UNANIJUA MIMI NI NANI?


mngereza pic



NILIKUTANA kwa mara ya kwanza na marehemu Godfrey Mngereza (aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa BASATA) mwanzoni mwa mwaka 2020. Ilikuwa ni katika jengo la Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, ndani ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es Salaam.

Hatukuwa tunafahamiana kabla, ingawa mimi kama mwandishi wa michezo na burudani, nilimtambua kwa nafasi yake na mara kadhaa, nimewahi kuwasiliana naye kwa simu nikihitaji ufafanuzi wa jambo.

Katika jengo hilo linalotoa huduma bora kabisa kwa wagonjwa wa moyo hapa nchini, mimi nilikuwa nimeenda kumpa 'hope' mke wa mdogo wangu, aliyekuwa amelazwa hapo akisubiri kufanyiwa upasuaji siku tatu mbele. Katika hema ambalo wagonjwa na ndugu hulitumia kusubiria, nilikuwa nimekaa na mdogo wangu mwenye mke.

Baadaye, wakatokea watu wawili ambao sikuwafahamu wala kuwatilia maanani, wakasalimiana na mdogo wangu huyo, dhahiri wakionyesha kufahamiana. Kisha akanitambulisha.

"Bro, huyu hapa ni shemeji yangu, mdogo wake mke wangu na huyu ni mumewe, anaitwa Mngereza. Huyu ni mtwasi."

Nikatabasamu, tukapeana mikono kusalimiana. Tukawakaribisha vitini, mazungumzo ya pamoja yakaanza. Muda wa kusalimia wagonjwa ulipofika, ni mtu mmoja tu kwa mgonjwa ndiye anaruhusiwa, kwa hiyo mdogo mtu akapanda juu, sisi watatu tukabakia hemani.

Mdogo wangu akaibuka tena. "Bro, kwa kazi yako nadhani huyu utakuwa unamfahamu au kumsikia, anafanya Basata, ni bosi pale. Mtwasi, kaka yangu ni mwandishi wa habari, nyie watu kuna sehemu mnakutana."

Ghafla fahamu zikanirudia, nikamkumbuka. Yeye hakuweza kunitambua, ingawa nilipomkumbusha kuhusu ishu mbili tatu nilizowahi kumpigia, naye akakumbuka, tukawa sasa ni ndugu...

Tukaendelea na mazungumzo mengine ya kawaida. Tukaanza na jengo lile. Jinsi ambavyo Kikwete alivyofanya jambo la maana kusimamia ujenzi ule. Kama unadhani tatizo la moyo ni dogo hapa nchini, ukifika pale utatoa machozi ukiona umati wa watu wanaougua magonjwa ya moyo na ndiyo utajua kama huduma hizi zilikuwa zinapatikana India, ni kwa kiasi gani tumepoteza watu wengi waliokosa uwezo wa kifedha.

Wengi wa wagonjwa wanaojazana pale, kimuonekano tu, hawawezi kugharamia shilingi milioni tisa (kwa bei ya miaka miwili iliyopita) ya matibabu ya moyo kule India. Hapo ni matibabu pekee, hujazungumzia kuhusu usafiri, chakula na malazi kwa siku si chini ya 14. Bravo sana mzee wa Msoga.

Tukazungumza siasa. Jinsi John Pombe Magufuli alivyokuwa 'ananyoosha' nchi, lakini wezi wa mali ya umma wakiongezeka, licha ya nidhamu ya kazi kurejea.

Ni katika eneo hili la nidhamu ya kazi kurejea, ndipo aliponieleza jambo lililonifanya kwanza nimkumbuke leo, lakini pia nimsifu, kwa sababu katika miaka hiyo ya 'unanijua mimi nani' linaonekana kama gumu kutokea.

Lilimhusu msanii mmoja mkubwa kutoka nje ya Tanzania. Huyo msanii alikuwa amealikwa na kituo kimoja cha redio kwa ajili ya tamasha ambalo walikuwa wameandaa. Kwa mujibu wa taratibu, wenyeji hao walipaswa kupata kibali cha Basata kinachomruhusu mwanamuziki huyo kufanya shoo nchini. Walifanya hivyo na Basata kupitia Mngereza, ikaidhinisha kibali hicho..

Siku kadhaa mbele, mdau mmoja wa muziki, kutoka kituo kingine cha redio, alifika ofisini kwa Mngereza na kutaka kupata kibali cha msanii yuleyule kwa ajili ya onyesho waliloandaa, mbaya zaidi, kwa siku ileile ambayo tayari kibali kilishatolewa kwa redio ile ya kwanza.

Mngereza akakataa, akitoa sababu za msingi kabisa kuwa jambo lile lisingewezekana kwa sababu tayari ameshatoa kibali kwa watu wengine kwa msanii yuleyule na siku ileile.

"Jamaa alinitazama kama anayeniuliza kama ninafahamu yeye ni nani. Nikamsisitizia kuwa jambo lile halitawezekana. Aliniambia nisijali, mimi nitoe tu kibali mambo mengine atayamaliza yeye, nikasema no, hayo mambo ya yeye kuyamaliza, mimi ninao uwezo wa kuyazuia yasitokee," alisema Mngereza.

Basi, akasema jamaa akatoka ofisini kwake lakini akimuahidi kuwa wangekutana tena ili kulimaliza suala lile. Akasema usiku wake, akapigiwa simu na bosi wake (Kimuundo, BASATA ipo chini ya Idara ya Maendeleo ya Utamaduni/Sanaa katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo), akimtaka kufika ofisini kwake kesho yake.

Anasema alijua simu ile ni matokeo ya msimamo wake kwa jamaa wa ile redio. Na kweli, kesho yake, ofisini kwa bosi wake, alimkuta yule jamaa na ishu ikawa kama walivyozungumza jana yake.

"Nilimweleza ukweli bosi wangu kwamba jambo lile lisingewezekana kwa sababu zilezile nilizompa jamaa jana, lakini bosi akasisitiza niandike tu kibali, mambo mengine yatakayotokea watajua namna ya kuyamaliza.

"Kwa kuwa maadili yanakukataza kubishana na mkubwa wako wa kazi nikamkubalia. Akaniambia niende na huyo jamaa nikamwandikie kibali. Tukatoka, wakati tukiwa kwenye lifti tunashuka, nikamwambia jamaa, siwezi kumpa hicho kibali kwa sababu mimi ndiye nitawajibika endapo lolote litatokea," alisema Mngereza.

Jamaa akashtuka na kuniuliza nasemaje, nikamwambia kama ulivyosikia. Akashuka haraka na kurudi kwa bosi kusema, mara nikapigiwa simu nirudi ofisini, nilipofika akaniuliza nimemwambia nini huyu mtu, nikasema bosi huyu ni kijana mwenzangu, nilikuwa namtania nashangaa yeye amechukulia siriazi.

Nikatoka ofisini hapo nikiwa na msimamo uleule. Pamoja na kuwa yule ni bosi wangu, lakini yeye si mamlaka ya uteuzi wangu. Zilikuwa zimebaki siku mbili tu haya matamasha yafanyike na redio zote zilikuwa zinamtaja msanii huyo kuwa atashiriki kwenye tamasha lao ambalo bahati mbaya pia muda ulikuwa ni uleule.

Kwa kuwa nilijua nitasumbuliwa, nikaamua kuzima simu. Huyo jamaa akatuma mtu ofisini kwangu akiwa na bahasha, nikacheka sana nikamwambia mrudishie mwambie mshahara wangu unanitosha. Wale jamaa wa ile redio ya kwanza wakaniuliza hili jambo liko vipi, nikawaambia hata mimi sielewi, lakini mimi nimetoa kibali kwao tu.

Wale watu wa redio wakapelekana mahakamani. Lakini Mngereza alisema kwa huzuni kubwa "Basi bwana, siku zikawa zimeisha, yule msanii kweli akaja, lakini amini usiamini, huyo msanii alienda kufanya tamasha kwa wale jamaa ambao sikuwapa kibali na sijajua kesi ya madai ya fidia ya ile redio nyingine iliishaje."

Kuna watu katika hii nchi hawana cheo chochote serikalini, lakini wanaweza kufanya chochote na wasifanywe chochote.

Godfrey Mngereza alifariki ghafla Desemba mwaka jana akiwa Dodoma kikazi ambako licha ya kukimbizwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa huo, lakini juhudi za kumuokoa hazikufanikiwa. Mungu mlaze mahala pema peponi Amina.

 

 

 

 

No comments