HERSI HAIJUI HADHI YA YANGA

NILIPATA nafasi ya kusikiliza sehemu ya mahojiano kati ya Mkurugenzi wa Uwekezaji kutoka kampuni ya GSM, Injinia Hersi Said na kituo cha redio cha Efm katika kipindi cha Sports HQ.
Hersi pia ni Mjumbe
wa Kamati ya Utendaji ya Yanga. Alialikwa katika kipindi hicho akiwa kama
kiongozi wa klabu hiyo. Mambo mengi aliyoulizwa alitoa ufafanuzi mzuri sana,
akiongezea hata kuelelzea baadhi ya vitu ambavyo mashabiki wa kawaida ndani ya
timu hiyo, pamoja na watu wengine walikuwa hawajui.
Mambo hayo ni
pamoja na muundo wa klabu baada ya mageuzi makubwa yanayotarajiwa kufanyika,
endapo wanachama wataridhia katika mkutano wao unaotarajiwa kufanyika Juni 27
mwaka huu.
Lakini kuna swali
aliulizwa ambalo majibu yake binafsi kama mdau wa soka, sikutegemea kama
yangetoka kwa mtu anayehubiri mambo makubwa kiasi hicho kwa klabu hiyo yenye
mashabiki wengi zaidi Tanzania.
Hili ni swali
ambalo kila mwandishi anayefuatilia mwenendo wa soka letu na siasa zake,
asingesita kuuliza, once amekutana na Hersi. Aliwaahidi wanayanga kuwa endapo
timu yao itakosa ubingwa msimu huu, waulizwe wao (viongozi, na hasa GSM), je
kwa mwenendo wa lLigi Kuu hadi sasa, anaonaje kuhusiana na kauli yake hiyo?
"Tayari
tumeshachukua ubingwa mmoja, tena mbele ya mtani, Kombe la Mapinduzi. Tuna matumaini
ya kutwaa taji la Ligi Kuu na tupo Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho, bado
tuna nafasi ya kutwaa mataji. Tuna uhakika wa kulitwaa hilo kombe, mshindi kati
ya Azam na Simba tukikutana naye lazima tumfunge."
Kwangu, Yanga bado
ina nafasi ya kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu (ingawa kwa
asilimia ndogo mno) na ule wa FA nafasi kwao ipo, kama ambavyo klabu zote
zilizofikia hatua ya Nusu Fainali zinayo. Yanga, Simba, Azam na Biashara wote
wana nafasi sawa ya kutwaa taji hili.
Lakini ambacho
sijakielewa kwa Hersi ni kulitaja Kombe la Mapinduzi. Kwanza siamini kama
aliposema Yanga ikikosa ubingwa msimu huu waulizwe wao, alimaanisha makombe
mengine zaidi ya lile la Ligi Kuu. Hakika, hadi hapo itakavyokuwa vinginevyo,
ninaamini mamia ya mashabiki wa soka kote nchini waliamini alimaanisha VPL!
Silidharau Kombe la
Mapinduzi, ni kombe lenye hadhi kutokana na umuhimu wa siku hiyo kwa wananchi
wa Tanzania. Lakini tunapokuja kumaanisha katika soka la ushindani ndani ya nchi
hii, michuano ile ni kama bonanza tu, kama ambavyo huko nyuma tumewahi kuwa na
michuano kama ya CCM Cup, Jengo Cup, Hedex Cup na mengineyo.
Mshindi wa michuano
hii haendi popote katika michuano ya kimataifa. Unapokuwa kiongozi wa timu kama
Yanga, unapozungumza kuhusu kutwaa mataji, unamaanisha yale yatakayoifanya
klabu kushiriki mashindano ya kimataifa. Kulitaja kombe la Mapinduzi kama moja
ya makombe ya klabu kujivunia, ni kutofahamu hadhi ya klabu ya Yanga. Yanga ya
kushangilia makombe ya Bonanza?
Katika soka la nchi
hii, Yanga inajisikia fahari zaidi kuweka rekodi ya kuifunga Simba. Ushindi
dhidi ya Simba una hadhi kubwa kwa Yanga kuliko kubeba Kombe la Mapinduzi!
Pengine alikuwa
anajaribu kulifanya suala la kukosa ubingwa wa Ligi Kuu lionekane dogo, la
kawaida, kwani kama ubingwa tayari wanao!
Ninajua mashabiki
wa kweli wa soka, wakiwemo wengi wa Yanga, wanaamini timu yao haiwezi kutwaa
taji la Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.

Post a Comment