KUELEKEA DERBY YA KARIAKOO, SIMBA NA YANGA



Mech ya leo simba vs yanga

KABLA hawajaja wale wachambuzi wetu wa baada ya mechi na vibwagizo vyao vya WHAT A MATCH!!, WHAT A GOAL!!! kwa uzoefu wangu wa kutazama mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, nina machache nataka kuzungumza nikiutazama mchezo huu kabla haujachezwa siku sita zijazo.

Kwanza tukubaliane kwamba mwenye presha kubwa zaidi katika mechi hii ni Yanga. Kuna sababu kadhaa za kwa nini awe na presha, lakini chache ni hizi..

1. Matumaini ya ubingwa yamebakia bahati nasibu..

Kulikuwa na matumaini makubwa ya mabingwa hawa wa kihistoria kuibuka na ubingwa msimu huu, hasa baada ya wafadhili wao wakubwa, GSM kuamua kuingia kwa miguu miwili na kusimamia mchakato mzima wa usajili wa wachezaji na benchi la ufundi. Walifanya kazi kubwa na kila mmoja ameona.

Usajili wa wachezaji wa viwango kama Calinyo, Fiston, Yocouba, Tonombe, Saido na Dickson Job. Hawa ni wachezaji walioongeza thamani ndani ya timu na haikushangaza, ilipoongoza Ligi na hivyo kuweka hai matumaini ya mashabiki. Baada ya kuongoza kwa muda mrefu, taratibu ikaanza kupoteza makali na hatimaye hadi unaposoma makala haya, kimahesabu, Yanga iko nyuma kwa pointi kumi kwa Simba.

Kwa hiyo, hii ni moja kati ya sababu za msingi sana za kuipa Yanga presha. Wote ndani ya Yanga wanajua, wachezaji, viongozi na mashabiki, kwamba ubingwa kwao msimu huu ni miujiza na njia pekee ya kujiliwaza ni ushindi dhidi ya Simba.

Ili Yanga wapumue na wawe na cha kusema, ni LAZIMA waifunge Simba Jumamosi ijayo. Watashindaje mchezo huo, ni KITENDAWILI.

2. Kutocheza soka la kuvutia...

Presha nyingine inayokumbana nayo Yanga kuelekea mchezo huo, ni ukweli kwamba wamekuwa hawana soka la kuvutia kama ilivyo kwa wapinzani wao. Yes mpira ni magoli, lakini katika wakati ambao soka pia ni biashara, burudani inahusika sana kwa mashabiki.

Wachezaji, viongozi na mashabiki wa Yanga wataingia katika mchezo huo wakijua wapinzani wao wanacheza soka la kuvutia kuliko wao, hivyo njia pekee ya kuwatuliza, ni KUWAFUNGA. Hata ucheze mchezo wa kuvutia vipi, ni lazima utoke na matokeo chanya, vinginevyo, unakuwa kama Arsenal ya enzi za mwishoni mwa zama za Arsene Wenger!

3. Imani ya mashabiki kwa kocha mpya

Baada ya kumuondoa kibaruani kocha Cedric Kaze, Yanga waliutangazia umma kuwa Juma Mwambusi, ambaye ametumika sana msimu huu kama Kocha Msaidizi, atapewa timu awe Kaimu Kocha Mkuu hadi mwisho wa msimu...na Of course mashabiki walielewa.

Kwamba klabu itafute kocha bora taratibu ili aje aichukue timu aanze nayo msimu ujao. Mwambusi amefanya kazi yake vizuri akipata matokea ya kawaida. Sijui nini kimetokea, ghafla viongozi wamemleta kocha mpya na kumpa timu.

Yes, CV yake inaonyesha ni kocha mzuri, pengine kuliko Gomez, kwani ana vikombe kama sita hivi katika ufundishaji wake wa soka la Afrika, ingawa naye kama alivyo mwenzake wa Simba, wana leseni ya Uefa.

Ameiongoza Yanga katika mechi mbili. Yanga imeshinda mechi zote mbili chini yake, lakini zote  ikionekana kupambana kwelikweli. Ni matumaini ya wana Yanga kwamba timu yao iwe inawatisha wapinzani ndani na nje ya uwanja.

Presha hii ya kocha, ipo zaidi kwa viongozi, kwa sababu, kwa vyovyote vile, kufungwa na Simba ni kutokufaa kwa kocha huyo. Kama kuna eneo viongozi walicheza karata zao 'kwa kubahatisha', ni kumruhusu huyu jamaa akae pale benchi kabla ya mechi hii. Ili wabebwe tena na mashabiki, ni LAZIMA MNYAMA AFE KWA MKAPA.

Siku zote, hakunaga mechi ndogo au isiyo na umuhimu zinapokutana timu hizi, bila kujali nani yupo katika nafasi gani kwenye msimamo wa Ligi. Ukitazama, unaiona Simba kama timu inayoingia ikiwa haina mashaka yoyote, kwani hata ikifungwa, bado itaendelea kubakia pale juu, hata kama ni kwa muda.

Inaingia uwanjani ikiwa mabega juu kila idara. Licha ya kuwa imecheza mechi mbili chini ya wapinzani wao, lakini ndiyo wanaongoza Ligi Kuu, tena wakiwa juu kwa pointi nne.

Katika michuano ya kimataifa, imeingia robo fainali ya Kombe la Ligi ya  Mabingwa Afrika, tena ikiwa imeweka historia ya kuongoza kundi lao, ambalo lilikuwa na bingwa mtetezi Al Ahly. Unaweza kubeza mafanikio haya kwa sababu tu ni shabiki wa Yanga, lakini kiukweli, hii ni hatua kubwa sana katika soka letu la Bongo.

Simba pia inaingia uwanjani ikijivunia uwezo wake wa kuumiliki mpira. Kwa mujibu wa takwimu za kila baada ya mchezo, Simba ndiyo timu pekee iliyokuwa na wastani mzuri wa kumiliki mpira katika mechi zake zote ilizocheza katika Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.

NINI KITATOKEA?

Yanga itaingia uwanjani ikiwa na lengo moja tu, kuibuka na ushindi katika mechi ambayo ikishinda, itakuwa na faida mbili.

Kwanza itapunguza wigo wa tofauti ya pointi na kufikisha saba na pili itakuwa imewapa matumaini upya mashabiki wao. Lakini ni wachezaji gani wataisaidia Yanga? Sina uhakika, lakini nadhani mfumo wa 4-4-2 utawasaidia kusukuma mashambulizi langoni mwa Simba.

Mfumo huu unatengeneza mizani katika safu ya ulinzi na kiungo, kwani viungo hao wanagawika, wawili wakisaidia ulinzi na wawili ushambuliaji. Washambuliaji wa Simba ni wazuri, lakini ni wazito ukimuondoa Konde Boy.

Safu ya Ulinzi ya Yanga inapaswa kuwa na walinzi wenye nguvu, hasa katikati na mmoja anayetumia zaidi akili. Kwangu, Lamine Moro, japo ni mzuri, lakini ana hasira. Huyu asubiri kwanza, aanze yule dogo mrithi wa Cannavaro, Ninja. Kama Dickson Job atakuwa amepona majeraha, huyu anastahili kuwepo uwanjani, kwani licha ya ufupi wake, lakini ana timing za aina ya akina George Masatu.

Kushoto na kulia kwa Yanga sionagi kama wana tofauti sana, kwa hiyo hata wanaocheza sasa, Kibwana na Adeyum wanaweza kuendelea na majukumu yao.

Kiungo cha chini Yanga itahitaji huduma za Mwalimu Mukoko Tonombe na Feisal Salum. Hawa wana nguvu, ari na uwezo mzuri wa kumiliki mpira. Hili ni eneo ambalo Yanga inahitaji watu watulivu mno kiakili, kwa sababu wanakutana na wapinzani wenye uwezo kama wao katika umiliki wa mpira. Hata hivyo, itabidi Feisal apunguze pia presha, maana kuna wakati ni kama anapanik hivi!

Pale katikati, yule dogo mtanashati wa Kireno akisimama na Saido, wanaweza kufanya jambo, hasa kwa kuwa hawa hawana mambo mengi. Wanaweza kukontroo mpira na wana macho ya tai, yenye uwezo wa kuona mnyama aliye umbali wa maelfu ya kilometa.

Wana kile watu wa mpira wanaita penetration passes, yaani kwa kiswahili pasi mpenyezo, ambazo mtu anakutana nazo kwenye nafasi. Itazame ile aliyopewa Yacouba siku Prisons anaanguka pale Sumbawanga kwenye FA Cup.

Yacouba naona kama anajimilikisha ile namba ya Sarpong. Huyu anastahili kuanza na kwa mawazo yangu, aanze sambamba na Deus Kaseke. Kwa nini? Hawa wawili watataka ku-prove kuwa wanaweza kucheza pacha kwa sababu kuna vitu wanafanana, navyo ni ari ya upambanaji.

Kaseke amekuwa na maana kubwa sana anapoingia dakika za mwishoni anazopewa, kiasi cha kujiuliza kwa nini anabakia nje kwa muda mrefu. Khalid Mussa, Haruna Niyonzima, Ditram Nchimbi na Bakari Mwamnyeto ni watu ninaotegemea pia kuwemo ndani ya 18.

Simshauri kocha kumpanga mlinda mlango Metacha...

Kwa Simba, wataingia tayari wakiwa washindi. Ushindi wa Simba Jumamosi si ushindi wa mabao, bali matokeo. Shida kubwa ya Gomez itakuwa ni kujilinda ili asipoteze mchezo, period!

Ushindi wa mabao kwake ni bonasi tu, kwa nini? Wekundu hawana cha kupoteza kwa kupata sare, kwa sababu wataendeleza wigo wao wa pointi kumi dhidi ya Yanga, huku michezo ikizidi kupungua kabla ya ligi kumalizika.

Kwa kuzitazama timu zilizobaki kucheza na Simba kabla ya msimu kumalizika, ni Yanga pekee ndiyo unaweza kuiwekea fedha ya kuishinda Simba na bado bia baridi ikapita bila wasiwasi. Na hii ndiyo mechi ngumu zaidi kwa Simba kuliko zote zilizopita na kubaki.

Kwa maana hiyo, Simba wataingia kwa kujilinda zaidi na bahati nzuri inao wachezaji wa kuliwezesha hilo, kama ilivyotokea katika michuano ya Ligi ya Mabingwa walipofanya hivyo ugenini.

Ili kulifanikisha hilo, Gomez atakuja na mfumo wake wa siku zote akitafuta kujilinda, wa 4-2-3-1. Ikimaanisha walinzi wake wataendelea kuwa ni wale wale kama hakutakuwa majeruhi, Kapombe, Tshabalala, Wawa na Onyango. Pale juu ana machaguo mengi, lakini Mkude, Lwanga na Nyoni wanaweza kuwa chaguo la kuanza na wawili kati yao.

Kiungo cha ushambuliaji pia machaguo ni mengi, lakini uzoefu unatuonyesha Bwalya, Chama na Konde Boy wataingia na kuanza usumbufu kwa Yanga huku mshambuliaji mmoja wa kumalizia, hauhitaji kumtaja jina, kwani yeyote kati ya Kagere, Mugalu na Bocco anafaa.

Bwalya, Chama na Konde Boy pia wanaweza kutumika kurudi nyuma na kujilinda kutoa msaada kama presha itakuwa kubwa kutoka kwa wapinzani wao.

Golini kwa Simba ataendelea kuwepo Manula, ingawa kwangu, siku zote nimekuwa nikimuona Benno Kakolanya kuwa ni bora kuliko Air Manula. Benchini sura ambazo hazitakosekana ni pamoja na Muzamiru, HD, Ndemla, Morrison na Kennedy.

Naitazama kama mechi inayoenda kuwa miongoni mwa mechi bora zaidi msimu huu, kwani timu hizi ndizo zenye wachezaji wengi zaidi wa kigeni kuiko timu zingine, hivyo uzoefu wao kuleta ladha inayotarajiwa na mashabiki.

Hofu yangu pekee, ni waamuzi!!!!

 

No comments