoteza.
"Mara ya
mwisho kuchungulia, wakakuta wanapigwa WIKI. Ikawa hamna namna. Ndipo mwenzao
mmoja, akaja na wazo la kumtumia mtu wa nje yao ili aharibu mambo. Ndiyo
akapendekeza MTU AHARIBIWE AKILI AHARIBU MCHEZO.
"Ndipo huyo
jamaa, bila kujifahamu, kwa nafasi yake, akajikuta akiinua simu na kuwapigia
TFF akitaka mchezo huo usogezwe mbele. Tunasikia baada ya hao wenzetu kupata
ile taarifa ya kuahirisha mechi, walirukaruka kwa furaha wakijua mipango yao
imekubali.
"Ndipo sasa
wakawa wamepata pa kutokea. Waliposikia na sisi tumekubali mabadiliko ya muda,
wakazidi kushangilia kwani hilo ndilo hasa walilolitaka. Ndiyo maana
wakakomalia kuvunjwa kwa kanuni na hivyo kuepuka kipigo.".....
Shabiki mwingine
yeye anadai ukweli ni kwamba timu zote mbili zingeweza kushuka dimbani na
kuucheza mchezo huo, lakini kitu ambacho watu walikuwa hawajui ni kuwa kila
aliyetaka muda wake alifaidika na matokeo.
"Mechi ile kama
ingepigwa ule muda wa awali, Simba alikuwa anatota, tena kwa bao nyingi, ndiyo
maana nin kama Mnyama alifurahi sana kubadilishwa kwa muda, kwani wazee wa
milingotini wanasema, kwa mchezo ule kupigwa usiku, Wekundu walikuwa
wanashinda.
"Sasa ndiyo
maana unaona Yanga ambayo ilikuwa ishinde mchana, ikakataa kucheza usiku na
Simba ikafurahia mchezo huo kuahirishwa muda wa awali.
UKIACHANA na imani hizo za kishirikina, mchawi
wa mchezo huo ni TFF na Bodi ya Ligi. Period!

Post a Comment