Elimu bado haijatolewa vya kutosha Uhifadhi wa mazingira
Na Ojuku Abraham
Kwa miaka mingi, nchi imekua ikiendelea
kuathirika taratibu katika sekta ya uhifadhi wa mazingira, kutokana na ukosefu
wa elimu ya kutosha kuhusu jambo hili, hasa kwa ngazi za chini zaidi ambazo ni
familia.
Vyombo vingi vya umma vilivyoundwa kusimamia
mazingira, likiwemo Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira
(NEMC), vimekuwa vikitoa elimu ya uhifadhi wa mazingira katika ngazi kubwa,
hasa kwenye semina, makongamano, warsha na kampeni mbalimbali za muda mfupi.
Mikusanyiko hiyo imekua ikiwakutanisha wataalamu,
watumishi wa umma, waandishi wa habari, watendaji wa Halmashauri za Wilaya na
Miji na mara chache, watendaji wa serikali ngazi za vijiji, vitongoji na kaya.
Ushahidi wa kimazingira unaonyesha kwamba,
kumekuwa na matokeo chanya machache katika maeneo mengi yanayohubiriwa katika
semina na makongamano hayo, hasa kwa vile wengi wa washiriki, siyo watu ambao
wanaguswa moja kwa moja na wajibu wa kuhifadhi na kutunza mazingira.
Vyombo vingi vya umma, ambavyo kimsingi
vilipaswa kuwa mstari wa mbele katika kukabiliana na janga hili, baadhi yao
vimeonekana kuwa sehemu ya tatizo kwenye kampeni nyingi za kuhamasisha utunzaji
wa mazingira.
Kwa mfano, wakati kampeni nyingi zimekuwa
zikielekezwa katika kuelezea ubaya wa ukataji miti ovyo katika misitu asilia na
iliyopandwa, vyombo vya umma vimeendelea kuruhusu magunia kwa magunia ya mikaa
yakiingizwa mijini kwa ajili ya matumizi ya kila siku ya shughuli za
kibinadamu.
Ingawa hakuna takwimu rasmi, lakini upo
uwezekano mkubwa kwamba angalau ekari kadhaa za miti zinakatwa kila siku kwa
ajili ya mkaa pekee Tanzania nzima, kitu ambacho hakiendani na kasi ya upandaji
miti kote nchini.
Ukiacha miti inayokatwa kwa ajili ya
kutengeneza mkaa, lakini pia inakatwa kwenye shughuli zingine za kibinadamu
kama ujenzi wa makazi, miundombinu, samadi za maofisini na majumbani, achilia
mbali misitu inayopotea kutokana na majanga kama vile moto, mafuriko, vimbunga
na kadhalika.
Uharibifu huu wa misitu, hauishii tu katika
kumpa athari binadamu kwa maana ya kukausha vyanzo vya maji na kukaribisha
jangwa, lakini pia huwakuta hadi wanyama, wanaofungwa na wa porini. Vyanzo vya
maji vinapokauka kutokana na shughuli za kibinadamu, husababisha mifugo kukosa
sehemu ya kupata maji ya kunywa.
Hali hii ni bora kwa mifugo ifungwayo, ambayo
wamiliki wao wanaweza kuwatafutia namna nyingine ya kuwapatia maji, lakini
inapotokea kwa wanyama wa porini walio mbugani, huwafanya kuhama kutoka eneo
moja kwenda lingine pasipo utashi wao.
Ushahidi usio shaka unaonyesha jambo hili
linapofanyika, yapo madhara ambayo yametokea, yakimuathiri binadamu. Wanyama
hawa wanaohama kwa kukimbia moto unaowashwa makusudi katika mapori na hifadhi,
huwafanya wanyama hao kwenda karibu na makazi ya watu na kufanya uharibifu wa
mashamba na wakati mwingine hata kujeruhi na kuua wananchi.
Ukiachana na uharibifu wa misitu ambayo
mojawapo ya athari zake ni pamoja na kukauka kwa vyanzo vingi vya maji, lakini
hata mazingira ya kawaida ya jamii ya Kitanzania, yako shaghalabaghala.
Kumekuwa na uduni mkubwa na ukosefu wa elimu juu ya namna bora ya kukabiliana
na changamoto za mazingira tunayoishi, ambayo kwa nyakati tofauti yamesababisha
magonjwa ya mlipuko, uharibifu wa miundombinu na athari zisizoepukika.
Ujenzi wa makazi na miundombinu yake limekuwa
ni tatizo sugu kwa miaka na miaka sasa. Kwa makusudi au kutojua, baadhi ya watu
wamekuwa wakivamia maeneo pasi na kupata baraka kutoka mamlaka zinazohusika,
kitu ambacho husababisha hata ramani za kuweka miundombinu kwa ajili yao kuwa
migumu.
Badala ya wananchi kwenda katika maeneo
yaliyopimwa ambayo ramani zitasomeka vyema ili kurahisisha uwekaji wa
miundombinu, wengi hutanguliza makazi kwanza, kitu ambacho huiwia vigumu
serikali katika kufanikisha kwa ufasaha ujenzi wa barabara, mitaro ya kukinga
maji, usambazaji wa huduma muhimu kama umeme na maji, sehemu za huduma za afya
na hata elimu.
Tumeshuhudia mara kadhaa, migogoro ikijitokeza
kati ya wanakijiji na baadhi ya hifadhi zilizotengwa, ama wananchi wakidai
maeneo hayo ni yao, au wakilazimisha kuingia hifadhini kwa ajili ya kupata
mahitaji ya vitoweo kutoka kwa wanyama pori waliomo ndani yake.
Mara kadhaa, jambo hili limesababisha uhasama
mkubwa baina ya watumishi wa serikali na wanakijiji wanaolizunguka eneo husika.
Kutokana na uhasama huu ambao siyo wa lazima, matokeo yake hifadhi ambazo ni muhimu
kwa maisha ya wote, wanyama na binadamu, huhujumiwa makusudi.
Kama nilivyotangulia kusema kule juu, tatizo
kubwa linalofanya janga hili la ukosefu wa uhifadhi wa mazingira ulio bora, ni
kutokuwepo kwa elimu ya kutosha, hasa kwa kada ya chini zaidi, inayoanzia ngazi
ya familia. Pengine kutokana na gharama au muda, lakini elimu kwa familia ndiyo
muarobaini wa uhakika katika kukabiliana na suala hili.
Kama baba, mama na watoto watatambua ubaya wa
kukata miti ovyo, kutupa taka kiholela na vitu vingine kama hivi vinavyoathiri
mazingira, ni wazi kuwa hawa watu watakuwa walinzi wa kwanza wa kuhakikisha
jambo hili halifanyiki.
Ninafahamu mbinu mbalimbali zimekuwa
zikifanyika ili kuhakikisha elimu inawafikia walengwa, kama vile vipindi katika
redio na televisheni, makala kwenye magazeti na hata kwa kutumia mitandao ya
kijamii. Pamoja na hayo, nina wazo ambalo linaweza kusaidia kusambaza elimu
zaidi kwa familia.
Watumishi wa umma, wenye utaalam na mambo ya
uhifadhi, kama walivyo mabwana na mabibi shamba, kwa kutumia viongozi wa serikali
ngazi za vitongoji na vijiji, wawe na vipindi maalum vya kuelimisha umma kwa
kuzungumza nao ‘live’.
Zoezi hili linaweza kuanza kwenye maeneo ambayo
yapo karibu au kuzunguka sehemu maalum zilizotengwa kama hifadhi, ziwe za
misitu, mapori hengefu au hifadhi za wanyama pori. Hapa ni vyema nikaeleweka.
Jamii iielimishwe na siyo kulazimisha kuelimisha.
Mtu anapaswa kuelezwa kwamba elimu anayopewa ni
kwa faida yake mwenyewe, kwanza kwa ajili ya kulinda mazingira yake ya sasa na
baadaye, kumnufaisha yeye na kizazi chake na pia, nini athari zake endapo hiki
na hilki kitafanyika, iwe kwa jamii au kwa mtu mmoja mmoja, ikiwa ni pamoja na
adhabu ya kisheria kwa wanaokiuka taratibu makusudi.
Elimu hii inapaswa kuanza kwa kuandaa watoa
elimu wenyewe. Tunao wataalam wa nyanja mbalimbali katika hifadhi, lakini
bahati mbaya si walimu wazuri kwa jamii. Tunahitaji mtu anayeweza kuongea
maneno machache ya kueleweka kuliko mtu mwenye Phd, anayeongea misamiati migumu
kwa watu ambao huenda hawajaenda shule kwa ngazi kama yake.

Post a Comment