Matapeli waibuka kivingine Facebook, waitumia Unicef

 


BAADA ya watu wengi kubaini mbinu za wizi zinazofanywa na matapeli kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii, sasa wamegundua mbinu mpya kwa kulitumia shirika la kimataifa la kuhudumia watoto (Unicef).

Matapeli hao, wametengeneza jina linalosomeka kama Unicef African Foundation, wakijifanya kutoa fedha kwa watu wenye uhitaji, wajasiriamali na wenye maisha magumu. Fedha zinazotolewa ni shilingi 2,440,000.

Blog hii ilifanya mawasiliano na watu hao, Unicef African Foundation ambao ili kutoa fedha hizo, waliuliza maswali kadhaa, yakiwemo sehemu ulikosikia kuhusu habari zao. Kisha wakataka kujua majina kamili, namba ya simu pamoja na sehemu mtu huyo alipo.

Baada ya hapo, matapeli hao walitutumia ujumbe ufuatao 

Hongera, unastahili kupokea Tsh.2,464,000.00.

Fedha hizi ni kutoka kwa Wakfu wa UNICEF kusaidia watu wetu ambao lazima wawe katika mazingira magumu. Mipango yetu inafadhiliwa na wafadhili binafsi, wakfu, biashara na taasisi. tunatumai unafahamu kuwa ingekugharimu ada ya kuwezesha ya TSH. 61,000.00 ili maelezo yako yaandikwe kwenye mfumo wetu. Hii ni malipo ya mapema kila wakati. Tujulishe ukiwa tayari ili tuendelee.

Blog hii ilifanya mawasiliano na mmoja wa marafiki zake aliyekiri kupokea fedha kutoka kwa watu hao katika akaunti yake ya Facebook, lakini alipoulizwa ukweli wa habari hizo, alikataa katakata na kudaki kuwa watu hao walidukua akaunti yake na hadi wakati huo, alikuwa haipati.

Akasema kuwa amekuwa akipigiwa simu nyingi na watu wanaomfahamu, wakitaka kujua habari hizo, ingawa wengine humpigia baada ya kugundua kuwa wametapeliwa.

Blog hii pia iliingia katika website ya Unicef ambako hakukuwepo na kitu kinachoitwa Unicef African Foundation Limited na hata ilipojaribu kuwasiliana na Unicef Tanzania, haikujibiwa.

Blog hii inaviomba vyombo vinavyohusika kuwatafuta matapeli hao wanaotumia namba ya simu ya airtel iliyosajiliwa Kenya, 254782529454.

Pia inawaomba wananchi wote kutosadiki aina yoyote ya mikopo inayowataka kutanguliza kutoa fedha. Hawa Unicef African Foundation ni matapeli kama matapeli wengine. WAEPUKE!


 

No comments