JAMII: KWA NINI NDUGU HAWATAKIANI MEMA KULIKO WATU BAKI?

NDUGU ni nani?
Laweza kuwa swali gumu kama utataka kulipa tafsiri kwa upana wake, lakini kwa
lugha nyepesi na ya kueleweka haraka, hapa tunamzungumzia mtu uliyezaliwa naye
damu moja.
Na damu moja nayo
ni tafsiri pana vilevile, lakini angalau inafahamika kuwa huenda ni jamii moja,
ukoo mmoja au familia moja.
Kwa mfano, mimi
simfahamu babu wa babu yangu, lakini naufahamu ukoo wetu unaoanzia kwa babu wa
baba yangu. Babu huyu wa baba alizaa watoto kwa mama wanne tofauti na watoto
wake hao ndiyo wakawazaa baba na shangazi zetu ambao nao walituzaa sisi ambao
sasa nasi tuna watoto!
Kwa hiyo ndugu si
lazima uzaliwe naye tumbo moja, mnaweza kuwa mnatoka jamii au ukoo mmoja.
Lakini kuna nyakati pia hata ndugu wa tumbo moja, huombeana mabaya!
Kwa nini?
Kutokana na uzoefu
wangu wa maisha ya kujichanganya na kuishi sehemu mbalimbali za nchi ambako
nimekutana na watu wa namna tofauti, kitu cha dhahiri nilichogundua ni kuwa
watu wachache sana wanandugu hupendana kwa dhati ya moyo.
Wengi wetu huishi
na ndugu wa namna hii kwa namna ya kuviziana, kila mmoja akiombea mwenzake
atende mabaya ili apate sababu ya kumsema kwa ndugu wengine.
Kwa mfano, ndugu
mmoja atatangulia kuanzisha maisha mjini, tuseme Dar es Salaam na wenzake
wakajua. Kwa vile tunafahamu kuwa Dar ni sehemu ya fursa, wengi watapenda kuja
wakiamini wakifika watafikia kwa ndugu yao, hasa kama amefanikiwa angalau
kidogo.
Ndugu atakapofika
hapo, tuseme labda ni mtoto wa shangazi, mjomba, baba mdogo, baba mkubwa, mama
mkubwa, mama mdogo na ye yote wa namna hiyo, atajieleza kuwa amekuja mjini japo
apate kibarua chochote cha kufanya ambacho kitaweza kumsaidia kupata fedha kwa
ajili yake na ikibidi kwa ajili ya ndugu zake wengine aliowaacha nyuma
kijijini.
Kikawaida, ndugu
yule wa mjini atajitahidi kutafuta fursa kwa ajili ya ndugu zake, ama kwa
kuwaomba marafiki zake wamsaidie kutafuta sehemu ya kujishikiza au kama ana
shughuli zake, basi atamuweka amsaidie huku akimlipa kidogo.
Kwa mfano ndugu
akiwa na duka, genge, shamba au gereji, atamuweka huyo nduguye. Hapo kuna
kuviziana baina yao, kila mmoja anamuomba Mungu nduguye akosee. Yule
aliyemkaribisha, ataombea mwenzake aharibu kazi ili apate sababu ya kumfukuza
au kumsimanga na aliyesaidiwa atasubiri asimangwe bila kosa ili apate sababu.
Ikitokea
wamekwaruzana, kila mmoja atakimbilia kwa ndugu na kulalamika. Huyu kanifanya
hivi, yule kanifanya hivi, ili mradi kila mmoja atajaribu kuonyesha jinsi
ambavyo nduguye asivyo mtu mzuri.
Pamoja na kwamba
binadamu tumezaliwa kila mmoja na karma yake, lakini kiasili, kila mmoja anayo
dhambi ya asili, UBINAFSI. Sisi hasa waswahili, ni wabinafsi tunaopenda mambo
mazuri yawe kwetu tu na si kwa wenzetu.
Ingawa ni kweli
kuwa wapo baadhi ya ndugu zetu wenye upendo na sisi kwa kiwango kikubwa, hata
kama wao wamefanikiwa, lakini dhambi hii haiwachepuki.
Binadamu tuna hulka
ya kupenda sifa. Tukiwa katika nafasi ya kusifiwa, hatupendi mwingine pia awe
na sifa kama yetu, yetu tunataka iwe spesho, kubwa na nzuri kuliko za wenzetu.
Katika familia kwa
mfano, aliyefanikiwa hupenda abaki yeye peke yake ili ndugu wote waende kwake
kulia shida, anaamini endapo ndugu mwingine atapata uwezo wa kuwasaidia wengine
kama afanyavyo yeye, hatapata sifa anazozipata hivi sasa.
Hii ndiyo sababu
kubwa ya kuombeana mabaya. Ikitokea kwenye familia wamefanikiwa wawili,
wataanza kupigana vijembe, kila mmoja akitaka aonekane bora kuliko mwenzake
mbele ya familia yao, jambo ambalo kimsingi, linakosa mbolea.
Ukichunguza familia
nyingi zilizokuwa bora huko nyuma kutokana na kufanikiwa kwa mmoja wao, leo zimejaa
ufukara kwa sababu aliyefanikiwa hakutaka kutengeneza mafanikio kwa wenzake,
aling'ang'ania kubaki peke yake ili aonekane ndiye Mungu wa familia.
Sasa angalia
familia zile ambazo mmoja aliyefanikiwa, aliwavuta na kuwawezesha wenzake nao
kupata mafanikio. Maisha yao yameendelea kuwa bora kwa sababu katika matatizo,
badala ya wote kumtegemea mtu mmoja, sasa wanashirkiana kulikabili tatizo,
kiasi kwamba hata mchango wao huonekana mdogo kwa kuangalia mafanikio yao.
Mtu, yaasi sisi
waswahili, hata akipata 'mchongo' wa hela nyingi kwa mfano, yupo tayari kumpa
mtu baki kuliko ndugu yake. Anaamini ndugu yake akipata mchongo kisha akapata
fedha nyingi, atajidai na kumdharau.
Lakini je, dhana
hii ina ukweli kiasi gani? Zipo baadhi ya nyakati zinathibitisha kuwa ndugu
wengi waliokuja kufanikiwa kupitia kubebwa na ndugu, baadaye waligeuka na kuwa
maadui. Wakati mwingine hata kudai waliowasaidia wanawaonea wivu.
Ingawa pia ni kweli
kwamba baadhi ya ndugu waliowapokea wenzao hapa mjini, wakiona waliyemsaidia
amefanikiwa, huanza kumtafuta kwa maneno ya chinichini, ili mradi tu kuonyesha
bila wao, huyo mtu asingepata mafanikio aliyopata.
Makosa yote haya
husababisha chuki baina ya ndugu na hivyo kuzalisha dhana mpya iliyowakaa watu
wengi kwamba ni heri umsaidie mtu baki atakuheshimu kuliko ndugu.
Hata hivyo, kitu
kimoja cha msingi ambacho wote tunapaswa kukielewa ni kuwa kiasili, wote tuna
ubinafsi. Hii ni dhambi ya kuzaliwa nayo, kila mtu anayo. Leo hii tutamlilia
ndugu yetu aliyetangulia mbele za haki na wengine hujikuta hata wakisema Mungu
ni bora ungenichukua mimi ungemuacha yeye!
Lakini kama Mungu
angekuwa anataka kututenda, angeweza kuibuka na kutushika mikono kwamba twende
badala ya marehemu, hakika wengi wangekimbia.
Kuishi na dhambi
hii, haikufanyi uwe na roho mbaya kwa ndugu yako. Kuna ule msemo usemao tenda
wema nenda zako. Usitoe kwa mategemeo ya kulipwa, wewe timiza jukumu lako,
matokeo anayajua Mungu.
Ninaamini kama kuna
mtu mmoja amefanikiwa kwenye familia, akimuwezesha mmoja naye akafanikiwa,
wawili hawa wana uwezo wa kuwawezesha wenzao kiasi kwamba baada ya miaka
michache, ndugu wote mtakuwa na uwezo wa kuweza kusaidiana.
Utataka sifa kwa
kuwa ndiye uliyefanikiwa peke yako, lakini unasahau jinsi unavyorudi nyuma kimaendeleo
kwa sababu shida zote za familia au ukoo unalazimika kuzitatua wewe peke yako.
Hii inaenda hadi
kwa wazazi, baba ni tajiri kwa miaka mingi, lakini akifa tu na mali zinaanza
kukimbia, kwa nini? Baba hakutaka kuwafundisha watoto namna ya kutafuta na
kulinda mali tangu akiwa hai, angewafundisha na kuwasimamia, leo hii
wasingeyumba!

Post a Comment