MIZANI WATAKIWA KUTOA ELIMU KWA WASAFIRISHAJI WAKATI WOTE

 

Naibu Waziri wa Ujenzi  na   Uchukuzi,   Mwita   Waitara,   amewataka Wakala wa Barabara (TANROADS), kukutana na wadau wa usafirishaji mara kwa mara ili kuwaelimisha Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018  zinavyofanya kazi ili kuondoa malalamiko ya mara kwa mara.

Akikagua utendaji kazi wa Mizani ya Nala jijini Dodoma leo, Naibu Waziri Waitara amewataka   wafanyakazi   wa   mizani   kutoa   elimu   kwa   kila   dereva   wa   lori   kila anapokaguliwa   ili   kuepusha   madereva   hao   kuongeza   mizigo   njiani   na kusababisha usumbufu kwa wamiliki wa malori na lawama kwa wafanyakazi wa mizani.

“Hakikisheni mnapopima magari mnawaeleza uzito uliopo na ni nini anastahili dereva kufanya ili kuepuka kuzidisha uzito na kuharibu barabara”, amesisitiza Naibu Waziri huyo.

Akiwa   katika   mizani   hiyo   Naibu   Waziri   Waitara   ameshuhudia   baadhi   ya madereva   wa   malori   kukiri   kuongeza   mizigo   ya   ziada   na   hivyo   kukamatwa kutokana na kuzidisha uzito hali ambayo inasababisha usumbufu kwa wamiliki.

Amewataka wasimamizi wa mizani kote nchini kuhakikisha kwamba  abiria wa mabasi yaliyozidisha uzito hawapati usumbufu wanapokuwa safarini kwa makosa ya madereva.

Aidha, amewasisitiza watumishi wa mizani kuhusu umuhimu wa kutenda  haki kwa magari yote yanayozidisha uzito ili kuondoa malalamiko na upendeleo.

Naye,   Kaimu   Meneja   wa   TANROADS,   Mkoa   wa   Dodoma,   Mhandisi   Salehe Juma,   amesema   magari   mengi   yanayotozwa   faini   yanatokana   na   ukaidi   wa madereva wenyewe kutotoa taarifa kwa wamiliki pindi wanapokamatwa kwa kosa la kuzidisha uzito kwani sheria inatoa fursa kwa magari kukaa siku tatu bila ya kuchajiwa kwa ajili ya kupunguza mizigo iliyozidi.

Naibu Waziri huyo alikuwa kwenye ziara ya kukagua changamoto zinazoikabili Kitengo cha Mizani ikiwa ni muendelezo wa mkakati wa Wizara kujenga taswira njema katika huduma ya usafirishaji wa mizigo ndani na nje ya nchi.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

 

No comments