Familia yabomolewa nyumba kibabe, kesi ilikuwa mahakamani, OCD amlinda, Mwenyekiti wa Mtaa amkana, Tibaijuka atajwa
MKAZI mmoja wa mtaa wa Kihonzile, Bunju B
wilayani Kinondoni jijini Dar es Salaam, Charles Forodha amevunjiwa nyumba yake
mchana kweupe na mtu ambaye inadaiwa ni tajiri yake, aliyemzawadia kiwanja
miaka kumi iliyopita.
Forodha aliiambia Ojuku Blog kuwa kwa zaidi ya
miaka 20, alifanya kazi kama mlinzi wa eneo (shamba) la tajiri yake aliyemtaja
kwa jina la Diana Alex Tibaijuka na mwaka 2014, alimkatia eneo pembeni la
shamba lake, akimwambia kuwa ni zawadi kwa mtoto wake (Forodha) aitwaye Joyce, aliyekuwa
na umri wa miaka nane wakati huo.
“Alisema ananikatia kiwanja hicho ili nijenge
nyumba, niipangishe ili kodi yake iweze kumsomesha mwanangu. Alisema kiwanja
hicho ni cha mtoto wangu lakini kwa kuwa alikuwa na umri mdogo wakati huo,
hakuweza kuwandiwa hati. Kwa hiyo mimi na mke wangu tukaanza ujenzi kidogo
kidogo hadi nyumba ikakamilika baada ya miaka mingi,” alisema Forodha ambaye
kutokana na hali yake kuwa katika hali ya kuchanganyikiwa, aliomba maelezo
zaidi yatolewe na mke wake.
Mkewe, Rose Forodha alisema kwa kipindi chote
hicho walikuwa na uhusiano mzuri, lakini hali ilikuja kubadilika baada ya yeye
(Rose) kumtaka tajiri wao (Diana) alipe deni ambalo yeye alimkopea kwa mtu.
“Kuna mtu nafahamiana naye vizuri, ana duka la
Hardware (vifaa vya ujenzi), sasa akawa ananiambia nimkopee na mimi kwa kuwa
namfahamu ni mtu mwenye uwezo, nikawa nakopa lakini deni likawa kubwa, mwenyewe
akawa anataka hela yake, nilipomwambia ndipo hali ilipoanza kubadilika.
“Kwanza alitutaka tuondoe paa ambalo alisema
linamwaga maji upande wake, tukalazimika kupandisha paa letu juu ili kuzuia
maji ya mvua kuangukia upande wake. Baadaye akaja akajenga ukuta kutuziba
kabisa upande tulioweka madirisha kwa ajili ya kupata hewa. Tukaenda serikali
ya mtaa wakamwambia avunje ule ukuta lakini akakataa.
“Badala yake akaanzisha kesi, lakini sisi
hatukuwahi kuitwa huko mahakamani. Yaani kesi ya upande mmoja hadi akaja tu
kutuambia ameshinda kesi. Ikabidi tumtafute mwanasheria wa kutusaidia,
alipofuatilia ndiyo ikaonekana alitushtaki sisi kama wakimbizi wakati kiwanja
alitupatia mwenyewe, tena mbele ya mashahidi wengi tu.
“Sasa wakili wetu akakata rufaa Mahakama Kuu na
hivi hapa tunasubiri siku ya kesi tuitwe, lakini tunashangaa leo ghafla amekuja
hapa na mabaunsa na polisi wa Mabwapande wamesimamia. Tumewaomba karatasi za
kuonyesha kwamba wameruhusiwa na mahakama hawatuonyeshi. Wanasema tu huyu
anayesimamia zoezi ni dalali wa mahakama. (Analia).
Akizungumza kwa shida huku akilia, mama huyo
alisema alijaribu kuwaomba wabomoaji hao wampe nafasi japo ya kutoa vitu vyake
nje lakini wakakataa hali iliyosababisha upotevu wa vitu vyake vingi, ikiwamo
fedha zaidi ya shilingi milioni nne zilizokuwa ndani kwake.
“Mimi nachezesha michezo ya wanawake na ninakaa
na hela za watu maana nina vikundi vingi, pesa zangu zimepotea, vitu vyangu
vimevunjwa hovyo na vitu vingine vimepotea kusikojulikana. Sijui hata nitafanya
nini mimi,” alisema mwanamke huyo.
Alisema mwanamke huyo anajivunia dada yake aliyemtaja
kuwa ni Anna Tibaijuka, aliyewahi kuwa Waziri siku za nyuma.
“Anajivunia huyo dada yake, anasema yeye ana
hela na hatuwezi kumfanya kitu maana serikali ipo mikononi mwake. Hapa hata
akiitwa ofisi za serikali ya mtaa haendi, anasema hadhi yake si ya kuitwa na
ofisi kama hiyo. Hapa mtaani anagombana na kila mtu. Kuna siku wale watu
waliokuwa wanamdai walimkamata na kumweka ndani, akaja huyo dada yake akamlipia
na akatoka, toka siku hiyo hatunywi maji,” alisema.
MSIKIE
MWENYEKITI WA SERIKALI YA MTAA
Ojuku Blog ilizungumza na Mwenyekiti wa Serikali
ya Mtaa wa Kihonzile, Hassan Mnondwa alisema yeye ni mkazi wa mtaa huo kwa
miaka mingi na anafahamu kuhusu familia hiyo kupewa kiwanja hicho miaka ya nyuma.
Alisema anatambua pia kuhusu chanzo cha mgogoro huo na ofisi yao inalifahamu
vyema jambo hilo.
“Mgogoro huu tunafahamu kuwa ulikuwa mahakamani,
juzi nilipigiwa simu na OCD wa Mabwepande akaniambia kama nina taarifa za
nyumba ya mkazi wangu kuvunjwa, nikasema sina taarifa. Lakini cha kushangaza
akasema ofisi yetu inafahamu na kwa hiyo anatuma askari ili waje kushirikiana
na mimi kwenye uvunjaji.
“Nilipomwomba kama kuna nyaraka zozote za
uvunjaji huo akasema tayari zilishasainiwa na mahakama tokea mwezi wa kwanza.
Mimi nikasema sitashiriki zoezi hilo bila kuona nyaraka hizo. Wakaja ofisini
wakanikuta, nikawapa msimamo wangu. Wakampigia Mtendaji ambaye aliwaambia
alikuwa njiani, wakamsubiri na alipokuja wakaondoka naye kuja hapa bila mimi
kuona hizo nyaraka,” alisema.
Alipoulizwa kama Mtendaji anaweza kufanya jambo
bila ya kumshirikisha yeye, alidai jambo hilo linawezekana kwa kuwa kila mmoja
ana muhuri wake na anaamini kiongozi huyo ameshiriki zoezi hilo bila
kumshirikisha.
MWANASHERIA NAYE ASHUSHA NONDO ZAKE
Mwanasheria wa familia hiyo, Noelina Bippa
alisema alianza kuisadia familia hiyo baada ya hukumu katika shauri la awali
kuwa limeshahukumiwa, kitendo kilichomlazimu yeye kuomba rufaa ambayo
ilikubaliwa na walikuwa wakisubiri siku ya kusikilizwa.
Alipoulizwa kama wabomoaji wanaweza kutumia
hukumu ya awali kutekeleza walichokifanya, alisema kisheria inawezekana lakini
katika mazingira yafuatayo:
“Hukumu ya awali ingeweza kutekelezwa kama tu
mahakama ingetoa taarifa ya maandishi kwa familia juu ya nia ya kuvunja nyumba
hiyo. Ingeweza kuwa siku 7 au 14. Sasa kama taarifa hiyo ingetolewa, sisi
tungeitumia ili kuomba kusitishwa kwa jambo hilo kwa vile kuna rufaa.
“Nafikiri hawa walijua jambo hili, ndiyo maana
waliamua kuvunja bila notisi jambo ambalo ni kinyume cha sheria. Tutafuatilia
mahakamani ili tuone cha kufanya,” alisema mwanasheria huyo.
Diana Alex Tibaijuka hakuweza kupokea simu kila
alipopigiwa. Blog hii itaendelea kumtafuta ili kupata maelezo ya upende wake.

Post a Comment