Familia iliyovunjiwa nyumba yamlilia Mtendaji wa Mtaa
Na Mwandishi Wetu
FAMILIA ya Charles Forodha, mkazi wa mtaa wa
Kihonzile, Bunju B Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, imemlilia Ofisa
Mtendaji wa mtaa huo, Jackson Mwilima wakimwita msaliti, kwani licha ya kujua
haki yao, aliungana na mtu aliyewavunjia nyumba yao wiki iliyopita.
Akizungumza huku akibubujika machozi nyumbani kwake, mama wa
familia hiyo, Rose Forodha, alisema ofisi ya mtaa ilikuwa inafahamu kila kitu
kuhusu mgogoro uliokuwepo kati yao na jirani yao, ambaye ni tajiri wa baba wa
familia hiyo aitwaye Diana Alex Kajumulo.
“Huyu mama alitupatia hiki kiwanja kama zawadi kwa binti yetu
wakati huo akiwa mdogo baada ya mume wangu kuwa amefanya kazi ya kumlindia hili
shamba kwa zaidi ya miaka 20, lakini ghafla tukashangaa anaanza kusema sisi ni
wavamizi. Majirani wanafahamu kuhusu jambo hili na tulienda serikali ya mtaa
tukashinda hili shauri.
“Akaanza chokochoko. Kwanza akajenga ukuta ambao uliziba kabisa madirisha ya nyumba yetu. Tukaenda ofisi ya serikali ya mtaa kulalamika akaamriwa abomoe. Mwenyekiti wa Mtaa na Ofisa Mtendaji walikuwa upande wetu kwa sababu wote wanajua jinsi tulivyokipata kiwanja hiki.
“Baadaye sijui nini kilitokea, yule Ofisa Mtendaji akahamishwa.
Ndipo akaletwa huyu mtendaji ambaye tangu amekuja, tunaona yupo upande wa huyu
mama, wakati hata hajui historia ya jambo hili. Amekataa kushirikiana na
Mwenyekiti wa Mtaa anayefahamu kuhusu jambo hili, yeye hata sijui amepewa nini,”
analalamika mama huyo ambaye katika zoezi la uvunjaji wa nyumba yake, anadai
kupoteza shilingi milioni nne alizokuwa amekusanya kama ‘kijumbe’ kwenye
michezo ya kinamama.
Mama huyo anasema kinachowatia mashaka hadi kuamini kuwa kiongozi
huyo wa serikali alinunuliwa, ni kitendo chake cha kusimamia ubomoaji bila
kujali kwamba familia hiyo haikupewa taarifa kama sheria zinavyotaka na
alikataa katakata kuwaruhusu kutoa mali zao wakati zoezi hilo likiendelea.
“Tulimuuliza mbona sisi hatuna taarifa ya kimaandishi, akawa
hatusikilizi. Hata tulipoomba tupewe muda kidogo wa kutoa vitu vyetu ndani ya
nyumba, alikataa na kuamuru mabaunsa kuendelea kuvunja nyumba yetu huku vitu
vyetu vikivunjwa na vingine kuibiwa na vibaka bila msaada wowote,” alisema mama
huyo.
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa huo wa Kihonzile, Hassan Mnondwa alikiri kutokea kwa tukio hilo na kwamba
yeye ni mkazi wa mtaa huo kwa miaka mingi na anafahamu kuhusu familia hiyo
kupewa kiwanja hicho miaka ya nyuma. Alisema anatambua pia kuhusu chanzo cha
mgogoro huo na ofisi yao inalifahamu vyema jambo hilo.
“Mgogoro huu tunafahamu
kuwa ulikuwa mahakamani, juzi nilipigiwa simu na OCD wa Mabwepande akaniambia
kama nina taarifa za nyumba ya mkazi wangu kuvunjwa, nikasema sina taarifa.
Lakini cha kushangaza akasema ofisi yetu inafahamu na kwa hiyo anatuma askari ili
waje kushirikiana na mimi kwenye uvunjaji.
“Nilipomwomba kama kuna
nyaraka zozote za uvunjaji huo akasema tayari zilishasainiwa na mahakama tokea
mwezi wa kwanza. Mimi nikasema sitashiriki zoezi hilo bila kuona nyaraka hizo.
Wakaja ofisini wakanikuta, nikawapa msimamo wangu. Wakampigia Mtendaji ambaye
aliwaambia alikuwa njiani, wakamsubiri na alipokuja wakaondoka naye kuja hapa
bila mimi kuona hizo nyaraka,” alisema.
Alipoulizwa kama Mtendaji
anaweza kufanya jambo bila ya kumshirikisha yeye, alidai jambo hilo
linawezekana kwa kuwa kila mmoja ana muhuri wake.
Ojuku Blog ilifanikiwa
kumpata Ofisa Mtendaji huyo, Jackson Mwilima kupitia simu yake ya mkononi na
alipoulizwa kuhusu suala hilo alikata simu. Lakini alipotumiwa maswali kupitia
mtandao wa What’sApp, akiulizwa kuhusu kusimamia zoezi hilo la uvunjaji bila
kufuata taratibu ikiwa ni pamoja na tuhuma za kuhongwa na mvunjaji wa nyumba
hiyo, alijibu kuwa asingeweza kujibu kwenye simu na badala yake waandishi
wamfuate ofisini kwake.

Post a Comment