WATOA TIBA KWA VYAKULA WAPIGWA MARUFUKU

SERIKALI imesema watu wanaojiita watoa tiba kwa
kutumia vyakula wanatakiwa kuendesha shughuli hiyo kwa kibali cha Wizara ya
Afya.
Katazo hilo limetolewa na mganga mkuu wa Serikali, Dk Aifello
Sichwale jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu
magonjwa yasiyoambukiza ambayo baadhi amesema yanatokana na ulaji wa vyakula
usiofaa.
Dk Sichwale amesema kumeibuka wimbi kubwa la wanaojiita watoa
tiba mbadala kwa wananchi wakitumia mchanganyiko wa vyakula na hawana utaalamu
wowote.
Amesema siyo dhambi mtu kutoa elimu ya mchanganyiko wa
chakula lakini anapaswa kuwa amepewa kibali na Wizara ya Afya.
“Hatuwezi kuruhusu watu wakaendelea kujitangaza katika mambo
yenye kuhatarisha afya za watu, kama kuna mtu ana uwezo wa kutoa elimu ya
mchanganyiko huo aje kwetu na tutakapojiridhisha kuwa anaweza kusaidia jamii,
tutampa kibali cha kufanya hivyo ili asisumbuliwe,” amesema Dk Sichwale.
Ameeleza sababu za kutoa zuio hilo ni kutokana na kuibuka kwa
magonjwa yasiyoambukiza yanayotokana na ulaji wa vyakula usiofaa chanzo kikiwa
washauri wa mchanganyiko wa chakula.

Post a Comment