FBI yaonya kuhusu jasusi wa Iran anayedaiwa kupanga njama ya kuwaua maafisa wa Marekani
FBI inamsaka mtu anayedaiwa kuwa jasusi wa Iran ambaye inaamini anahusika katika njama za kuwaua maafisa wa sasa na wa zamani wa serikali ya Marekani.
Shirika hilo linamtuhumu Majid Farahani, 42, kwa kupanga njama ya kulipiza kisasi mauaji ya jenerali wa Iran Qasem Soleimani.
Soleimani, kamanda wa kikosi cha Quds cha Iran, aliuawa katika shambulio la ndege isiyo na rubani ya Marekani nchini Iraq mnamo Januari 2020.
FBI inasema Bw Farahani amechukua hatua kwa niaba ya Wizara ya Ujasusi ya Iran.
Katika notisi iliyotumwa Ijumaa, FBI ilisema inamtaka Majid Dastjani Farahani kuhojiwa kuhusiana na kuajiri watu binafsi kwa ajili ya operesheni nchini Marekani.
Maafisa wanasema Bw Farahani husafiri kati ya Iran na Venezuela na pia amewaajiri washirika kwa "shughuli za uchunguzi zinazolenga maeneo ya kidini, biashara na vituo vingine" nchini Marekani.
Mnamo Desemba 2023, Bw Farahani na afisa mwingine anayedaiwa kuwa wa ujasusi waliwekewa vikwazo na hazina ya Marekani.
BBC imewasiliana na maafisa wa Iran huko Washington na New York kwa maoni.
Maafisa wa Iran wameapa kulipiza kisasi kwa mauaji ya Soleimani, ambaye alionekana na watu wengi kama mtu wa pili kwa nguvu zaidi nchini Iran wakati wa kifo chake. Aliuawa katika uwanja wa ndege wa Baghdad pamoja na Wairani wengine kadhaa kwa amri ya Rais wa wakati huo Donald Trump.
Kikosi cha Quds ambacho Soleimani alikiongoza ni tawi la Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ambalo limebobea katika vita visivyo vya kawaida na ujasusi wa kijeshi.
Inafanya kazi nje ya Iran na kuunga mkono vikundi vikiwemo Hamas, Hezbollah na Houthis nchini Yemen. Marekani inaichukulia jeshi la Quds kuwa ni kundi la kigaidi.
bbc

Post a Comment