Wenye akili wanatushangaa sana

 


Na Ojuku Abraham

Yes, Taifa linaadhimisha miaka mitatu ya uongozi wa Madame President, Samia Suluhu Hassan ambaye alichukua nafasi kikatiba, kufuatia kifo cha hayati John Pombe Magufuli. Rais wa kwanza mwanamke Tanzania, wa kwanza Afrika Mashariki na miongoni mwa wanawake tisa tu kuwahi kuongoza serikali barani Afrika.

Kwa nafasi yake, anastahili pongezi nyingi kwa namna ambavyo amefanya tofauti na mawazo ya wengi hapo awali ambao kwa miaka mingi, mfume dume umetufanya tuamini kuwa wanawake si watu wa kuwapa kazi nzito wakazifanya ipasavyo. Amethibitisha, kwa kiwango kikubwa, kwamba anaweza kuliongoza taifa letu kuelekea kwenye matarajio.

Yapo mambo ambayo ameshindwa kuyapatia uvumbuzi wa moja kwa moja, ama kwa sababu ya muda, au kwa sababu zilizo nje ya uwezo wake kama kiongozi wa kitaifa. Kushindwa kwake, hakuwezi, kwa namna yoyote kuchukuliwa kuwa ni kwa jinsia yake, bali ameshindwa kama ambavyo Mwalimu Julius Nyerere, Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa, Jakaya Kikwete na JPM walishindwa.

Yes, Mwalimu alishindwa kuikomesha rushwa, akajitahidi kwa kiwango cha kuridhisha kudhibiti ubadhilifu, alimudu, angalau kukazia uwajibikaji miongoni mwa watumishi wa umma na hakuna shaka kabisa kuwa aliishi falsafa yake ya Ujamaa na Kujitegemea kwani aliwezesha ujenzi wa viwanda vingi vilivyotumia malighafi za ndani.

Kila kiongozi aliyeingia, kuna mambo aliweza na yapo yaliyomshinda, kwa hiyo, leo akitokea mtu akisema Madame President ameshindwa kufanya hili, asionekane msaliti au hana adabu. Bali iwe ni changamoto tu ambayo tukiibeba kwa mlengo chanya, itatusaidia kufika tunakoenda.

Katika maadhimisho haya ya miaka mitatu ya mama madarakani, kuna mengi yanasemwa juu yake. Bahati mbaya sana, mengi yanayozungumzwa kufanywa naye, ni yale mazuri tu. Kila kiongozi, wa kila kada, akipata nafasi ya kuzungumza kuhusu miaka hii mitatu, ni kutaja yale mema tu, kana kwamba hakuna mambo ambayo hayakwenda vizuri, kitu ambacho siyo kweli.

Tumejenga utamaduni wa kuwaona wasema kweli kuwa ni maadui. Utamaduni huu unaligharimu sana Taifa na kuwanufaisha watu wachache wanaojificha katika kusifu. Pamoja na mazuri yote yaliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan, lakini bado kuna changamoto nyingi zinazowakabili wananchi wa hali ya chini.

Bado kuna baadhi ya wateule wa Rais Samia wanawadhulumu wananchi wa chini kwa kutumia ofisi za umma. Kuna malalamiko mengi ya wananchi juu ya kunyimwa haki zao na watu wenye fedha ambao wanasaidiwa na wateule hawa wa kiongozi mkuu wa nchi, kwa vile tu wanafaidika na dhuluma hizi.

Bado kuna upigaji mkubwa wa fedha za umma katika nyanja mbalimbali. Maofisa wakubwa wana wakandarasi wao, wanawapa tenda, wanafanya kazi ndogo kwa malipo makubwa. Kuna dhuluma kubwa inafanywa na wenye viwanda kwa wafanyakazi kwa kulipwa kiwango kidogo cha mishahara na wanakaa muda mrefu wakitumika kama vibarua.

Bado viongozi wengi, wakiwemo mawaziri, manaibu wao, makatibu wakuu, wakurugenzi wa idara mbalimbali za serikali, wanaishi kama malaika ili hali wananchi wanahangaika kupata huduma bora za afya, elimu na fursa za kiuchumi zilizo sawa.

Ni kweli, majengo mengi ya shule na zahanati yanajengwa kila kukicha. Lakini je, nguvu kazi ipo? Watumishi wa sekta za elimu na afya, wanalipwa vizuri kiasi cha kuwapa motisha?

Viongozi wanapiga kelele kutaka vijana wajiajiri. Oke, sawa pengine vyuo vya ufundi vimeboreshwa kwa maana ya vifaa vya ufundishaji, lakini je, nchi imeandaa mazingira rafiki ya vijana kujiajiri? Kijana kujiajiri siyo tu kwa sababu ameshapata maarifa chuoni, je kuna mikakati ya makusudi ya kumkopesha, kumuendeleza na kumlinda ili asimame?

Serikali inasema elimu inatolewa bure. Bure hii ni nini? Kule kijijini kwetu wazazi wanatakiwa kupeleka chakula shuleni na hili ni jambo la lazima. Wanachangia majengo ya shule, wanatumia nguvu kazi kuyajenga (wanafyatua matofali, wanashiriki ujenzi, wanachangishwa fedha, lakini ukija Mwenge wa Uhuru, wanatoa takwimu zinazoonyesha majengo hayo yamejengwa kwa mabilioni ya shilingi bila michango na nguvu kazi za wananchi kuainishwa). Kuna michango isiyo na idadi inayobuniwa na walimu. Mbele ya kamera tunasema tunapata elimu bore, lakini ukweli halisi ni kuwa hakuna cha bure.

Haya ni machache, lakini kuna mengi ambayo hayaendi sawa huku mitaani, ambayo hatutaki kumwambia mama ili ayafahamu. Tumebaki kutafuta namna ya kumfurahisha hadi tunamkera, kiasi cha yeye kukataa. Alianza kuwakataa watu wanaojiita chawa. Wakaanzisha vikundi, ambavyo juzi pia kavikataa. Yeye hana vikundi, ni mama wa wote.

Kuna mtindo mbaya ambao unaanza kuwa utamaduni wetu, unakera sana. Ni jambo la ajabu kwamba hata wale tunaoamini ni wasomi, nao wanaingia kwenye mtego huu. KUMTAJA RAIS SAMIA HATA ASIPOSTAHILI!

Unashangaa msiba umetokea mtaani. Ni kawaida kwa watanzania kupeana pole na kushiriki shughuli bila kujali hadhi wala jina. Lakini mathalan, kwa kuwa kuna diwani, mbunge au waziri ameungana nanyi, kwa heshima anapewa nafasi ya kuongea chochote.

Pamoja na kutoa pole kwa wafiwa kama ilivyo utaratibu, atatafuta kila ‘engo’ ili mradi tu amtaje Rais Samia Suluhu Hassan. Jamani, kitu gani hiki? Haya, tupo kwenye sherehe au tafrija za kibinafsi, kwa mfano za kidini au kielimu (mahafali). Mtu katumia gharama zake, amewakaribisha ndugu, jamaa na marafiki!!

Anatokea mtu anatafuta nafasi ya kumtaja Rais bila sababu zozote. Hili jambo, pengine hatufahamu, lakini linatuondolea sana heshima mbele ya jamii kwa sababu watu wanazungumza.

Ni kawaida sasa, hawezi kusimama kiongozi ye yote wa kisiasa, kuanzia mjumbe wa shina, mwenyekiti wa kitongoji/kijiji, diwani, mbunge au Waziri, atasimama na kuzungumza bila kumtaja Rais Samia. Sawa ni kiongozi wetu, lakini mbona kuna wakati tunamtaja bila sababu?

Huko nyuma, ukiachana na yale Mabilioni ya Kikwete yaliyoliwa na wajanja, ulikuwa huwezi kusikia eti Rais Mwinyi, Mkapa au Kikwete ametoa mabilioni ya shilingi kujenga zahanati, shule, barabara, maabara, soko au ofisi za umma.

Ilifahamika kwamba fedha hizi ni za serikali. Lakini leo hii, waziri kabisa ambaye huku tunaambiwa ni msomi, anasimama mbele ya hadhara na kusema anamshukuru rais kwa kutoa mabilioni ya fedha kwa ajili ya ujenzi wa hiki au kile. Kwa nini shukurani hizi zisiende kwa serikali ambayo kiuhalisia ndiyo yenye fedha?

Tunamtaka rais wetu ajue, hawa wanampamba ili kuficha ubadhilifu wao, kuficha matumizi yao mabaya ya ofisi za umma, kuficha ushiriki wao katika kuwadhulumu wananchi haki zao ikiwemo mashamba/nyumba, kusaka teuzi na vyeo. Vyema akajua kuwa katikati ya kupambwa kwake, watu wanaugulia sana maumivu kutoka kwa baadhi ya wateule wake!

 

No comments