KWA NINI WATU WANASHANGILIA SABAYA KUSIMAMISHWA?

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amemsimamisha kazi Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya kwa kile alichosema, kupisha uchunguzi juu ya tuhuma zinazomkabili.
Rais alichukua
uamuzi huo jana na katika mitandao ya kijamii, habari hiyo imepokewa kwa hisia
tofauti, wengi wakionekana kufurahishwa, ingawa hakuna popote palipotajwa
tuhuma zinazomkabili ni zipi hasa.
Hata hivyo, kwa
mujibu wa wachangiaji kwenye mitandao mbalimbali, Sabaya ambaye alikuwa mmoja
kati ya viongozi vipenzi wa hayati Rais John Magufuli, anachukuliwa kama mtu
aliyekuwa amejawa na jeuri ya kimamlaka.
Kama Mwenyekiti wa
Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Hai, Sabaya analaumiwa kwa kutochukua
hatua stahiki kwa matukio kadhaa yaliyotokea wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu
uliopita, ikiwemo kushambuliwa kwa msafara wa aliyekuwa Mgombea Urais wa
Chadema, Tundu Lissu.
Aidha, Sabaya pia
alituhumiwa na Mwenyekiti wa chama hicho cha upinzani, Freeman Mbowe, kwa kitendo
chake cha kumfuata eneo alilokuwepo, akiwa na silaha za moto wakati wa kampeni
hizo, akiwa na nia ya kumdhuru, ambapo watu kadhaa waliokuwa karibu naye
walikamatwa.
Baada ya hatua hiyo
kuchukuliwa na mkuu huyo wa nchi, ambaye katika siku zake za mwanzo za uongozi wake
anaonekana kuungwa mkono na wananchi wengi, wapo wanaotaka hatua kama hiyo
ichukuliwe kwa viongozi wengine zaidi, ambao wanaonekana kushabihiana na
Sabaya.
Wakuu wa mikoa
miwili ambao bado wapo katika nafasi zao ndiyo wanazungumzwa zaidi, wakimtaka
rais kuwachukulia hatua, kwani nao wanatajwa kutumia vibaya nafasi zao wakiwa
katika ofisi za umma.
Ma RC hao vijana,
wanadaiwa kuwa na kauli zisizo za kiuongozi, kujaa ubabe, wenye kebehi na wasio
na staha kwa wananchi, ambao badala ya kuwaunganisha kuwa taifa moja, wao
wamekuwa wakiwabagua na kuwagawa kwa misingi ya kiitikadi.
Licha ya wakuu hao
wa mikoa ambao bado wapo ofisini, katika mitandao hiyo ya kijamii, wananchi pia
wanataka wakuu wa mikoa mingine miwili, ambao kwa sasa hawapo ofisini, nao
wachukuliwe hatua kwa makosa wanayodaiwa kuyafanya wakiwa katika utumishi wa
umma.
Mabosi hao ambao
nao ni vijana, pia walikuwa ni 'watoto wa mfalme' wakati wa uongozi wa Hayati
Rais wa Awamu ya Tano, John Pombe Magufuli. Katika mitandao, viongozi hao
wanadaiwa kuwa wakati wao, walijawa na jeuri, majivuno, kutoheshimu sheria na
pia, waliendeleza dhambi kubwa ya kuligawa taifa kwa misingi ya kiitikadi.
Katika kundi la
wanaotakiwa kusimamishwa na kuchunguzwa, pia wanatajwa viongozi wawili
waliowahi kushika nafasi nyeti ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), wakidaiwa
kuwa washauri wakuu wa Mwenyekiti. Kwa sasa makada hao hawako katika nafasi
zao.

Post a Comment