WAZIRI CHAMURIHO ATAKA TAASISI ZA UJENZI, UCHUKUZI KUWAJIBIKA


Wakurugeni wa Wizara, Wakuu wa Vitengo pamoja na Viongozi wa Taasisi zilizo chini ya Wizara wakimsikiliza Waziri wa Ujenzi na Uchukuz iMheshimiwa Dkt. Leonard Chamuriho (hayupo pichani),  katika kikao kazi kilichowakutanisha viongozi hao jijini Dodoma.


Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Dkt. Leonard Chamuriho, amewataka Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara yake kuhakikisha wanaandaa taarifa kila mwezi zinazoelezea utekelezaji wa majukumu yao ili kusaidia Wizara kufahamu kwa undani utendaji wa Taasisi hizo ikiwemo mafanikio na changamoto zake.

Hayo aliyasema Waziri huyo, jijini Dodoma, katika kikao kazi cha kumtambulisha NaibuWaziri wa Wizara hiyo  Mhe. Mwita Waitara, kwa mara ya kwanza kwa viongozi wa Taasisi hizo ambapo pamojana mambo mengine amesisitiza kuwa Wizara itakuwa inaandaa vikao kama hivyo  mara nne kwa mwaka ili kujadiliana kwa pamoja na kupata tathmini na  mwelekeo wa Wizara katika ufanisi wake wa utendaji kazi.


"Nimeamua leo kuitisha kikao hiki ili kumtambulisha Naibu Waziri kwa  wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara yangu, pia kukumbushana kuhusu utekelezaji wa masuala mbalimbali yaliyo katika Taasisi zao", amesema Waziri Chamuriho.

Aidha, Chamuriho amezisisitiza Taasisi hizo kushirikiana na kuwajibika ipasavyo katika miradi wanayoitekeleza kwani mingi huigusa jamii ambapo  ameongeza kuwa, kufanya hivyo kutapelekea maendeleo kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Mwita Waitara, amewataka viongozi hao wa Taasisi kumpa ushirikiano wa kutosha na kwamba ofisi yake itakuwa wazi kwa ajili ya kupokea ushauri na maoni mbalimbali  lengo likiwa ni kusaidia kufanikisha utekelezaji wa miradi mbalimbali iliyo chini ya Wizara hiyo ili kuleta maendeleo kwa wananchi.

“Naomba Wakuu wa Taasisi wanipe tu ushirikiano wa kutosha na niwabainishie kuwa Ofisi yangu itakuwa wazi wakati wote kwa ajili ya kupokea ushauri lengo likiwa ni kuleta tija na maendeleo kwa wananchi”, amefafanua NaibuWaziri Waitara.

Naye, Msajili wa Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi, Arch. Edwin Nunduma,  amesema kuwa agizo hilo la Waziri la kuleta taarifa za utekelezaji Wizarani litawafanya kuwajibika zaidi kutokana na kuwa Wizara itafuatilia kwa karibu utendaji wao.

"Utaratibu huu ni mzuri, kwani hata  changamoto zikitokea itakuwa ni rahisi kuzitafutia ufumbuzi mapema na  kwa haraka", amesema Nunduma.

Kikao hiki cha siku moja ambacho kimemkutanisha Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mheshimiwa  Dkt. Leonard Chamuriho, NaibuWaziri wa Wizarahiyo, Mhe.Mwita Waitara, Menejimenti ya Wizara hiyo pamoja na viongozi wakuu wa Taasisi 23 zilizo chini ya Wizara hiyo, kilikuwa na lengo la kutambuana na kukumbushana kuhusu uwajibikaji katika Taasisi zao.

Imetolewana Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi



 

No comments