SERIKALI KUKAGUA MADUKA YA DAWA YANAYOUZA VIDONGE KUZUIA MIMBA


HAHAHAHAHAH INDUSTRY: MZEE NA BINTI YAKE MJAMZITO

SERIKALI imesema itaanza kufanya ukaguzi katika maduka ya dawa muhimu na yatakayobainika kuuza vidonge vya dharura vya kuzuia ujauzito (P2) na vya kutoa mimba (misoprostol) bila cheti cha daktari yatachukuliwa hatua

Pia, wananchi wametakiwa kutoa ushirikiano ili kuyabaini maduka hayo na kupunguza madhara yanayoweza kutokea.

Msajili wa Baraza la Famasia nchini, Elizabeth Shekalaghe alisema hayo katika mkutano mkuu wa chama cha wafamasia (PST) wenye kauli mbiu “Wataalamu wa famasia ni muhimu kuboresha upatikanaji wa dawa bora Tanzania.”

Shekalaghe alisema P2 na misoprostol ni dawa za cheti zinazoruhusiwa kuuzwa katika famasi lakini kwa cheti cha daktari.

“Pamoja na changamoto tunazokabiliana nazo katika udhibiti wa uuzwaji holela wa dawa, imebainika dawa hatarishi nikimaanisha misoprostol na P2 zimekuwa zikitumika kinyume na makusudio ya Serikali, tunatarajia lazima zitolewe na cheti cha daktari,” alisema Shekalaghe.

Alitoa wito kwa wananchi kutoa taarifa pale watakapokuta dawa zinazotolewa au kuuzwa kinyume bila cheti sababu ni kinyume cha sheria na kanuni zinazosimamia utoaji wa dawa za cheti.

“Nawakumbusha wataalamu wote hata katika yale maduka yanayoruhusiwa kuuza hizi dawa, ni vizuri kuweka kumbukumbu sahihi ili mamlaka zinapopita zifahamu hizi dawa zilitolewa kwa misingi ipi,” alisema Shekalaghe.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima aliagiza hatua zichukuliwe kwa wafamasia na wauzaji wa maduka ya dawa wanaokiuka taratibu na kanuni hivyo kuweka maisha ya Watanzania kwenye hatari.

“Iweje dawa zinazohitaji cheti cha daktari zitolewe kinyume na kanuni, chukueni hatua kali kwa wote wanaokiuka, pia rekebisheni sheria na kanuni zinazodhibiti suala la uandikaji na utoaji wa vyeti vya dawa,” alisema Dk Gwajima.

Mfamasia Mkuu wa Serikali, Daudi Msasi alisema maduka ya dawa muhimu ndiyo yanayouza dawa ambazo hazikubaliki na yanaongoza katika kuuza P2.

“Wananchi wanalalamika wafamasia tumeshindwa kuwalinda dhidi ya dawa hizo, matokeo yake watoto wanazitumia ndivyo sivyo, kumbukeni maduka haya vyeti vyenu vya taaluma vimetumika kuyafungua, lakini ndiyo yanayoongoza kuuza dawa kinyume na sheria,” alisema Msasi.

Daktari bingwa wa magonjwa ya kinamama na uzazi kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Living Colman alisema vidonge vya P2 hutumiwa na mtu ambaye amekutana na mwenzake bila kujua yupo katika kipindi cha hatari cha kupata ujauzito.

“Au itokee kama amebakwa lakini kwa vyovyote na si yawe matumizi ya mara kwa mara,” alieleza Dk Colman.

Alisema matumizi ya mara kwa mara ni kufanya mrundikano wa uzazi wa mpango katika mfumo wa kizazi ambao husababisha madhara baadaye.

“Anayekusudia kutumia mara kwa mara ina maana anajiwekea homoni nyingi mwilini ambazo zinaweza kuvuruga mfumo wa uzazi na pengine akashindwa kupata mtoto,” alitahadharisha Dk Colman.

No comments