WAITARA AZITAKA TAASISI ZA MIUNDOMBINU KUSHIRIKIANA KATIKA UJENZI WA MIUNDOMBINU
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya B & F Global, Bw. Bruno Kinyaga
akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari katika kongamano la tatu la
ustahimilivu wa miundombinu linaloendelea jijini Dar es Salaam.
NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe. Mwita Waitara amesema miundombinu ya barabara, umeme, mawasiliano, maji na reli nchini itadumu kwa muda mrefu ikiwa wajenzi wa miundombinu hiyo watashirikiana wakati wa ujenzi wake.
Akifungua Kongamano la
tatu la Ustahimilivu wa miundombinu jijini Dar es Salaam, Mhe. Waitara amesema
ujenzi wa miundombinu shirikishi ndio suluhisho la miundombinu bora wakati wote.
“Hakikisheni wajenzi wa barabara, reli, umeme, miradi ya maji na mawasiliano mnawasiliana tangu hatua ya mipango ili miundombinu ya aina moja isiharibu miundombinu ya aina nyingine na kuisababishia Serikali gharama zinazojirudia,” amesema Mhe. Waitara.
Amesisitiza kuwa taasisi zinazojenga miundombinu zikishirikiana katika hatua zote zinaweza kujenga miradi yao kwa pamoja na kwa gharama nafuu zaidi na hivyo kuondoa usumbufu na uharibifu wa miundombinu.
“Nawapongeza kwa
kuandaa kongamano hili la wadau wa miundombinu natarajia mtatoka na suluhisho
la kudumu katika ujenzi wa miundombinu na kuipunguzia Serikali gharama kubwa ya
kujenga na kuikarabati mara kwa mara,” amesisitiza Naibu Waziri Waitara.
Mwakilishi wa
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari nchini, Dk. Bonifasi Nobeji amesema ushirikishwaji wa wajenzi wa
miundombinu unachangia ufanisi katika mnyororo wa thamani katika huduma za
uchukuzi na ugavi na hivyo kuisaidia sekta ya bandari kufanya kazi kwa tija.
Kwa upande wake,
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya B & F Global, Bw. Bruno Kinyaga amesema
kongamano hilo la siku tatu linalowaweka pamoja wadau wa miundombinu linalengo
la kupitia changamoto zilizopo sasa na kutafuta suluhu ya sasa na siku zijazo
katika sekta ya miundombinu.
Imetolewa
na Kitengo cha Habari na Mawasiliano Serikalini Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Post a Comment