UKIONA WANASHANGILIA ANGUKO LAKO, UJUE KUNA SHIDA

KUNA watu wapo mitaani wanashangilia kitendo cha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan, kumsimamisha kazi aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazomkabili.
Tuhuma
zinazomkabili hazijawekwa wazi. Chereko za wanaoshangilia jambo hilo unaziona
wazi kule mitandaoni, kuanzia Twitter, Instagram, Facebook, Jamii Forum na hata
kwenye makundi mbalimbali ya WhatssAp.
Kwa nini
wanashangilia? Wanashangilia kwa sababu aliwaalika wafanye hivyo siku ya anguko
lake. Yes, aliwatengeneza watu na akawaweka tayari kushangilia siku kama ya
jana ilivyotokea. Lakini siyo wanaoshangilia tu, aliwatengeneza hata wale
walioguswa na kujisikia vibaya baada ya uamuzi huo kuchukuliwa.
Sabaya alipewa
nafasi ya ukuu wa dola wa wilaya. Ni cheo kikubwa kinachomfanya kuwa ndiye
muamuzi wa mwisho katika mambo yote yanayohusu wilaya yake. Ndiyo maana,
kuthibitisha ukubwa wa nafasi yake, yeye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi
na Usalama wilayani mwake, wakimaanisha awe mtu wa mwisho kuamua linapokuja
suala la usalama.
Matumizi ya nafasi
yake hiyo, ndiyo yanayowafanya watu leo washangilie, bila kujali kuwa hajafutwa
kazi, isipokuwa amewekwa tu pembeni kwa muda ili tuhuma zake zichunguzwe,
zikithibitika ndipo maamuzi zaidi yachukuliwe, lakini akionekana hana hatia,
anarejea katika nafasi yake.

Maana halisi ya
wale wanaoshangilia ni kuwa mambo aliyokuwa anayafanya, hayakuwapendeza. Ni
yapi hayo? Ni ngumu kujua kwa sababu ukiwa katika nafasi ya kuwa muamuzi, siyo
kila utakachoamua kitawapendeza watu wote, wapo watakaoumizwa na wale
watakaonufaika.
Kimaadili, kiongozi
anatakiwa achukiwe na wanaopenda kupindisha mambo, kwa manufaa yao. Hawa
wanaweza kuwa wabadhilifu, wezi, wanaotumia vibaya ofisi za umma na watu wa
aina hiyo, ambao kimsingi, huwa ni wachache katika taasisi.
Inapotokea watu
wengi wakachukizwa na matendo yako ukiwa ofisini, maana nyepesi ni kuwa wewe
kiongozi ndiye unayefanya mambo yasiyokubalika.
Sabaya ni mmoja
kati ya vijana walioaminiwa na kupendwa na hayati Rais wa Awamu ya Tano, John
Pombe Magufuli. Pengine kwa maagizo au kwa kujikomba, alitekeleza majukumu yake
kwa namna isiyopendeza, akihubiri ubaguzi kwa itikadi za kisiasa. Wapinzani
badala ya kuonekana kama wakosoaji wenye nia nje na nchi yao, wakageuzwa adui.
Lakini siyo tu
aliwabagua wapinzani, pia alizidisha mikogo na jeuri za mamlaka, akiwajibu
aliowaongoza kwa namna alivyotaka. Hata kwenye majukwaa ya kawaida, alipenda
uongozi wa kuamrisha badala ya ule wa kushirikisha.
Sabaya aliuchukulia
uteuzi wake wa kuwa Mkuu wa Wilaya kama kukabidhiwa rungu. Lugha nzuri zaidi
hapa ni kusema cheo kilimfanya akengeuke. Na hapa, vijana kadhaa waliwaangusha
wenzao mitaani, wakionekana kuwa malimbukeni wa uongozi, kwani badala ya wao
kuongoza kisasa na kuwaonyesha wazee kuwa WANAWEZA, wenyewe ndiyo wakaja kuwa
kikwazo na hatari kwa dunia ya utandawazi.
Hapa hakuwa Sabaya
peke yake. Paul Makonda, Ally Hapi, Mrisho Gambo, Richard Kasesera na Albert
Chalamila nao wanaingia katika kundi hili. Waliwaangusha sana vijana kwa
kushindwa kukidhi matakwa ya zama zao.
Tulizoea kuwaona
wazee ndiyo wakiishi na dhana ya kuamini katika vyeo vyao vya umma, lakini hawa
wakaleta ujana kuwa kero kwa wenzao. Fikiria mkuu wa mkoa, tena kijana, anaenda
kwenye kituo cha redio akiwa na askari wenye silaha, kisa jambo lake,
NASISITIZA, jambo lake halikwenda alivyotaka.
Ni heri kituo hicho
kingekuwa kimekwamisha maendeleo ya mkoa wake, ingawa nayo pia haikumstaili
kukifuata na silaha. Angalia ulimbukeni wa vyeo, akakataa hata kuomba radhi kwa
kosa hilo la dhahiri la kimaadili!
Hata hivyo,
kulikuwa na vijana kadhaa pia walifanya vizuri katika zama hizohizo za Magufuli
na wamebakia kuwa mifano hadi sasa. John Mtaka, Jokate Mwegelo na Godwin Gondwe
wanawakilisha.
Hawa hawakuwahi
kuripotiwa kuwa na uongozi wa kuwazidi kichwani ingawa kwenye maeneo yao ya
utawala kulikuwepo wapinzani na watu wasiokubaliana nao.
Hakuna kijana
mwenye akili timamu, awe ndani ya CCM au Upinzani, kama hana maslahi binafsi ya
moja kwa moja, anayependa kumuona Makonda akirejea kwenye uongozi ndani ya nchi
hii. Mrisho Gambo hali kadhalika.
Na huku nje, watu
wanasubiri anguko la hawa wengine waliobaki huko, ambao wanaamini wao wamekuwa
viongozi kwa sababu wameumbwa tofauti na wenzao, wakisahau kwamba nafasi hizo
za kisiasa hazina mwenyewe.

Post a Comment