Jaji Mkuu, Waziri Jerry Silaa na Paul Makonda wasikilizwe

 

KWA nyakati tofauti, viongozi wawili wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali wameonyesha kutoridhishwa kwao na namna Idara ya Mahakama inavyoshughulikia migogoro ya Ardhi nchi nzima.

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Paul Makonda akiwa katika ziara yake ya kusikiliza kero za wananchi katika mikoa mbalimbali, wengi wakionekana kusononeshwa na namna watu wenye fedha wanavyowadhulumu viwanja, mashamba na ardhi kupitia hukumu zinazotolewa na mahakama za ngazi mbalimbali.

Katika kile alichoonyesha kukubaliana nao, Makonda aliwashauri wananchi kutokimbilia mahakamani mara wapatapo matatizo kwenye migogoro ya ardhi, kwani huko watu wenye fedha wana nafasi nzuri za kushinda mashauri hayo.

Kuonyesha kwamba anamaanisha anachokisema, Mkuu huyo wa Mkoa wa Dar es Salaam wa zamani, aliwaambia kuwa yeye binafsi aliwahi kudhulumiwa nyumba na watu wakamshauri aende mahakamani, lakini akafikiri na kuona kuwa kutokana na ukwasi wa mdhulumishi wake, asingeweza kushinda endapo angeenda mahakamani.

Kana kwamba hilo halitoshi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa, ambaye anakutana na changamoto nyingi hivi sasa katika migogoro ya ardhi, naye amewashauri, siyo tu wananchi, bali hata maofisa ndani ya wizara yake, kutowashauri wananchi kwenda mahakamani kwenye ishu za migogoro.

 
Waziri Silaa amefafanua kuwa katika Sekta ya ardhi, ina jukumu la kitu kinaitwa administrative justice (inatoa haki ya kiutawala), kwamba yapo mambo na wataalam wa wizara ya ardhi ameshawaagiza waache tabia ya kugeuka washauri wa sheria wa wananchi.

Anasema unakuta raia anakuja na vielelezo vyote muhimu vya umiliki wa ardhi, lakini eneo lake anakalia mtu mwingine, hivyo anavyokutana na wataalam wa wizara, badala ya kutoa haki ya kiutawaka, wanageuka kuwa washauri wa sheria, wanawaambia wananchi waende mahakamani, ameongeza kuwa jambo hilo ameshalipiga marufuku.

Waziri Silaa amezidi kusema kwa kuwa mahakama inasikiliza kila mtu, hivyo wapo watu ambao hutumia mwanya huo kuchelewesha haki za wengine au kuwasumbua watu wengine hasa ambao hawajui sheria au hawana nguvu ya kupambana kimahakama. Hivyo suala hilo ni misuse of court process.

Amemalizia kwa kusema kuwa Wizara ya Ardhi itamsikiliza mwananchi yeyote na maadam atakuwa na vielelezo vyote na pale penye haki za watu watazitoa.

Hawa ni viongozi wawili wenye dhamana kubwa ndani ya chama na serikali. Wanatoa kauli hizi, siyo kwa ajili ya kubeza kazi na wajibu wa mahakama katika kutenda haki, lakini kimsingi, wanatoa ishara ya kutokuwepo kwa uwiano mzuri wa haki kuonekana imetendeka.

Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma Hamis anaweza kuwa, huko aliko, akawa na mawazo tofauti juu ya kauli za viongozi hawa. Lakini kwa manufaa yake binafsi kama binadamu na kiongozi wa Idara nyeti kabisa ya uhai wa binadamu, ni vyema tukamweleza kuwa pamoja na lugha ya kistaarabu iliyotumiwa na viongozi hao, ukweli ulio wazi ni kuwa mahakama zetu zinatenda haki kwa wenye fedha.

Ni ngumu kuthibitisha kauli yangu hii, kwa sababu mimi si mwanasheria na hukumu hutolewa kwa vifungu vya sheria. Pamoja na kwamba kila hukumu sisi wengine hutajiwa vifungu hivyo vilivyopelekea hukumu iliyotolewa, lakini tumeshuhudia mara nyingi, kwenye kesi inayomhusu mlalahoi na mwenye nazo, matajiri huibuka videdea.

Si mara zote hushinda kwa rushwa. Isipokuwa kwa uwezo wao kifedha, huweza kuweka mawakili wazuri, wakati mwingine zaidi ya mmoja na hivyo kupelekea kuwa na nguvu katika mwenendo mzima wa kesi.

Lakini upo ushahidi wa kimazingira kuwa katika migogoro ya ardhi, watu wenye fedha, huwahonga baadhi ya watumishi wa serikali wasio waaminifu, ambao hutoa nyaraka za uongo zinazowaongoza kwenye katika mabaraza ya ardhi na mahakama, ambako huko nako, watumishi wenye tamaa, hushawika kwa fedha na kukuta shauri ambalo lingeisha siku moja, linachukua miaka mingi na hukumu kutolewa kwa uonevu.

Tumeshuhudia, jeuri ya wenye fedha, wakivunja nyumba za watu wakati suala likiwa mahakamani. Hii ni katika kuwavuruga tu na mara nyingi, jambo hili hulindwa na vyombo vya dola.

Ninao mfano kuthibitisha hili. Familia ya Charles Forodha, inayoishi katika Mtaa wa Kihonzile, Bunju B jijini Dar es Salaam, wiki iliyopita ilivunjiwa nyumba yao, wakati shauri linalohusu mgogoro baina yao na jirani, ambaye anamiliki fedha nyingi, likiwa bado mahakamani.

Mwathirika huyo hakutaarifiwa kimaandishi kama sheria zinavyotaka juu ya kusudio la kuvunjwa kwa nyumba hiyo na wala hakupewa hata ruhusa ya kutoa vitu vyake ndani. Matokeo yake vibaka wakagawana vitu vyake, ikiwa ni pamoja na kuibiwa kiasi cha shilingi milioni nne zilizokuwa ndani.

Dalili kwamba kulikuwa na rushwa katika jambo hilo, wavunjaji hao walisimamiwa na maofisa wa polisi pamoja na mtendaji wa mtaa, ambao wanafahamu vyema sheria zinasema nini kwa tukio kama hili.

Ujumbe wa Waziri na Katibu wa Uenezi wa chama, siyo kubeza kazi za idara hii muhimu kabisa katika uhai wa wananchi, lakini ni kuutaka uongozi wa Mahakama kuliona tatizo hili kwa ukubwa wake na kulifanyia kazi.

Zile kauli za ‘si uende mahakamani’ ni kama kejeli tu, kwa sababu katika hali halisi, mtu akiwa hana fedha, hakufai.

Ukishafikishwa mahakamani, ili mtuhumiwa aweze kupata dhamana, inatakiwa barua kutoka serikali ya mtaa, ambayo hawezi kupewa bila kutoa hela. Akifika nayo mahakamani, ni lazima pia atoe hela ili aachiwe kwa dhamana, licha ya kumpeleka mtu wa kumdhamini.

Huu umeshakuwa kama utamaduni. Haki inayopatikana mahakamani ni pale wanaposhtakiana wakubwa kwa wakubwa, maana hapo sheria zitafuatwa kwa sababu wote wana uwezo, lakini mnyonge anapohusika, ni uonevu.

Na hii ipo mahakama zote, nchi nzima kwa kesi za aina zote. Matajiri na wakubwa serikalini huwabambikia kesi watu waliokosana nao, wanaochukuliana mabwana au mabibi mitaani na kwa nguvu zao, wengi wanafungwa.

 

 

No comments