BOTSWANA YAKANUSHA KULA NJAMA KUMUUA KIONGOZI WAKE WA ZAMANI

Serikali ya Botswana imepuuzilia mbali madai kwamba inapanga kumkamata na kumuua rais wa zamani aliye uhamishoni Ian Khama iwapo atarejea nyumbani.

Katika mahojiano wiki iliyopita, Khama aliliambia shirika la habari la AFP kwamba alikuwa na taarifa kuhusu mipango ya kumkamata na kumtia sumu alipofika nyumbani kutoka Afrika Kusini, ambako amefukuzwa tangu 2021.

Alidai serikali ya Botswana inahofia ushawishi wake kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Lakini katika taarifa yake siku ya Jumanne, Katibu Mkuu wa mawasiliano William Sentshebeng alipuuzilia mbali madai ya Khama na kusema ni ‘ya kukasirisha na ya kusikitisha.’

"Tunayachukulia madai hayo kuwa yamechochewa kisiasa na kwa nia moja tu ya kuchafua sifa nzuri ya Botswana na serikali yake," Bw Sentshebeng alisema.

Huku uchaguzi ukikaribia mwaka ujao, Khama ameapa kumng'oa mrithi wake Mokgweetsi Masisi, ambaye sasa ni mpinzani mkubwa anayemtuhumu kuwa tishio kwa demokrasia.

Khama alisema anajiandaa kurejea nyumbani kujiunga na vyama vingine ili kuhakikisha kwamba kiongozi wa sasa na chama chake wanashindwa katika uchaguzi.

Kiongozi huyo wa zamani alisema amefanyiwa uchunguzi kamili wa matibabu na kusasisha wosia wake kwa sababu alikuwa na uhakika kwamba ndani ya siku chache baada ya kuwasili atakamatwa.

Khama mwenye umri wa miaka 70, afisa mkuu wa zamani wa kijeshi, alitawala mojawapo ya mataifa ya juu zaidi barani Afrika yanayozalisha almasi kwa muongo mmoja hadi 2018, kabla ya kukabidhi enzi kwa Masisi, ambaye wakati huo alikuwa naibu wake.

Mzozo kati yake na mrithi wake ulianza 2018 wakati Rais Masisi alipoanza kubadili baadhi ya sera kuu zilizopitishwa wakati wa uongozi wa Bw Khama.

Mnamo Januari, Rais Masisi alitia saini makubaliano ya maridhiano lakini ushindani kati ya wawili hao unaendelea.

Mnamo Disemba mwaka jana, Botswana ilitoa hati ya kukamatwa kwa Bw Khama, kwa madai ya kumiliki silaha kinyume cha sheria.

  

No comments