JIDE ALIVYONIKAGUA KABLA YA KUKUBALI INTERVIEW


Why Lady JayDee won't marry her current boyfriend – Nairobi News


KAZI ya Uandishi wa habari ina mazonge mengi sana, hasa unapojikuta unagusa masilahi ya mtu bila wewe kujua au kwa kutokuwa na namna nyingine ya kufanya ili kuepuka kutomgusa mtu.

Katika hii kazi nilitengeneza marafiki wengi sana, lakini pia sikukosa maadui. Hata hivyo maadui walikuwa ni wachache ambao hata hivyo, nao niliwapata baada ya kuwa marafiki kutokana na kazi hiyo hiyo ya uandishi.

Yaani unajikuta umempata mtu mkaelewana kwa sababu ya uandishi, lakini baadaye mnatofautiana tena kutokana na uandishi huo huo.

Msanii wa muziki wa kizazi kipya, Judith Wambura Mbibo, wengi wakimfahamu kama Lady Jaydee au Jide, ni mmoja kati ya watu niliofahamiana nao na kujenga ukaribu kutokana na uandishi, lakini baadae tukatofautiana kabla ya kurejesha tena ukaribu huo.

Nilimfahamu Jide kipindi kile cha mwanzoni mwa miaka ya 2000, akiwa bado hajachomoza na kujitofautisha na wasanii wengine wa kike. Kipindi kile alikuwa katika vita kali ya kumpata mbabe wa wadada, kwani Rehema Chalamila 'Ray C' alikuwa kwenye chati, Stara Thomas alikuwa ana-shine, Unique Sisters walikuwa hot, hivyo yaani.

Wakati huo nilikuwa katika kampuni moja ya habari ambayo magazeti yake yalipendelea zaidi kudili na watu maarufu na matukio. Kwa watu maarufu, wasanii wa muziki, filamu, komedi walikuwa ndiyo walengwa wakubwa.

Hii ilinifanya watu hawa niwafahamu, niwe nao karibu na ndiyo niliofanya nao kazi. Siku moja nilikutana naye katika ukumbi wa Msasani Club, nyumbani kwa FM Academia akiwa na Profesa Jay.

Enzi hizo ni kawaida sana kukutana na wasanii wa muziki wa kizazi kipya katika kumbi za muziki wa dansi, kwa vile kipindi hicho, FM Academia 'Wazee wa Ngwasuma' na African Stars 'Twanga Pepeta' walikuwa katika kiwango chao cha juu kabisa cha ubora.

Nikasalimiana nao na kuanza kupiga stori. Jide aliniambia kuwa hakuwa akipendezwa na namna magazeti ya kampuni yetu yanavyomuandika, kwani ni kama yanamuonyesha kwa sura ambayo si nzuri kwa jamii.

Nilijaribu kumwelewesha namna ambavyo yeye alipaswa kudili nayo, kwani mara nyingi hakuwa akitoa ushirikiano kwa waandishi ambao walikuwa wakimtafuta ili kutoa majibu au ufafanuzi wa mambo kadhaa, kitu ambacho kinapelekea yeye kuona kama hatendewi haki.

Akaniambia kuanzia siku hiyo, hatataka tena kuongea na mimi kuhusu mambo ya habari, labda kusalimiana tu. Mimi na Profesa Jay tukacheka, lakini Komando alikuwa anamaanisha, mkali kwelikweli. Nikamwambia asijali, lakini atambue kwamba yeye ni staa na watu kama wao ndiyo walengwa wakubwa wa vyombo vya habari, nikimtolea mfano wa jinsi Michael Jackson alivyokuwa akiishi kwa kujificha ficha kwa kuwaogopa paparazi kutokana na ustaa wake.

Na kweli, akanichunia. Maisha yakaendelea, mimi na yeye hazipandi. Tunakutana lakini katika maeneo mengine, ikitokea tukawa uso kwa uso, tunasalimiana na ikitokea vipi, kila mtu anachukua time yake.

Ilikwenda hivyo, ingawa mimi kwa nyakati tofauti, nimeshawahi kuandika makala kadhaa za kusifia kazi za Jide, maana kadiri muda ulivyokuwa unakwenda, yeye akachomoza na kuwa kileleni miongoni mwa wasanii wa kike.

Katika kipindi cha miaka kumi kuanzia 2000, unagundua kuwa Stara Thomas alififia, Ray C alijiondoa katika ushindani na wale wadada wa Unique Sisters wakawa wameamua kuachana na muziki, pale akabakia mkongwe Jide pekee.

Baadaye nikahama pale kwenye ile kampuni, nikahamia nyingine. Hii ilikuwa ya magazeti pia lakini haikuwa na mlengo kama ule wa kampuni ya awali. Hata hivyo sikurejea kwa Jide ili tuendelee kufanya kazi. Tukaendelea hivyo hadi mwaka 2008 hivi nafikiri, nilipohama tena kampuni nyingine.

Nikiwa hapo, bosi wangu akaniambia alikuwa anafuatilia sana kazi zangu na kupendezwa na namna ninavyoandika habari za wasanii. Akanipa orodha ya wasanii ambao alitaka nifanye nao mahojiano ili niandike makala zao gazetini. Kati ya wasanii hao, jina la Jaydee lilikuwamo!

Kwa kuwa sikuwa na namba yake, nikaitafuta na kuipata, nikampigia. Nikamwambia nilihitaji kuonana naye. Akaniambia hajabadili msimamo wake juu yangu, lakini mimi nikamwambia ingekuwa ni vyema tukakutana kwanza, asikilize ninachotaka kumwambia halafu aamue.

Akakubali. Akanipa muda ambao angekuwepo katika hoteli ya Southern Sun, pale katikati ya jiji. Ilikuwa jioni flani hivi, mida kama saa mbili usiku nikafika pale tukakutana.

Jide ni msichana jasiri, mwelewa, mpambanaji na anajielewa. Akaniambia kabla ya chochote, nimwambie kwanza ninachokitaka kutoka kwake maana hajui hasa nimefuata nini. Nikamwambia nahitaji kufanya naye mahojiano (Interview), akacheka sana na kuniuliza kama niko sawasawa.

"Nipo sawa, ni kwamba mimi kule nimeshahama kitambo sana, hivi sasa nipo kampuni nyingine," nikamwambia na kumtajia huko nilikohamia.

Akaniambia hana taarifa za kuhama kwangu na akaniomba kitambulisho ili ajiridhishe. Nikampa, akakipiga picha na kuniambia kwamba hana matatizo na mimi, isipokuwa yeye alikuwa na tatizo na pale nilipokuwa nafanyia kazi.

Tukapanga siku ya interview na hadi ninapokamilisha kukupa kisa hiki, Jide ni mmoja kati ya wasanii wakongwe ambaye bado tuna mawasiliano mazuri ya kikazi.

 

No comments