DIAMOND PLATNUM TUNAMKUZA WENYEWE


Diamond Platnumz On Breaking Into The U.S. Market | GRAMMY.com


KWAMBA Diamond Platnum ni msanii mkubwa wa muziki wa kizazi kipya, siyo jambo la kutia mashaka tena. Amethibitisha hivyo mara nyingi na kwa namna zote, ndani na nje ya uwanja.

Ndani ya uwanja, Diamond ndiye msanii mwenye mafanikio zaidi kimuziki, kwani aina ya muziki wake na video zake, zimemfanya kuwa msanii ghali zaidi kuliko wote hadi sasa katika tasnia hiyo.

Ndiye msanii ambaye ili kumchukua aweze kufanya onyesho, kwampasa anayemhitaji kutoboka sana mfukoni, tofauti na wasanii wengine. Hii ndiyo sababu inayomfanya kutoonekana katika matamasha yaliyozoeleka, yanayowakutanisha wasanii karibu wote maarufu.

Diamond alishaacha kuonekana kwenye tamasha maarufu la Fiesta, ambalo wajuzi wa mambo wanasema ndiyo sababu ya kumfanya msanii huyo kuanza kupigwa zengwe na nyimbo zake kutopigwa katika kituo kimoja kikubwa cha redio na televisheni kinachohusishwa na uendeshaji wa tamasha hilo.

Sababu kubwa ni malipo. Inasemekana msanii huyo alidai fedha nyingi kuliko wengine ambazo ziliwashinda na hivyo kuondolewa. Diamond ndiye pia msanii mwenye mialiko mingi nje ya nchi kimuziki na jambo lingine, ndiye msanii ambaye siyo tu amewashirikisha wasanii wengi wakubwa wa nje, lakini pia ndiye msanii aliyeshirikishwa zaidi na wasanii wakubwa wa nje kuliko wote Tanzania.

Jambo ambalo linapelekea kumfanya msanii huyo kuwa ghali, maarufu na mkubwa kuliko wote kwa sasa, ni kutokana pia na namna video zake zinavyofanya. Video zake zinadaiwa kuwa zina gharama kubwa zaidi kuliko za wasanii wengine.

Siyo tu zina gharama kubwa, lakini pia zinatajwa kuwa na ubora wa hali ya juu, kwa namna ambavyo wanenguaji wake wanavyovaa, nguo nzuri, za bei mbaya na kwenye maeneo mazuri, lakini pia watengenezaji wa video zake ni wenye uzoefu, wenye vifaa bora na bei kubwa.

Nje ya uwanja, Diamond Pllatnum ni msanii mkubwa kwa maana halisi, kwani ana mafanikio mengi ya kifedha. Ndiye msanii anayetumiwa kutangaza kampuni nyingi na kubwa kwa malipo mazuri kuliko msanii mwingine ye yote. Au kwa lugha ya kisanii, ndiye msanii mwenye ubalozi wa brand nyingi.

Ndiye msanii pekee nchini anayemiliki chombo cha habari, akiwa ni mmiliki mwenza wa Wasafi Media, yenye redio na televisheni ambayo ndiyo inayosikilizwa na kufuatiliwa zaidi na vijana kwa sasa. Pia ana mtandao anaouza nyimbo za wasani wote nchini.

Ndiye msanii mwenye lebo yenye mafanikio makubwa kuliko lebo zote nchini, akiwa ni bosi wa wasanii zaidi ya wanne, wote wakiwa ni wakubwa. Katika lebo yake ya Wasafi, anawamiliki wasanii RanVany, Mbosso, Lavalava, Zuchu.

Ndiye msanii mwenye tamasha lake binafsi, linalojulikana kama Wasafi Festival, ambalo lilipaswa kuwa linafanyika kila mwaka, lakini kutokana na matukio kadhaa, limeshindwa ku-mantain.

Mafanikio haya ya Diamond, ndiyo yanayowafanya mashabiki wengi kumkuza zaidi, kwani hivi sasa kila wanapotajwa wasanii bora kwa kila jambo Afrika, macho yao kuangalia namba ambayo Diamond Platnum atakuwa ameshika.

Wakitajwa wasanii wenye fedha nyingi zaidi Afrika, mashabiki wa Tanzania huangalia kama Diamond yupo na inapotokea hayumo, wanaomshabikia hutilia mashaka orodha hiyo, wakati mahasimu wake hushangilia.

Kwa nini mahasimu wake wanashangilia? Wanashangilia kwa sababu kwa ndani ameshashinda kila kitu, hana tena wa kumlinganisha naye. Hofu ya mahasimu ni kumuona akichomoza Afrika na baadaye duniani.

Wakitajwa wasanii wanaofuatiliwa zaidi mitandaoni, macho ya mashabiki wa Tanzania huangaza kuona kama jina la Diamond litakuwepo na inapotokea halipo katika nafasi ya Kumi Bora, huanza kutilia mashaka ukweli wa habari hizo.

Kama kawaida, mahasimu wake hushangilia na kumuona kuwa si lolote si chochote kwa Afrika.

Kitu ambacho mashabiki hawakitambui ni kwamba kile kitendo tu cha kumtazamia msanii huyo kuwa anaweza kushika nafasi katika chati za Afrika au hawezi, maana yake ni kwamba hizo ndiyo levo ambazo anatarajiwa awe. Manaa yake pia ni kuwa kwa levo za Bongo, ameshatoboa kila tobo.

 

 

 

No comments