NDUMBARO: VIONGOZI ZINGATIENI MATUMIZI BORA YA ARDHI

 

WAZIRI DKT. DAMAS NDUMBARO: HATUWEZI KUWAUA NYANI WANATULETEA DOLA - 2 Eyez  Media

NA STEPHANO MANGO, TUNDURU

WAZIRI wa Maliasili na Utalii Dkt Damas Ndumbaro, amewataka viongozi wa Serikali wilayani Tunduru mkoanin Ruvuma, kusimamia mpango wa matumizi bora ya ardhi ili kukomesha vitendo vya uvamizi wa maeneo yaliyotengwa kwa kwa ajili ya uhifadhi wa wanyama na shughuli za kitalii.

Waziri Ndumbaro ametoa kauli hiyo katika kikao kazi  na viongozi  wa wilaya hiyo kuhusiana na mikakati ya kukabiliana na tatizo kubwa la uvamizi wa wafugaji  kwenye hifadhi na shughuli mbalimbali za kibinadamu katika maeneo yasiyoruhusiwa.

Alisema, viongozi wa serikali ndiyo wenye jukumu la kusimamia matumizi ya ardhi kwa kuweka utaratibu ambao utakomesha vitendo vya  wafugaji kupeleka  na kuishi kwenye hifadhi za Taifa na mapori yaliyotengwa kwa ajili ya utalii.

Ndumbaro alisema, kuanzia sasa serikali kupitia wizara yake haitakuwa na mzaha kwa watu watakaovamia na kufanya shughuli za kibinadamu kwenye maeneo hayo, na kuwataka wananchi katika wilaya hiyo kufuata sheria na kuheshimu mipaka iliyowekwa  ili kuepuka matatizo.

Ameiagiza Halmashauri ya wilaya kutoa kipaumbele kwa idara ya maliasili kwa kuipatia vifaa na kuitengea fedha za kutosha ili iweze kutekeleza vyema majukumu yake badala ya kuona kama  haina mchango wowote.

Alisema, kila halmashauri hapa nchini ina idara ya maliasili lakini jambo la kusikitisha idara hiyo imeachwa kama mtoto yatima hivyo kushindwa kutekeleza wajibu wake kama sheria inavyotaka.

Aidha, amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Julius Mtatiro kwa kazi nzuri anayofanya  kusimamia uhifadhi wa maliasili na kuwataka watendaji wengine wa serikali kuiga utendaji kazi  wa mkuu huyo wa wilaya badala ya kumuacha akihangaika pekee yake.

Mbunge wa jimbo la Tunduru Kaskazini Hassan Zidadu Kungu alisema, kati ya mwaka 2019/2020 zaidi ya wananchi 24 wameuawa na wanyama wakali hususani Tembo wanaotoka hifadhini na kwenda kwenye makazi ya watu.

Alisema, kutokana na tatizo hilo ipo haja kwa wizara ya maliasili kuwa na mikakati mbadala ya kukomesha matukio ya wananchi kuuawa na wanyama wakali na kuweka mipaka  itakayoonesha sehemu za hifadhi na makazi ya wananchi ili kuepusha muingiliano kati ya watendaji wa wizara na jamii.

Kungu, ameiomba wizara ya maliasili  kuhamisha kikosi maalum cha kuzuia ujangili kanda ya kusini (KDU) kutoka Songea  ambako hakuna  hifadhi wala shughuli yoyote ya utalii na kuhamishia  shughuli zake wilayani Tunduru ambako ndiko sehemu sahihi.

Mkuu wa wilaya ya Tunduru Julius Mtatiro alisema, katika kipindi cha mwaka 2018/2020 jumla ya watu 78 wamekamatwa wakifanya shughuli za ujangili kwenye hifadhi ya Taifa ya Nyerere.

Mtatiro ameipongeza wizara  ya maliasili na utalii kwa  mpango wake wa kutoa kifuta machozi na kifuta jasho kwa waathirika wa wanyama wanaoharibu mazao na wanaosababisha vifo kwa wananchi.

Hata hivyo alisema, changamoto kubwa katika kukabiliana na vitendo vya ujangili na uvamizi kwenye hifadhi ni upungufu wa watumishi wa idara ya maliasili kwenye halmashauri kwani waliopo ni tisa kati ya mahitaji ya watumishi 31.

Alitaja changamoto nyingine ni uvamizi wa mipaka kutokana na shughuli za kibinadamu, vitendea kazi,wafugaji kuingiza makundi makubwa ya mifugo ambapo ameiomba wizara hiyo kuisaidia katika operesheni za kuondoa mifugo kwenye hifadhi ya Nyerere.

 

 

 

 

No comments