UFUTA EKARI TANO YA SHAMBA DARASA LASHINDWA KUVUNWA NAMTUMBO
NA STEPHANO MANGO, NAMTUMBO
BAADA ya kutumika kwa shilingi milioni mbili kwa ajili ya kulima
shamba darasa la kuwashawishi wakulima kujiingiza kwenye kilimo cha ufuta, Halmashauri
ya Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma imeshindwa kuvuna kutokana na ukosefu wa
fedha.
Ofisa Kilimo wa halmashauri hiyo Laurance Ndaka pamoja na
mkuu wa idara ya kilimo ushirika na umwagiliaji, Joseph Mbilinyi waliiambia
ojuku1 blog kuwa idara iliomba fedha kwa Mkurugenzi kiasi cha shilingi milioni
moja ili kukamilisha zoezi la kuvuna na kujenga sehemu ya kuweka ufuta huo
pamoja na kazi ya kuupiga lakini tangu April mwaka huu imekuwa kimya.
Walisema Idara ya kilimo wilaya ya Namtumbo iliomba fedha hizo
kupitia vikao halali vya kisheria vya Halmashauri kulima shamba la maonyesho
kwa wakulima wa zao la ufuta ili wananchi waweze kujifunza kupitia shamba hilo
la ekari tano.
Na kwamba wazo hilo liliungwa mkono na vikao halali
vya kisheria ambapo awali Halmashauri ilitoa shilingi milioni 2 kwa
ajili ya kusafisha shamba, kulima pamoja na palizi hali iliyowafanya baadhi ya
wakulima kuvutiwa kutembelea shamba hilo kujifunza.
Wakizungumza na blog hii, wakulima waliolima shamba hilo Saidi
Kiokola na Sijawa Omari wameshangazwa na hali ya shamba hilo kutovunwa na
kuuacha ufuta ukikaukia shambani na kuikosesha Halmashauri fedha nyingi ambazo
zingepatikana kutokana na kuuza kwa ufuta huo kwa mfumo wa stakabadhi ghalani.
Kiokola alidai gharama iliyotumika kwa Halmashauri ya milioni 2
na ile ya kuvunia shamba hilo ingerudi na kupata faida kubwa licha ya yeye
kutokuwa mtaalamu ila kutokana na kuona hali ya uzalishaji ulivyo na kiasi cha
pesa ambacho kingeweza kupatikana kwa makadirio.
Akizungumza kwa njia ya simu, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri
ya Wilaya ya Namtumbo Evance Nachimbiya alikiri kuwepo kwa shamba darasa la
ufuta lenye ukubwa wa heka 5 ambalo lilianzwa kulimwa mwezi disemba mwaka jana
katika eneo la Nafco wilayani humo.
Nachimbiya alisema kuwa awali idara ya kilimo walileta dokezo la
kuomba fedha shilingi milioni 3 kwa ajiri ya kulima na kuvuna ufuta
katika shamba hilo, ambapo kwa awamu ya kwanza walipewa shilingi
milioni moja kwa ajiri ya maandalizi na kulima shamba hilo na baadae tena
walipewa milioni moja kwa ajiri palizi na mbolea na kufanya jumla kuwa na
milioni mbili.
"Nashangaa kukusikia kuwa ufuta huo umekauka na haiwezekani
kuvunwa kwa sababu mie sikuwepo kwa zaidi ya wiki mbili, nilikuwa safarini
kikazi mjini Dodoma, labda mpaka niwasiliane na Ofisa kilimo kwa ajiri ya
maelezo zaidi," alieleza Nachimbiya.

Post a Comment