Kuingia bure kwa sharti la jezi ya Yanga ni batili

 


Sawa. Uamuzi wa bosi Ghalib ni mzuri kwa klabu yake, kwa mashabiki wake na pengine, kwa watu wengi wa mpira. Ule mzunguko pale Uwanja wa Taifa, ndiyo unaobeba mashabiki wengi zaidi kuliko maeneo mengine yote ya kukaa.

Unapozungumzia Uwanja wa kubeba watu 60,000 wakiwa wamekaa, sehemu ile ya MZUNGUKO, inaweza kubeba takribani ya asilimia 80 ya watu hao.

Soka ni mchezo wa mashabiki. Kuna watu wanapenda kuangalia mpira, lakini hawana timu wanayoishabikia, kwao burudani ni soka. Basi.

Kati ya hawa wasio na timu, wengi hukaa eneo hilo la mzunguko. Na tukumbuke, mechi ya kesho kati ya Yanga na Madeama, siyo mali ya miamba hawa wa Jangwani. Hii ni mechi ya CAF.

Yanga kuibeba na kuifanya yao, siyo sawa. Hii si mechi ya Wiki ya Wananchi, ambapo klabu ingeweza kufanya itakavyo.

Unamlazimishaje shabiki wa mpira avae jezi ya klabu kama sharti la kuingia uwanjani?

Mechi hizi zina viingilio, weka kiingilio watu wa mpira waje uwanjani, mtu ashindwe kiingilio. Unataka kusema nini kwa mashabiki wa Madeama waliopo hapa nchini, wavae jezi za Yanga ndipo waingie?

Ni vyema mamlaka zinazohusika zikaingilia kati suala hili.

Ni kweli, mashabiki wengi wa Yanga ndiyo watakaojitokeza, lakini vipi mashabiki wa mpira wanaoshabikia Simba, Coastal, Azam na Namungo?

Nasisitiza, hii siyo mechi ya Bonanza la Yanga, hii ni mechi mali ya CAF, ila Yanga wanachezea nyumbani. TFF, kama mwakilishi wa shirikisho la soka Afrika, fanyeni jambo kwa faida ya mashabiki wote wa mpira!

No comments