LUKUVI AITWA MGOGORO WA ARDHI KATI YA DC MSTAAFU NA WANANCHI MCHOMORO
NA STEPHANO MANGO, NAMTUMBO
WANANCHI kutoka
katika koo 16 wa Kijiji cha Mchomoro kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya
Namtumbo Mkoani Ruvuma wamemuomba Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
William Lukuvi kuingilia kati utatuzi wa mgogoro wa ardhi zaidi ya heka 700
kati yao na Mkuu wa Wilaya hiyo Mstaafu Luckness Amlima ili waweze kuendelea na
shughuli zao za kimaendeleo kuliko mateso ambayo wanayapa hivi sasa ya kufunguliwa
kesi kila wanapoenda katika mashamba hayo.
Wakizungumza na waandishi
wa habari waliofika katika kijiji hicho jana wawakilishi wa koo 16 zenye
familia zaidi ya 68 walisema kuwa mgogoro huo umedumu kwa zaidi ya miaka mitano
sasa na kwamba viongozi wa kijiji na Wilaya wamekuwa wakipuuzia mgogoro huo kwa
sababu zao binafsi hali ambayo inaashiria kuwa ni kumpendelea mkuu huyo wa
Wilaya mstaafu kwa kuwa alisaidiwa na baadhi ya viongozi kujimilikisha maeneo
hayo kinyume na utaratibu.
Akizungumza kwa niaba ya koo
hizo Rashid Malamaye alisema kuwa kiongozi huyo amevamia katika maeneo yao ya
asili ambayo wao walikuwa wanayatumia kwa shughuli za kilimo na ufugaji toka
miaka mingi lakini cha kushangaza kwa sasa wanataka kudhulumiwa.
Malamaye alisema kuwa
katika mashamba hayo kulikuwa na nyumba za nyasi lakini zimechomwa moto, mazao
ya muda mrefu aina ya minazi, machungwa, migomba na mihogo lakini cha
kushangaza mazao hayo yamefyekwa bila wao kujulishwa na kuwekwa walinzi ambao wamekuwa
wakiwapiga wananchi ambao wanakwenda katika mashamba hayo na kuwafungulia
mashataka mbalimbali kwa lengo la kuwanyanyasa
“Tumeshtushwa sana na
kitendo hicho cha uharibifu wa mazao yetu na uvamizi wa mashamba hayo ambayo
yapo katika maeneo ya mihane katika kitongoji cha Nyerere na mwekezaji ambaye
aliwahi kuwa mkuu wa Wilaya bila sisi wenye maeneo kujulishwa na hata
tulipolalamika kwenye uongozi wa kijiji na Wilaya hakuna hatua zinazochukuliwa
dhidi yake”alisema Malamaye
Naye Issa Languka alisema
kuwa mara baada ya kutokea kwa uvamizi huo walitoa taarifa katika uongozi wa
kijiji na kwenye uongozi wa Chama cha Mapinduzi lakini majibu waliyoyatoa kuwa
mwekezaji huyo yupo kihalali bila kufafanua sheria ipi au mkutano gani wa
hadhara ambao ulihalarisha mwekezaji huyo kupewa heka zaidi ya 700 na kijiji
kinyume na sheria za ardhi.
Languka alisema kuwa
inasikitisha kuona kuwa viongozi wa kijiji badala ya kulinda raia na mali zao
wao wamekuwa chanzo cha kutengeneza migogoro kinyume na kiapo chao cha uadilifu
ambacho waliapa na mara kadhaa wamekuwa wakitoa taarifa za uongo kuhusu mgogoro
huo.
Alifafanua kuwa hali
iliyopo kwa sasa siyo nzuri kwani wenye mashamba wamekuwa wakienda kufanya
shughuli zao wanakamatwa na kufunguliwa kesi mbalimbali katika kituo cha polisi
Wilaya ya Namtumbo hali ambayo inazidisha uhasama kati ya wananchi na mwekezaji
huyo.
Alisema kuwa kutokana na
kitendo hicho walimwandikia Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Christine Mdeme kumjulisha
madai yao ili aweze kuchukua hatua stahiki kwani mwenendo wa viongozi wa wilaya
ya Namtumbo dhidi ya mgogoro husika hauridhishi na hawana imani nao kwani ni
zaidi ya mwaka wa nne sasa wameshindwa kuukomesha.
Kwa upande wake
Mwenyekiti wa kijiji hicho Said Mohamed Mkalela alikiri kuwepo kwa mgogoro huo
na kusema kuwa hatua zinaendelea kuchukuliwa ingawa wananchi hao wamekuwa
wakikosa imani kutokana na kuchelewa kumalizika kwa mgogoro huo.
Mkalela alisema kuwa wao
waliingia madarakani mwaka 2019 lakini nyaraka zinaonyesha mwekezaji huyo
alipata eneo la heka 40 kihalali toka mwaka 2016 katika maeneo ya Namambigi na
sio Mihane, lakini hatua za kutatua mgogoro huo zinaendelea ingawa wananchi
wanateseka.
Naye Mkuu wa Wilaya
mstaafu Luckness Amlima alipotafutwa ili kuelezea mgogoro huo
alisema yeye hautambui waulizwe viongozi wa kijiji husika na sio yeye kwani
yeye amepewa na viongozi wa kijiji hicho kwa kufuata utaratibu waliokubaliana.
Kwa upande wake Katibu
Tawala wa Wilaya hiyo Aden Nchimbi alikiri kuusikia mgogoro huo na kuagiza
wahusika kwa kushirikiana na afisa ardhi wa Halmashauri kukutana na kuumaliza
mgogoro huo ili kuwaondolea kero wananchi.
Kwa upande wake Mbunge wa
Jimbo la Namtumbo Vita Kawawa alipotafutwa ili aweze kuzungumzia mgogoro huo
alisema atafutwe baadae kwani kwa sasa yupo kwenye shughuli za Bunge.

Post a Comment