WAITARA AZITAKA SEKTA ZA UJENZI NA UCHUKUZI KUFANYA KAZI KWA PAMOJA
Mtendaji
Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Patrick Mfugale, akiwasilisha
taarifa ya utekelezaji wa Wakala huo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi,
Mwita Waitara (hayupo pichani),katika kikao kazi mkoani Dar es Salaam.
Imeelezwa kuwa mafanikio katika Sekta za miundombinu ya Ujenzi na Uchukuzi nchini ambayo ndiyo roho ya uchumi wa Taifa yatafikiwa tu endapo watumishi na wadau wote wa sekta hizo watafanya kazi kwa ubunifu, nidhamu na uadilifu.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Waitara,
katika kikao kazi na menejimenti za taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo jijini
Dar es Salaam ambapo amesisitiza umuhimu wa kila taasisi kujipima kama zina tija
na ufanisi wake katika jamii unaharakisha maendeleo ya nchi.
“Hakikisheni kazi zinazofanyika zinapimika kwa kuzingatia Mpango wa Maendeleo
2020 - 2025 na miongozo ya viongozi wakuu wa Serikali ili huduma bora kwa wananchi
ziimarike na kuleta nafuu kwa wananchi”, amesema Waitara.
Ameutaka Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), kuhakikisha kuwa nyumba za makazi
zilizopo katika mikoa mbalimbali nchini zinawanufaisha kwanza watumishi wa umma
kabla ya kuzipangisha kwa watu wengine kibiashara ili kuondoa utaratibu wa udalali
unaofanya Serikali kupata mapato kidogo na
madalali kuzikodisha kwa bei ya juu na hivyo kupata faida binafsi.
Ameitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu (LATRA),
kuhakikisha malalamiko, kero na usumbufu kwa wasafirishaji na abiria vinapatiwa
ufumbuzi kwa kuzingatia sheria ili kuiwezesha Serikali kupata mapato stahiki na
kukuza sekta ya usafiri nchini.
Kuhusu miundo mbinu ya barabara na madaraja, Naibu Waziri huyo ameutaka Wakala
wa Barabara Tanzania (TANROADS), kutengeneza mpangokazi wa miaka mitano mitano unaonesha
namna bora ya ujenzi wa madaraja na barabara nchini kote ili kuleta matumaini kwa
wananchi na kuhamasisha huduma nyingine za kiuchumi.
Naibu Waziri huyo amesisitiza kwamba mafanikio katika sekta ya ujenzi na
uchukuzi yatafikiwa haraka kama watumishi, wakandarasi na wadau wote wanaoshiriki
katika miradi ya ujenzi watafanya kazi kwa bidii na kuepuka vitendo vya rushwa.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Patrick Mfugale, amesisitiza
kuwa Wakala huo umejipanga kikamilifu kuhakikisha barabara kuu na za mikoa zinapitika
kwa uhakika katika msimu wote wa mvua za masika.
Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Bw. Masanja Kadogosa,
amemhakikishia Naibu Waziri huyo kuwa huduma za usafiri wa abiria na uchukuzi wa
mizigo kwa njia ya reli zimeimarika na kazi ya ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR)
kati ya Dar es Salaam – Morogoro–Makutupora na Isaka hadi Mwanza inaendelea kwa
kasi
Naibu Waziri Waitara yupo katika ziara ya kikazi ya siku nne (4) katika mikoa
ya Dar es Salaam, Pwani na Tanga ambapo pamoja na mambo mengine atakagua miradi
ya sekta hizo na kuzungumza na watumishi.
Imetolewa
na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Post a Comment