KILICHONIPUNGUZIA USHABIKI KWA SIMBA


Sharif: Sudan midfielder has five matches to earn Simba SC contract |  Goal.com

 NCHINI Tanzania, angalau watu wamegawanyika kwa ushabiki wa timu mbili kongwe, Simba na Yanga. Hawa ni wote, akina baba na akina mama, wazee, vijana na hata watoto. Ingawa wapo, japo kwa kiwango kidogo sana, ambao si mashabiki ama wa Simba au wa Yanga.

Ndivyo hata mimi nilivyokuwa. Niliipenda sana, na bado naishabikia timu hiyo, ingawa si kwa mapenzi kama yale niliyokuwa nayo siku za nyuma, kabla sijaijua undani wa timu hizi zinazotoka Kata moja ya Kariakoo, Ilala jijini Dar es Salaam.

Tokea utoto wangu, nimekuwa ni shabiki wa Simba, yaani ile huniambii kitu. Ilipofungwa, nilikosa raha sana na kila mmoja angefahamu na iliposhinda, furaha yangu haijawahi kuwa na kifani. Tangu nilipopata akili, sijawahi kuacha kufuatilia mambo ya Simba.

Nilianza kuijua timu hii kipindi kile cha mabeki Kihwelu Mussa na Mohamed Kajole hadi nilipokuja kugundua kitu mwanzoni mwa miaka ile ya 2000.

Moja ya matukio makubwa kabisa ninayokumbuka kuhusu Simba ni ahadi ya mmoja wa waliowahi kuwa viongozi wa klabu hiyo miaka ya nyuma, Jabir Shikamkono, aliyeahidi endapo Simba ingefungwa na Yanga angenyoa nywele zake na kuwa upara.

Ikumbukwe miaka ya themanini kuelekea tisini, upara haikuwa fasheni kabisa kwa watu wazima. Lilionekana ni jambo la ajabu kidogo. Ni kweli Simba alipigwa mechi hiyo na Jabir alinyoa kweli kipara.

Mwaka ambao nilikosa furaha kabisa kwa sababu ya Simba ni 1987, ambapo timu hii almanusra ishuke daraja, kama siyo mipango kuinusuru baada ya kuishinda Yanga mechi ya mwisho. Leo naweza kujua sababu za kwa nini Simba ilishinda mechi ile na kwa nini Yanga iliuachia ubingwa ili kuinusuru Simba.

Ikumbukwe mwaka huo Yanga ilikuwa ya moto kwelikweli na Simba mbovu. Kila shabiki wa soka aliamini Mwananchi anakwenda kuchukua 'ndoo' lakini kilichotokea kinabaki kuwa historia.

Mwaka ambao nilikuwa na furaha sana moyoni ni 1993, ambao Simba ilifika fainali za Kombe la Shirikisho wakati huo likiitwa kombe la CAF. Aaah, ilikuwa ni timu ya kibabe sana ile aisee.

Nakumbuka pia tukio la mwaka mmoja kabla ya hapo, 1992, Simba ilishinda fainali za michuano ya Afrika Mashariki na Kati iliyofanyika Zanzibar dhidi ya Yanga. Simba ilishinda kwa penati. Mechi ile ilichezwa usiku na nakumbuka hadi saa sita usiku nilikuwa barabarani na mashabiki wa Simba mjini Dodoma tukishangilia ushindi.

Mwaka 2000 mwanzoni nikaingia katika tasnia ya uandishi wa habari. Kama ambavyo ilikuwa kawaida, nilianza kwa kuripoti habari za mahakama za mwanzo, baadaye nikaingia kwenye kitengo cha Michezo.

Huo ndiyo ukawa mwanzo wa kufahamiana na kuwa na ukaribu na wachezaji, makocha, viongozi wa klabu, viongozi wa mpira wa wilaya, mikoa hadi Taifa, wafadhili, makomandoo na wadau hasa wa mpira.

Miaka hiyo ya 2000 kulikuwaga na michuano flani maarufu sana ikijulikana kama Hedex Cup, ambayo ilikuwa inaratibiwa na kampuni hiyo ya dawa ya kichwa kutoka Kenya. Wakati wa michuano hiyo, jamaa walikuaga wanamleta mwakilishi wao ambaye anaisimamia na mara nyingi kama siyo zote, fainali ilizikutanisha Simba na Yanga.

Huyo jamaa wa Kenya siku nafanya naye mahojiano, nilipomtajia jina langu, akashtuka na kuniuliza kama mimi ni mtu wa Kenya.

Kwa kuwa alikuwa ni mtu muhimu kwangu nyakati hizo za shindano, haraka nikamkubalia, nikimwambia kuwa mimi ni mwenyeji wa Thika na huku nilikuja na wazazi wangu nikiwa mdogo. Akafurahi sana na kuanzia siku hiyo akawa siyo tu mtu wangu wa karibu, bali rafiki kabisa.

Nilipata mambo mengi sana kutoka kwake. Kuna siku alinitaka nimsindikize kwa viongozi wa Simba akakutane nao. Nilimsindikiza hadi Food World wakati huo, mgahawa uliomilikiwa na Kassim Dewji ambaye amewahi kuwa kiongozi kwa nafasi mbalimbali, uliokuwa maeneo ya Posta.

Kwa kawaida, waandishi wengi walikuwa wakifika mgahawani hapo, kwani kwa vyovyote kama hutakutana na viongozi wa klabu hiyo, ambao ni chanzo kikuu cha habari za michezo, basi watakutana na wachezaji wa Simba au hata viongozi wa TFF (FAT) wakati huo.

Mkenya huyo alipofika waandishi wakamdaka, lakini akasema kwa wakati huo hakuwa na cha kuwaambia, labda mpaka kwanza akutane na viongozi wa Simba waliokuwa wakimsubiri. Akanishika mkono nikapanda naye ngazi hadi kwenye ofisi ya Kassim.

Niliwakuta Kassim Dewji (ambaye nilifahamiana naye hata kabla sijawa mwandishi), Crecentius Magori, Evans Aveva na mtu kama Mulamu au Salim 'Try Again', nimemsahau hasa alikuwa nani.

Hao wote walikuwa wananifahamu, baada ya kusalimiana na walipotaka kuanza kikao chao, walinitaka nitoke nje,nilitii lakini yule Mkenya akawazuia, akawaambia anaomba nibaki kama rafiki yake na siyo kama mwandishi.

Jamaa wakamkazia, nikatoka nje nimsubiri. Basi baada ya kumaliza mazungumzo yao, akaja tukaondoka zetu kuendelea na ratiba zingine.

Nikajaribu kumdodosa ili nipate cha kuandika, akaniambia hana chochote kinachoweza kuwa habari, lakini ataniambia mambo waliyojadili ambayo alitaka yasitoke kama habari, nibaki nayo.

Aisee acha kabisa. Sisi tunakaa tunashabikia, wakati mwingine hadi tunapinga (siku hizi wanasema kubet), kumbe watu wanacheza mpira mezani. Ili timu hiyo iende hadi fainali, kila hatua ina kiwango chake cha pesa. Na kama fainali itakutana na Yanga, basi kiwango pia huongezeka. Ngoma inakuja nani afungwe mechi hiyo?....

Nikaanza kufanya uchunguzi wangu kimyakimya ili nigundue kama hali huwa ipo hivyo pia upande wa pili. Nilichogundua ni kwamba kama walivyo wachezaji wa Simba na Yanga, viongozi hawa pia ni marafiki mno nje ya uwanja.

Wakati flani bwana mdogo Athuman Idd Chuji aliondoka Simba na Katibu Mkuu wa Simba wakati huo, Mwina Kaduguda akasema hatacheza tena mpira. Jioni moja nilikuwa na mdau mmoja wa Simba, siyo kiongozi ila mtoa hela mzuri, akapigiwa simu na kiongozi mwenzake wa Yanga (alinionyesha jina la mpigaji kabla hajapokea).

Kwa kuwa aliweka sauti ya juu ili nisikie wanachozungumza nikasikia waziwazi. Yule wa Yanga alimuuliza mwenzake wa Simba, umemsikia Katibu wenu anasema Chuji hatacheza mpira? Yule wa Simba akacheka na kumwambia, achana naye, hatacheza mpira anajua jinsi alivyokuja hapa Simba?

Na kila mtu anajua Chuji alicheza soka la mafanikio sana Yanga. Nini kilitokea sijajua. Kuanzia wakati huo, nikapunguza huo ushabiki wa kutupwa. Sijawahi kukosa raha kwa matokeo yoyote ya Simba tangu wakati huo. Na kama siyo kutumwa kwenda uwanjani kuripoti mechi, au kwenda kwa ajili ya kupata habari za kuziandika gazetini, ningekuwa nimeshaacha zamani kufuatilia mpira.

Tangu nilipoacha kuandika habari za michezo mwaka 2010, sijawahi tena kwenda uwanjani, ingawa nina uhakika wa kuingia bure.

Kidogo sasa hivi naanza kupata hamu mpya baada ya kuiona Simba inavyocheza. Kiwango chake kinakufanya uamini katika uwezo na si mipango. Kama Yanga nayo itajenga kikosi imara na kuanza kucheza mpira, nitaweza hata kwenda uwanjani siku za usoni.

Ushauri wangu kwa mashabiki, muwe na ushabiki wa kiasi, wakati mwingine nyinyi mnapigana, wakubwa wa Simba na Yanga wapo Serena wanakunywa bia!

 

No comments